Roho Mtakatifu anavyoongoza wana wa Mungu, kutembea na Mungu katika maeneo mbalimbali ya maisha yao-3

Na Mwl Christopher Mawakasege
Leo tunaendelea  somo hili unaohusu “jinsi Roho Mtakatifu anavyotumia amani ya Kristo ndani yetu ili kutuongoza”.
Wakati mwingine amani hii ya Kristo (Wakolosai 3:15), inajulikana kama “amani ya Mungu” (Wafilipi 4:7). Amani hii ina tabia yake unayohitaji kuifahamu, ili iwe rahisi kuelewa Roho Mtakatifu anapoitumia katika kukuongoza kwenye maisha yako.
Ukisoma mstari huu wa Yohana 14:27 utakuta tabia 6 za amani ya Kristo. Ndani ya mstari huu Yesu alisema hivi: “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo…”
Tabia ya 1: Ikiwa Yesu anaweza “kutuachia” amani yake, ina maana hiyo inaweza “ikabaki” nasi. Na ikiwa inaweza “kuachwa ibaki” nasi, ina maana ya kwamba inaweza “kuondolewa” isibaki nasi!
Tabia ya 2: Ikiwa tunaweza “kupewa” amani hiyo, ina maana pia ya kuwa tunaweza “tusipewe”!
Tabia ya 3: Ikiwa tunaweza “kupewa” amani ya Kristo, ina maana pia ya kwamba inaweza “ikakataliwa” na “isipokelewe” na huyo anayepewa!
Tabia ya 4: Ikiwa tunaweza “kupewa” amani ya Kristo, ina maana tunaweza “kunyang’anywa” pia!
Tabia ya 5: Ikiwa tunaweza “kupewa” amani ya Kristo, ina maana amani hiyo “tulikuwa hatunayo” au “ilikuwa haipo” na kwa hivyo “inaweza kuwepo” mahali ambapo “haikuwepo”!
Tabia ya 6: Ikiwa Yesu “anavyoitoa” amani yake kwa mtu, ni tofauti na ulimwengu “utoavyo” kwa mtu; ina maana “utofauti huo” wa amani “inavyotolewa”, unatusaidia kutofautisha ikiwa amani tuliyoipokea mioyoni mwetu ni amani ya Kristo au ni amani ya ulimwengu!
Kumbuka: Roho Mtakatifu hatumii “amani ya ulimwengu” katika kutuongoza, bali anatumia “amani ya Kristo”!
Hebu soma mstari mwingine huu unaosema hivi: “Akatoka farasi mwingine, mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa” (Ufunuo wa Yohana 6:4).
Mstari huu unatupa kuijua tabia ya 7 ya amani – nayo ni hii: Ikiwa amani inaweza “kuondolewa” na mahali pake pakachukuliwa na “mauti”; ina maana amani hiyo iliyoondolewa inaweza “kurudishwa” eneo ilipoondolewa na kuiondoa mauti iliyokuwepo hapo!
Na kufuatana na mstari huu wa Yohana 14:27, amani “ikiondolewa” moyoni kunaweza kutokea “mfadhaiko” na “hofu”. Na amani hiyo “ikirudishwa” inaondoa mfadhaiko na hofu vilivyochukua nafasi yake ilipoondolewa!
Tusomapo mstari huu wa 2 Petro 1:2 tunapata tabia ya 8 ya amani. Mstari huu unasema hivi: “Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu”.
Ndani ya mstari huu wa 2Petro 1:2 tunaona tabia ya 8 ya amani – nayo ni hii: “Ikiwa amani inaweza “kuongezwa”, ina maana ya kuwa amani hiyo inaweza “kupunguzwa” pia!
Ukizisoma na kuzitafakari tabia hizi za amani kama ifundishavyo biblia, utakuwa umejiweka mahali pazuri pa kuweza kumwelewa Roho Mtakatifu anapoamua kukuongoza kwa kutumia amani ya Kristo.
Hebu tuangalie mifano kadhaa inayofundisha jinsi amani hii ya Kristo inavyotumiwa na Roho Mtakatifu kutuongoza.
Mfano wa 1:
“Kutusaidia KUFANYA MAAMUZI yaliyo sahihi sawasawa na mapenzi ya Mungu katika maisha yetu”.
