SIFA NANE ZA MUME MWEMA:

Na Mtumishi Peter Mabula.
BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU aliye hai.

Wakolosai 3:19 '' Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao.''

Ni mara nyingi sana mabinti au wanawake wameniuliza kwamba watamjuaje mume mwema?
Nimewajibu nilioweza kuwajibu lakini nimegundua kwamba hili ni tatizo Kubwa sana kwa walio wengi.
Kipimo cha mke mwema au mume mwema ni kipimo cha kiroho na wala sio cha kimwili.

Wanaotaka Kuoa/kuolewa Wengi Husema Wanahitaji Mchumba Mwenye Hofu Ya MUNGU. 
Ni Vizuri, Lakini Kwanza Hakikisha Wewe Una Hofu Ya MUNGU Ndipo Umuhitaji Mchumba Mwenye Hofu Ya MUNGU. 
Sio Wewe Huna Hofu Ya MUNGU Kisha Unataka Mwenye Hofu Ya MUNGU. 
Haviendani Hata Kidogo, Na Dalili Moja Ndogo Ya Mtu Kutokuwa Na Hofu Ya MUNGU Ni Kutokutoa Fungu La Kumi, Dalili Nyingine Ni Kutaka Ngono Wakati Wa Uchumba, Dalili Nyingine Ni Kutokudhuria Ibada Na Dalili Kuu Ni Dhambi. Je, Wewe Una Hofu Ya MUNGU Hata Uwe Na Haki Ya Kumpata Mchumba Mwenye Hofu Ya MUNGU? 
Biblia inasema mkioana hamtakiwi kuachana.
Hakuna talaka katika ndoa za wakristo.
Kama unampango wa kutoa talaka au kuomba talaka nakuomba ujue pia kwamba hayo ni machukizo kwa MUNGU.
Ukimwacha mke wako au mume wako kule utakakokwenda kuolewa au kuoa utakuwa unazini tu na kuzini ni machukizo mbele za MUNGU na hakuna mbinguni ya mzinifu hata mmoja.

 1 Kor 7:11 '' lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe. ''

Kwa sababu tumeitwa katika imani ya KRISTO ili tuishi maisha matakatifu na baada ya kumaliza siku zetu za kuishi tuende mbinguni aliko BWANA YESU.

 Baada ya kusema hayo hapo juu naomba sasa nizungumzie sifa za kiroho za mume mwema. Najua kuna mtu atauliza ''na sifa za mke mwema ni zipi?''
Nimeshazungumzia sana kuhusu mke mwema alivyo na sifa zake hivyo fungua tu blog yangu ya maisha ya ushindi u-search juu kulia, utaandika somo ulitakalo na utaona  masomo hayo.

Sifa Nane(8) za mume mwema.


1. Ameokoka.

''Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha MUNGU; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu-Waefeso 2:8-9''

=MUNGU ametuita katika Imani ya KRISTO ili tuishi maisha ya hapa duniani na baada ya kumaliza maisha ya hapa duniani twende mbinguni aliko BWANA YESU. Hivyo kwanza kabisa naomba kila mtu aondoe mawazo ya kumpata mume mwema nje na Wokovu Wa BWANA YESU.
=MUNGU hajawahi kumpa mteule wake  yeyote mke/mume mwema kutoka katika watoto wa shetani.
Mtu kama amemkataa YESU na Wokovu wake hakika huyo hayuko katika kundo la mume/mke mwema.

''Amwaminiye Mwana(YESU) yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana(YESU) hataona uzima, bali ghadhabu ya MUNGU inamkalia.-Yohana 3:36''

-Ukiona umepata mume/ mke kutoka kundi la wasio na Wokovu wa BWANA YESU hakika huyo mwenzi wako hajatoka kwa MUNGU bali ametoka katika akili zako mwenyewe.


2. Anamtii KRISTO.

BWANA YESU anasema 

''Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea.-Yohana 15:4-6  ''
 
=Sifa ya pili na muhimu kumjua mume mwema ni kama huyo ndugu anamtii YESU KRISTO.
Kama mtu anamkataa YESU kama BWANA na MWOKOZI wake basi huyo hamtii YESU na kama hamtii YESU huyo ndugu hayuko katika kundi la waenda uzima wa milele maana bila YESU hakuna mwanadamu hata mmoja atakayenenda uzima wa milele.
- Walio wake KRISTO ni wale wanaomtii na wanalitii Neno lake.
-Sasa haiwezekani wewe unamtii KRISTO kisha MUNGU akakupa mume mwema kutoka katika kundi la wapagani, haiwezekani maana MUNGU anajua kabisa kama mume wako atakuwa mpagani ni rahisi sasa mume huyo kukupeleka wewe kwa waganga na wasoma nyota  na wachawi maana yeye bado yuko upande huo.

3. Anawaza Uzima wa milele kabla ya mengine yote.

 1 Yohana 5:11-13 '' Na huu ndio ushuhuda, ya kwamba MUNGU alitupa uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanawe.
 Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa MUNGU hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa MUNGU.'
'


=Mume mwema wako lazima awe anampenda MUNGU zaidi yaanavyokupemda wewe.
-Lazima awe Hakutendeshi dhambi si kwa sababu anakupenda bali ni kwa sababu anamheshimu MUNGU wa mbinguni.
-Kama mume huyo ni mtu anayeudharau uzima wa milele hakika huyo itakuwa rahisi pia kukufanya na wewe uudharau uzima wa milele na uukose, hivyo MUNGU hawezi kukupa mume kutoka katika kundi la waasi mbele zake.

