Roho Mtakatifu anavyoongoza wana wa Mungu, kutembea na Mungu katika maeneo mbalimbali ya maisha yao -4

Na Mwalimu Christopher Mwakasege.

Ikiwa umekuwa ukifuatilia somo hili tangu tulipoanza mfululizo wake wa 1 – naamini umekuwa ukipata mafundisho yanayokusaidia kuimarisha uhusiano wako na Mungu katika Kristo Yesu.
Leo nataka tujifunze “jinsi Roho Mtakatifu anavyotumia amani ya Kristo mioyoni mwetu, kutusaidia kuamua ikiwa tumpokee mtu mioyoni mwetu au tusimpokee”.
Je, Mungu akitaka kukushauri ikiwa umpe mtu nafasi moyoni mwako au usimpe anatumia njia ya namna gani?
Njia anazotumia ni nyingi – na mojawapo ni hii ninayokufundisha leo, inayohusu Roho Mtakatifu kutumia amani ya Kristo moyoni mwako.
Somo hili linaweza kukusaidia maamuzi ya mtu wa kuoa, au mtu wa kuolewa naye. Litakusaidia kuamua ni mtu yupi wa kushirikiana naye,au kutoshirikiana naye katika huduma, au katika biashara, au kwenye “mradi”.Na pia somo hili litakusaidia kukupa maamuzi sahihi juu ya nani awe rafiki yako wa karibu, au nani wa kushirikiana naye kukaa chumba kimoja, au nyumba moja.
Njia hii ndiyo iliyomsaidia Rahabu kuwapokea wapelelezi na kuwapa nafasi tofauti moyoni mwake.Biblia inasema: “Kwa imani Rahabu, yule kahaba, hakuangamia pamoja na hao walioasi; kwa kuwa aliwakaribisha wale wapelelezi kwa amani” (Waebrania 11:31). Kufuatana na mstari huu – kuna vitu viwili ambavyo vilimsaidia Rahabu – yule kahaba – navyo ni “imani” na “amani”!“Imani” ilimsaidia asiangamie “pamoja na hao walioasi” kwenye mji wa Yeriko. “Amani” ilimsaidia moyo wake uwe na utayari wa kuwakaribisha “wale wapelelezi” nyumbani kwake.
Nataka ufahamu ya kuwa kilichomsaidia Rahabu kuwapokea watu asiowajua, ni ile “amani” aliyokuwa nayo moyoni mwake, wakati wale wapelelezi wanafika kwake, na kusalimiana naye!
Hii “amani” ilifanya kazi kwa namna gani ndani ya moyo wa Rahabu, ili na sisi iweze kutusaidia juu ya kuchagua nani aliyekuja kwetu – kwenye maisha yetu kwa mapenzi ya Mungu ili tumpokee?Biblia inasema: “Iweni na amani ninyi kwa ninyi”. Hii ina maana ya kwamba “amani” ya kufanana (1 Wathesalonike 5:13) inaweza ikawekwa ndani ya zaidi ya mtu mmoja, ili iwape uhakika wa kuamua jambo kwa kufanana!
Yesu aliwafundisha wanafunzi wake juu ya kutumia “amani” katika kuwasaidia juu ya kuchagua na kuamua nani wa kushirikiana naye, na ni nani si wa kushirikiana naye.Yesu aliwafundisha wanafunzi wake hivi: “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi” (Mathayo 10:12,13)
Maneno ya aina hii kwenye kitabu cha Luka 10:5,6 yanasomeka hivi: “Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu”.
Yesu alitaka wanafunzi wake wajue, na sisi tujue yafuatayo:
(i) Kwamba; ukimsalimia mtu au mtu akikusalimia wewe, angalia hali ya amani yako ndani ya moyo wako – wakati mnasalimiana naye, au baada ya kusalimiana naye – je, unasikia amani moyoni mwako au unasikia kukosa amani moyoni mwako?
(ii) Kwamba; kupata amani moyoni unaposalimiana na mtu maana yake umekubalika moyoni mwake, na anakubalika moyoni mwako. Na kukosa amani moyoni mwako ina maana yake hujakubalika moyoni mwake.