Wakolosai 3:15 inatuelekeza hivi: “Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu, ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani”.
Hiii ina maana: (i) Tujifunze kuipa nafasi mioyoni mwetu amani hiyo, ili iwe inafanya maamuzi juu ya mambo yanayotuhusu;
(ii) Tujifunze kuisubiri amani ya Kristo ifanye maamuzi mioyoni mwetu juu ya jambo linalotuhusu, HALAFU ndipo sisi tufuate na kuamua juu ya jambo hilo – sawasawa na jinsi amani ya Kristo ilivyoamua juu ya jambo hilo;
(iii) Ukijizoeza kumsubiri Roho Mtakatifu akusaidie kufanya maamuzi moyoni mwako, utajikuta moyoni mwako inakuwa rahisi kutambua “ishara” zake anazokupa na kuzielewa!
(iv) Ukiona unakosa amani, au umenyimwa amani, au amani imeondoka moyoni mwako – juu ya jambo unalotaka kulifanyia maamuzi, hiyo ni ishara inayokueleza ya kuwa:
• “Stop” au usifanye huo uamuzi bali subiri kwanza;
• Na katika kipindi cha kusubiri, omba kwa Mungu juu ya uamuzi huo ili ujue cha kufanya! Hili ni muhimu kwa sababu; kukosa amani moyoni mwako inawezekana kukakupa ujumbe wa Mungu ya kuwa, usichukue/usifanye huo uamuzi maana si mapenzi ya Mungu kwako. Au unapokosa amani haina maana usifanye huo uamuzi, bali inawezekana MUDA unaotaka kufanya huo uamuzi siyo sahihi au siyo mzuri.
• Endelea kuliombea jambo hilo hadi upate amani ndipo ufanye uamuzi. Ukipata amani ina maana Mungu anakuruhusu ufanye huo uamuzi. Ukiendelea kukosa amani ina maana achana na huo uamuzi – usiufanye – kwa kuwa si mapenzi ya Mungu kwa ajili yako!


 Tumekwisha – anza kujifunza jinsi Roho Mtakatifu anavyoweza kutumia “huzuni ya Mungu” na “amani ya Kristo” katika kuongoza watu, ili wayajue mapenzi ya Mungu na kutembea ndani yake.
Leo nataka nikupe ushuhuda unaonihusu mwenyewe jinsi Roho Mtakatifu alivyotumia kwa pamoja – “amani ya Kristo na huzuni ya Mungu” katika kunisaidia kutembea katika mapenzi ya Mungu.
Lengo la kukushirikisha ushuhuda huu ni kutaka ujue ya kuwa Roho Mtakatifu anaweza kutumia “kiashiria” zaidi ya kimoja katika kukusaidia uyajue mapenzi ya Mungu kwenye jambo moja linalokuhusu!
Mwaka wa 1990 nilipokuwa nafanya kazi ya kuajiriwa kwenye ofisi fulani mjini Arusha, nilipokea barua ya mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa kikazi, nchini Switzerland mjini Geneva.Nilipoipokea barua ile na kuisoma, mara moyoni mwangu nikakosa amani! Niliamua kuiombea barua ile, ili nipate msaada wa Roho Mtakatifu, ili nijue namna ya kuujibu ule mwaliko.Kadri nilivyoendelea kuuombea ule mwaliko, hali ya kukosa amani ilikuwa inaongezeka moyoni mwangu; na hata nilipokuwa naifikiria safari ile, nilikuwa najikuta nakosa amani moyoni.
Nilijua ya kuwa kufuatana na Wakolosai 3:15 – amani ya Kristo moyoni mwangu ina jukumu mojawapo la kunisaidia kuamua.
Kwa hiyo ile hali ya kukosa amani, ilikuwa inanipa ujumbe wa Roho Mtakatifu ya kuwa, sitakiwi kuamua kusafiri kwenda kwenye ule mkutano, bali nikae katika maombi ili nipate maelekezo yake zaidi juu ya mwaliko huo.Lakini – kwangu haikuwa rahisi kukataa kwenda, kwa sababu nilialikwa kwa cheo nilichokuwa nacho ili nikaiwakilishe ofisi. Na mimi sikutaka kusema uongo ili kutafuta sababu ya kutokwenda!Nikalazimika kuijibu ile barua na kuukubali ule mwaliko, na kuwataarifu siku nitakayofika huko, ili nipokelewe uwanja wa ndege.Nilipoandika ile barua ya kukubali mwaliko na kuituma, mara moyoni mwangu nikapata huzuni kubwa sana! Nikajaribu kuiombea iondoke – lakini haikuondoka!