4. Anampenda mke wake kama nafsi yake.

Waefeso 5:28'' Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe.'' 

=Ni vigumu sana kumjua huyo mchumba wako kama hana pendo wa kweli kwako wakati wa uchumba, lakini ukienda kiroho hakika utabaini tu kwamba huyo sio mume mwema wako.
-Sio kwa sababu anakuandikia meseji za mapenzi kila siku mara tatu kwa siku ndio ujue ni mume mwema, bali unatakiwa uombe na ukiweza unaweza kuwashirikisha watu wengine wanaomjua kwa kina walio waombaji waaminifu watakushauri.
-Sio kwa sababu kila ukiomba pesa anakupa ndipo useme kwamba huyo ni mume mwema, hapana inabidi uende kiroho ndipo utajua kwamba hakika huyo ndugu ni mume mwema wako.
MUNGU ametupa ROHO MTAKATIFU Sisi wateule wake hivyo kama wewe kweli umesimama katika imani na unaongozwa na  ROHO na sio mwili hakika ni rahisi sana kumjua huyo mchumba wako kama ni kutoka kwa BWANA au la.

5. Yale asiyopenda yeye kutendewa na yeye hawezi kumtendea mwenzi wake.

Waefeso 5:29 ''Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama KRISTO naye anavyolitendea Kanisa. ''

=Kama mchumba wako huyo hataki kupata ukimwi kwa sababu ya uzinzi mtakaoufanya basi na yeye asikutendee wewe hivyo kwa kukuambia kwamba mfanye mapenzi wakati hamjaoana, huo ni mfano lakini dalili mojawapo ya kumjua kwamba huyo mchumba sio ni pale atakapotaka ngono wakati nyie ni wachumba tu, ukiona hivyo achana nae na omba MUNGU atakupa aliye sahihi.
-Kama hupendi kutukanwa hakika na wewe hutatukana wengine, -kama hupendi kudhalilishwa hakika na wewe hutataka kudhalilisha wengine.
Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake hivyo mume mwema humpenda mkewe kama anavyojipenda yeye.

6. Ana nia ya KRISTO ndani yake.

 Wakolosai 3:15 ''Na amani ya KRISTO iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani.'' 

Kama kuna kitu muhimu sana basi ni nia ya KRISTO.
Amani ya KRISTO ndio huamua ndani yetu hata tunamjua mtu mwenye nia ya KRISTO haraka sana.
Binafsi kwangu ni rahisi sana kumjua mtu mwenye nia ya KRISTO kama nikiabudu naye mara moja au mara mbili tu.
Makanisani  sio wote ni waenda mbinguni bali wengine wameingia makanisani ili tu wapate wake au waume kisha warudi duniani. Sasa mume mwema hatoki katika tu kundi la wanaoimba au wanaohubiri bali mume mwema ni yule mwenye nia ya KRISTO ndani yake.
=Nia ni dhamira ya kutaka kukamilisha jambo.
Sasa tumempokea YESU KRISTO ili tuwe na sehemu katika uzima wake wa milele. Kama hatutakuwa na nia ya KRISTO ndani yetu hakika hatutakuwa na lengo la kwenda uzima wa milele. 
Sasa mtu mwenye lengo la kwenda uzima wa milele huyo ni mtu muhimu sana na anafaa kuwa mume mwema.

7. Anamsaidia mwenzi wake ili wote wawili waurithi Uzima wa milele katika KTISTO.

1 Petro 1:14-15 '' Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu. '' 

-Kama mchumba wako hakusaidii katika kutenda matendo mema hakika huyo sio mume/mke mwema.
Kama mchumba wako anakushauri kwenda bar kulewa hakika huyo achana naye kabla ya ndoa.
Kama mchumba wako anakushawishi mwende disko kucheza mziki wa kidunia hakika huyo sio mke/mume mwema na utakiwa uachane nae.

8. Mwelewa, msikivu, mvumilivu na ana upendo wa dhati.

1 Kor 13;4-7 '' Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli;  huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.'' 


=Kama hana upendo huyo hafai maana kwenye ndoa atakuwa mtu wa kukutumia tu kama chombo chake cha starehe huku hana mpango wowote na wewe.
 Naamini kabisa kuna kitu umejifunza, lakini lengo la kwanza la MUNGU ni wewe uokoke. Kama unaishi maisha ya dhambi ndugu nakuomba tubu na okoka.
Kama hujampokea YESU nakuomba umpokee leo na uanze kuanzia leo kuishi maisha matakatifu ya wokovu.
Kama wewe ni mtu wa kanisani lakini maisha yako yamejaa dhambi nakuomba okoka upya na amua kumpendeza MUNGU kuanzia leo.
Kama wewe umegeuza kanisa kama kichako chako cha kuficha uovu wako , nakusihi sana umche MUNGU maana kuna ziwa la moto kwa waovu, lakini pia kuna uzima wa milele kwa wateule wa KRISTO wanaoishi maisha matakatifu.
MUNGU wangu akubariki sana na akupe
ufahamu wa kumjua yeye na Neno lake, akupe
ufahamu wa kuliishi kusudi lake jema kwako.
ubarikiwe sana pia kwa kujifunza masomo
yangu.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
0714252292.
mabula1986@gmail.com
Ubarikiwe sana kwa kusoma somo hili.


Comments