(iii) Kwamba; ikiwa moyoni mwako utasikia kukosa amani, ina maana uwe mwangalifu juu ya maneno utakayosema – ikiwa mazungumzo yataendelea zaidi ya kule kusalimiana
(iv) Kwamba; katika mazingira hayo jizoeze kuombea juu ya maamuzi unayokuwa nayo – hasa unapokutana na mtu mwingine – ili “amani ya Mungu, ipitayo akili zote”, ikuhifadhi “moyo” wako na “nia” yako “katika Kristo Yesu” (Wafilipi 4:6,7).
(v) Kwamba; Kukosa amani moyoni maana yake Roho Mtakatifu anakuangaliza na kusema “keep a safe distance” na mtu huyo! Halafu mwombe Mungu ili akujulishe cha kufanya.
(vi) Kwamba; waitegemee amani hiyo mioyoni mwao katika kujenga, au kutojenga mashirikiano yao na watu wengine. Na wasiangalie mazingira yanayowazunguka wakati wanapokutana na watu wengine – bali waitegemee amani ya Kristo mioyoni mwao. Ukisikia kukosa amani moyoni mwako, ina maana Mungu anakuelekeza kuwa usijenge mahusiano ya karibu na mtu huyo.
Kumbuka: Kilichomsaidia Rahabu (kama tusomavyo katika Waebrania 11:31) kuwapokea watu asiowajua ni “amani” iliyoambatana na “imani” iliyokuwa moyoni mwake, wapelelezi walipofika kwake na kusalimiana naye!
Imani ya Ki – Mungu aliyokuwa nayo Rahabu aliyoipata kwa kusikia (Warumi 10:17, Yoshua 2:8 – 13), na amani aliyoipata moyoni mwake aliposalimiana na wale wapelelezi walipofika nyumbani kwake; vilimsaidia si tu kuwapokea, lakini pia ilimsaidia namna ya kuwapokea – na maneno ya kusema nao.


 nataka nikufundishe njia nyingine anayoitumia.
Njia hiyo ni hii inayohusu Roho Mtakatifu kutumia uhuru wa Kristo moyoni mwako! Biblia inasema “Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli” (Yohana 8:36).Tena – biblia inasema hivi: “Basi ‘Bwana’ ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru” (2 Wakorintho 3:17). Mtu anapookoka huwa moyo wake pia unapokea “uhuru wa Kristo”, ambao huwa unatunzwa na kutumiwa na Roho Mtakatifu katika kumwongoza huyo mtu kutembea katika mapenzi ya Mungu.
Neno “uhuru” lina maana ya: “Kuruhusiwa”, au “kuachiliwa”, au “kuondolewa kilichokuwa kinakuzuia”, au “kupewa kibali cha kufanya jambo”, au “kujisikia uwepesi wa kufanya jambo”. Kinyume cha neno hili “uhuru” utakuta maneno kama haya yafuatayo: “Kufungika”, au “kuzuiwa”, au “kunyimwa kibali”, au “kusikia uzito”, au , au “kukatazwa”
Tena – nataka ujue ya kuwa, “uhuru wa Kristo” ndani ya moyo wa mtu, haufanyi kazi peke yake; bali hufanya kazi pamoja na “kweli” au neno la Kristo (Yohana 17:17) unalolifahamu!
Bila vitu hivi viwili kufanya kazi kwa pamoja, usikivu wa mtu katika kufuata maongozi ya Roho Mtakatifu unakuwa hafifu sana.Hii ina maana mtu anaweza kusikia uhuru moyoni mwake, au akasikia kufungika moyoni mwake – bila kusikia ikiwa ni Roho Mtakatifu anamsemesha au la … kwa sababu “kusikia huja kwa neno la Kristo” (Warumi 10:17).