Nikamuuliza Mungu maana ya huzuni hiyo moyoni mwangu ilikuwa ina ujumbe gani. Roho Mtakatifu akaweka moyoni mwangu maneno haya ya Mungu: “ratiba za maisha yako zimo mikononi mwangu. Mkutano huo haumo katika ratiba zangu nilizokupangia”.Ndipo nilipojihakikishia ya kuwa haikuwa katika mapenzi ya Mungu kwangu kuhudhuria mkutano ule kwa wakati ule.
Na kufuatana na 2 Wakorintho 7:9,10 ile huzuni niliyokuwa nayo moyoni, ilikuwa ni “huzuni ya Mungu” iliyokuwa inanitaka nitubu na kubadili msimamo wa uamuzi wangu ili nisiende kuhudhuria ule mkutano! La sivyo, ningeng’ang’ania kwenda kuhudhuria mkutano ule, ningepata “hasara” kufuatana na 2 Wakorintho 7:9,10.Kwa hiyo, nilitubu na kubadili uamuzi wangu, na wakati ule ule nikamwomba Mungu aingilie kati, ili anisaidie kushughulika na jambo lile kwenye ngazi ya kiofisi.
Mungu akanisikia na akaingilia kati, na “pasipoti” yangu ya kusafiria iliyokuwa inashughulikiwa na ofisi ili kunitafutia “visa”, ilichelewa kunifikia toka kwenye ubalozi wa Switzerland. Kwa hiyo mkubwa wangu wa kazi akasema niandike barua nyingine iliyosema sitaweza kuhudhuria mkutano ule kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Kwa hiyo sikusafiri. Na hali ya huzuni moyoni mwangu ikaondoka, na nikapata furaha na amani badala yake!
Kwa kukueleza ushuhuda huu, nilitaka ujue jinsi ambavyo Roho Mtakatifu anavyoweza kutumia kwa wakati mmoja uleule, na kwa jambo moja lile lile – “amani ya Kristo na huzuni ya Mungu” kumwongoza mtu ili aweze kutembea katika mapenzi ya Mungu yaliyopangwa kwa ajili yake!
Moyoni mwako kama hujui umuhimu wa kuyajua mapenzi ya Mungu kwa ajili yako na kuyafuata, haitakuwa rahisi kwako kukataa vitu vinavyokuja katika maisha yako, ambavyo kwa jinsi ya mwili vina maslahi kwako!Unapoletewa mwaliko kama nilivyoletewa mimi wakati ule na kulipiwa kila kitu – inakuwa vigumu sana kuukataa! Na wakati mwingine hata huoni umuhimu wa kumuuliza Mungu ili ujue Yeye anasemaje juu ya mwaliko huo – ikiwa uende au usiende!
Mapenzi ya Mungu kwetu yana faida sana kwetu, kuliko mapenzi yetu kwetu yalivyo!Kutaka kujua namna ya kumsikia Mungu na Roho wake, huku moyoni mwako hauko tayari kufuata mapenzi ya Mungu juu yako, yanapotofautiana na mapenzi yako juu yako – ni kupoteza muda wako bure! Tena – kukosa uwezo wa kumsikia Mungu huku unataka kuwa na maisha mazuri – ya kiroho, ya kiakili na ya kimwili – ni sawa na mtu kutaka kuendesha gari ambalo halina usukani – wakati linahitaji usukani ili kuendeshwa ipasavyo!Na kumsikia Mungu halafu hutaki kufanya mapenzi yake juu yako, ni sawa na kuendesha gari lenye usukani, lakini hutaki kutumia njia (barabara) zilizowekwa, wala hutaki kufuata sheria na alama za barabara ipasavyo!
Kumbuka: Kila wakati unahitaji kujitathmini na kujikumbusha sababu (au “motive”) za wewe kutaka kujua Mungu na Roho wake wanavyowaongoza watu katika maisha yao ya kila siku

Comments