SIFA MUHIMU ZA MCHUMBA ANAYEKUFAA WEWE.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.

BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la kutufanya tujue kile kitupasacho kujua.
Nimewahi kuulizwa swali hili zaidi ya mara kumi;
''Je nitamjuaje mchumba kutoka kwa MUNGU?''
''Je nifanyeje ili nijue kama huyu mchumba wangu  ni chaguo la MUNGU kwangu au ni maamuzi yangu tu?''
''Nikitaka kupata Mke mwema/Mume mwema nifanyeje?''
Ni kweli kabisa haya ni moja ya mambo yanayowasumbua sana watu wengi sana.
Wengi hutamani kupata mke mwema lakini wao sio waume wema.
Wengi hutaka sana kupata waume wema lakini wao sio wake wema.
Kuna sifa nyingi ambazo mtu anayetaka kuoa/kuolewa huziangalia kwa huyo mwenzi.

Mithali 19:14 '' Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye; Bali mke mwenye busara, mtu hupewa na BWANA.'' 


Mke mwema au mume mwema hutoka kwa MUNGU hakika.
Lengo la ujumbe wangu nataka ukaone tofauti hizi za kimwili au za kidunia na zile za kiroho. Baada ya kuzijua tofauti hizi basi unatakiwa utambue jinsi ya kubadili msimamo wako juu ya uchaguzi wako ili sasa umpate yule ambaye ana sifa za kiroho maana huyo ndio anastahili kwako.
Lakini pia unapohitaji mke mwema hakikisha wewe kaka unajichunguza kama kweli wewe ni mume mwema hata upewe mke mwema. Je unamcha MUNGU na unatembea katika utakatifu?
Kama dada unamhitaji mume mwema basi hakikisha wewe unafaa kuwa mke mwema kwa maana umeokoka na unaishi kwa kulitii Neno la MUNGU ndipo na wewe upewe mume mwema.

Mithali 19:22-23 '' Haja ya mwanadamu ni hisani yake; Ni afadhali maskini kuliko mwongo. Kumcha BWANA huelekea uhai; Atakaa ameshiba; hatajiliwa na ubaya. ''

Hebu sasa ona tofauti hizi za uchaguzi wa wachumba kulingana na kundi la mtu anayechagua.

=Kijana  wa kiume asiyemcha MUNGU akihitaji mchumba hutaka sifa zifuatazo zote au baadhi ya sifa hizi.

1.  Umbo zuri linalosifiwa na marafiki  zake.
2.  Sura nzuri inayowafanya marafiki zake wamsifie kwamba amepata  kifaa.
3.  Msomi kama yeye.
4.  Anatoka familia nzuri.
5.  Anamjua MUNGU japokua yeye muoaji ni mpagani.
6.  Tabia nzuri japokua yeye muoaji hana tabia nzuri hata moja.
7.  Atembee nae kwanza ili aone kama anafaafaa kumbe ni dhambi na hatari sana ya kuuvunja uchumba kabla hata ya ndoa.

Mithali 31:10 ''Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani. ''

=Binti asiyemcha MUNGU akihitaji mchumba hutaka sifa zifuatazo zote au baadhi ya sifa hizi.

1. Awe na pesa za kutosha zitakazomtosha katika mahitaji yake yote 100%.
2. Humtaka kijana aliyeokoka wakati yeye hajaokoka.
3. Awe Handsome na mchangamfu.
4. Awe na uwezo wa kumlinda hivyo awe na ka mwili kanakoweza kumpiga mtu mwingine kama atamchokoza huyo binti.
5. Awe na kazi nzuri sio tu kazi za ajabu ajabu.
6. Awe na elimu nzuri kuliko wote watakaomfuata.
7. Awe na usafiri au awe na mpango wa kununua usafiri mzuri.

 Waebrania 13:4-6 '' Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi MUNGU atawahukumia adhabu. Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, BWANA ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? ''

=Binti aliyeokoka anapompenda mvulana hupendelea sifa hizi;

1. Awe anamjua MUNGU na ana hofu ya MUNGU.
2. Awe na kazi nzuri na huduma nzuri.
3. Awe na muonekano mzuri na mtanashati.
4. Awe na tabia nzuri na msimamo mzuri
5. Awe na lugha nzuri katika kinywa chake.
6. Awe na historia nzuri ya mwanzo.
7. Awe anakubarika kwa mchungaji.
Isaya 55:8-9 ''Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema BWANA. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.'' 
 