Hebu tuangalie mifano ifuatayo inayofundisha jinsi Roho Mtakatifu anavyoongoza watu kwa kutumia “uhuru wa Kristo”, ili waweze kutembea na kuishi sawa na mapenzi ya Mungu:
Mfano wa 1: “Mahali pa kuhubiri neno la Mungu”. Njia hii ya kutumia “uhuru wa Kristo” aliwahi kuitumia Roho Mtakatifu katika kuwaongoza mtume Paulo na Timotheo, wajue mahali pa kulihubiri neno la Mungu, na mahali pa kutokuhubiri neno la Mungu.
Biblia inasema: “Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. Walipofika kukabiri Misia wakajaribu kwenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, wakapita Misia wakateremkia Troa (Matendo ya Mitume 16: 6 – 8).
Tunapoutafakari mfano huu – nataka utilie maanani maneno haya – “wakikatazwa na Roho Mtakatifu”, na pia maneno haya – “lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa”.
Nimetaka uyatafakari haya maneno kwa sababu yanatuonyesha ya kuwa Roho Mtakatifu alikuwa anatumia “uhuru wa Kristo” uliokuwa ndani ya mtume Paulo na Timotheo katika kuwaeleza juu ya mapenzi ya Mungu kwao katika kipindi walichokuwa wanapita katika maeneo ya nchi ya “frigia” na “Galatia”, na “Misia” na “Troa”.
Ndani ya mistari ya biblia ya mfano huu tunajifunza yafuatayo:
(i) Kwamba: Akina Paulo na Timotheo waliwekewa mioyoni mwao kusikia “kukatazwa” na “Kunyimwa ruhusa”, ili wajue ya kuwa wameondolewa hali ya kujisikia uhuru moyoni, ili wapate kutambua kuwa haikuwa katika mapenzi ya Mungu kwao kulihubiri neno la Mungu maeneo yale – kwa wakati ule.
(ii) Kwamba: Hata walipokuwa wanafanya maombi ya kuomba “kibali” ili waruhusiwe kwenda kuhubiri Bithinia, - walijisikia mioyoni mwao hali ya “Kutokupewa ruhusa” au “Kutokupewa uhuru” wa kwenda huko!
(iii) Kwamba: Hii ina maana wakati unaomba upewe kibali kwa Mungu cha kufanya jambo au cha kwenda mahali fulani – angalia na tathmini unavyojisikia moyoni mwako. Ikiwa unajisikia “uhuru” wa kwenda ina maana Roho Mtakatifu anakujulisha ya kuwa unaruhusiwa kulifanya hilo jambo kwa kuwa ni mapenzi ya Mungu kwako ulifanye!
(iv) Kwamba: Ikiwa wakati unafanya maombi ili Mungu akupe kibali cha kufanya jambo au cha kwenda mahali na ukajisikia moyoni “kusita”au “kufungika”, au “kukosa uhuru”, au “kujisikia uzito”…ina maana Roho Mtakatifu anakujulisha ya kuwa huruhusiwi kulifanya jambo hilo, kwa kuwa si mapenzi ya Mungu kwako kulifanya!
(v) Kwamba: Ukisikia “kukosa uhuru”moyoni mwako au “kusita” au “kufungika”, huku unasikia mzigo wa kuomba moyoni mwako kwa pamoja …ina maana unatakiwa kuliombea jambo hilo, ili upate ufafanuzi zaidi toka kwa Mungu. Hii ni kwa sababu, inawezekana unakatazwa kwa kuwa huo si muda ambao Mungu amekupangia kulifanya. Muda wa Mungu ukifika, utasikia uhuru moyoni mwako wa kulifanya hilo jambo…kwa hiyo tulia ili usubiri muda wa Bwana kwako!
(vi) Kwamba: Roho Mtakatifu anaweza kuweka ishara ya kufanana, au kiashiria cha kufanana, ndani ya moyo wa mtu zaidi ya mmoja kwa wakati mmoja, ili kuwajulisha jambo hilo hilo moja – kama alivyofanya kwa mtume Paulo na kwa Timotheo katika mfano wao huu tunaoutafakari.
Mungu azidi kukubariki!

Comments