=Kijana wa kiume aliyeokoka sifa anazopendelea kwa binti ni hizi;

1. Awe ameokoka kweli kweli kama yeye.
2. Awe ni mpole, mtii na mnyenyekevu na msikivu na mwelewa.
3. Awe na sura nzuri na muonekano kuwazidi wengine wote kanisani kwao.
4. Awe hana matumizi makubwa sana ya Pesa.
5. Awe anavaa mavazi yenye heshima yanayomstiri.
6. Awe anatoka familia ya wanaojiheshimu hasa dada zake wawe hawajawahi kubebeshwa mimba hovyo hovyo.
7. Awe na upendo wa kweli.
 Yeremia 17:5-7 ''BWANA asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha BWANA. Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea BWANA, Ambaye BWANA ni tumaini lake.''

=Sifa za kiroho za mchumba  anayekufaa wewe unayehitaji mchumba ni hizi;

1. Utii kwa MUNGU na Neno lake(Yakobo 4:7)
2. Awe na nia ya KRISTO ndani yake(Warumi 12:2)
3. Awe na hofu ya MUNGU(Mithali  8:13)
4. Awe Hana cha kumtenga na upendo wa MUNGU ulio katika KRISTO YESU(Warumi 8:35-39)
5. Amfanye KRISTO kuwa namba moja maishani mwake kabla hata ya wazazi au kabla ya huyo mchumba wake( Zaburi 34:8)
6. Awe mwana maombi(Waefeso 6:18)
7. Awe na kiasi na lugha nzuri(1 Petro 1:13-14)
8. Awe anavaa mavazi ya heshima kwa MUNGU na kwa wanadamu(Mathayo 11:8)
9. Awe ni mvumilivu na mkarimu(Yakobo 5:8-9)
10. Awe Mwaminifu kwa MUNGU na kwa wanadamu(Mithali 28:20)


Kama unatafuta mchumba nakuomba mtafute katika sifa za kiroho na sio za kimwili.

Ndugu mmoja alinipigia simu akiomba nimuombee ili apate mwenzi mwema wa ndoa. Akasema anaye mchumba lakini huyo mchumba anamzungusha tu na kumkataa. Nilipotaka kuanza tu kuomba kwa ajili yake akasema ana picha ya huyo mchumba wake hivyo nikiwa naomba yeye atakuwa ameishika. Rohoni sikushuhudiwa kabisa kuhsu huyo wa kwenye picha, niliomba maombi yasiyomhusisha wa kwenye picha maana sikushuhudiwa kuhusu huyo. Baada ya maombi yule ndugu ni kama hakulidhika maana alitamani nikiomba basi niombe kwa ajili ya mchumba wake wa kwenye picha. Wengi huomba wapewe mke mwema au mume mwema wakati wameshachagua kabisa, huwezi ukapata kwa kutumia njia hiyo.

Nimewahi kukutana na vijana wengi wanaohitaji wachumba na sifa zao wanazozitaka kwa wachumba zao ziliniaacha nacheka tu. Kila mtu hutaka kuoa mwanamke mzuri wa sura na mwenye umbo zuri lakini nikiangalia kwenye ndoa nyingi wanawake walioolewa sio wote wazuri sana wa sura wala sio wote wana makalio makubwa au shape nzuri  kwa sababu suala la ndoa ni la kiroho na sio kimwili. Ndio maana ni rahisi tu kumkuta binti mzuri anajiuza wakati kwa muono wa watu wengi huyo binti alitakiwa kuwa katika ndoa yake na sio kwenye uchangudoa.

Rafiki yangu mmoja aliniambia anataka mke mwema kutoka kwa MUNGU ila huyo mke wake mwema ni lazima awe na sifa zifuatazo; Mrefu na ana kazi. Nikamuuliza mbona wanawake wafupi ni wengi tu wako katika ndoa zao?

Je MUNGU akikupa mfupi huku wewe unataka mrefu je utamkataa?

Ninachojua mimi Peter  ni kwamba hakuna mwanaume mbaya duniani na hakuna mwanamke mbaya duniani ndoa maana wanawake wa kila aina wanaolewa na wanaume wa kila aina wanao. Vilema wanaolewa na wanaoa, wanene wanaolewa na wanaoa, wembamba wanaolewa na wanaoa, Wenye macho makubwa wanaoa ana kuolewa,wenye vichwa vikubwa wanaolewa na wanaoa, Waliowahi kuzaa wanaolewa na wanaoa. Kila mtu wa aina yeyote akimuomba MUNGU hakika MUNGU atamba huyo baraka yake ua ndoa. Tatizo tu kuna watu hujilaani wenyewe kutokana na hali zao. Kuna watu hujidharau wenyewe ndio maana hata wachumba huwadharau.

Tatizo tu watu hutaka kwenda kimwili na sio kiroho.

YESU anajibu maombi hakika kwa yeyote ambaye atasimama katika yeye.

Baraka yako ipo tu na hakuna wa kuizuia kama tu ukimtegemea BWANA YESU kwa maombi na utakatifu.

Mwanzo 2:24 '' Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.''
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa BWANA YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
0714252292.
mabula1986@gmail.com
Ubarikiwe sana kwa kusoma somo hili.

Comments