NENO LA CHRISTMAS KUTOKA KWA MWL. MWAKASEGE.

Christopher na Diana Mwakasege
Bwana Yesu Asifiwe!
Ujumbe tulionao kwako " Krismasi" hii ni huu: " Usiwasahau kina Mariamu na Yusufu!"
Baada ya wachungaji wa kondoo kupewa taarifa na malaika, juu ya kuzaliwa kwa Yesu " katika mji wa Daudi; biblia inasema:" wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini"(Luka 2:16).


Hawakumkuta Yesu peke yake, bali walimkuta Yesu akitunzwa na kulindwa na akina "Mariamu na Yusufu"! Pia, "mamajusi wa mashariki" walipoenda kumtazama Yesu, biblia inatueleza ya kuwa hawakumkuta peke yake bali " wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye"(Mathayo 2:11)


Lakini hebu angalia hili:Wachungaji walipomkuta Yesu walifurahi, wakamtukuza Mungu, na wakatangaza habari za kuzaliwa kwa Yesu. Ila hawakutoa sadaka - wala kwa Yesu, na wala kwa Mariamu na Yusufu waliokuwa wanamtunza Yesu? Mamajusi wao walitoa sadaka kwa ajili ya Yesu, lakini hawakutoa sadaka kwa ajili ya wale waliokuwa wanamtunza Yesu yaani akina Mariamu na Yusufu!
Watu wengi huwa wanawasahau,"watunzaji" wa Yesu, au watu wale waliopewa jukumu la "kumtunza" Yesu namna ambayo wale wanaohitaji kumwona, na kupata msaada kwake, waweze kumwona!
Ndiyo maana ujumbe wetu kwako katika "Krismasi" hii ni kukukumbusha "usiwasahau akina Mariamu na Yusufu" waliopewa jukumu la kumbeba Yesu na "kumtunza" ili uweze kumwona na kupata msaada wa Mungu kupitia kwake! Wakumbuke kwa kuwapa sadaka!
Mungu akijua, watumishi wake huwa rahisi kusahaulika, akatoa agizo kwa kinywa cha Musa ya kuwa :....."sadaka......nimempa Haruni kuhani na wanawe, kuwa haki yao ya milele kutoka kwa wana wa Israeli." (Mambo ya Walawi 7:14). Tena alisema;" Jilinde nafsi yako usimwache mlawi siku zote uishizo" ( Kumbukumbu la Torati 12:7).
Tizama na ujue "Yesu" unamwona kwa "nani"? Huyo ndiye "Mariamu" wako au "Yusufu" wako; au "Haruni" wako; au " Mlawi" wako! Pamoja na kumsifu Yesu waliyenayea;usiishie tu kutoa sadaka ya kueneza kazi za Yesu pekee, bali kumbuka kuwapa pia sadaka ya kuwatunza wao ili na wao " wamtunze Yesu" kama jukumu walilopewa Mariamu na Yusufu lilivyokuwa.
Mshirikishe mwingine ujumbe huu! Wewe na hao unaowashirikisha ujumbe huu - muweze kuutendea kazi ipasavyo. Na kwa ye yote atakayewatunza wale wanaomtunza Yesu mioyoni na maishani mwao, ili watu wengine wanufaike kwa kuwepo Yesu maishani mwao......wameahidiwa mengi toka kwa Mungu! Kwa mfano; wameahidiwa:


i) Baraka "katika kazi yote ya mkono" yao waifanyayo ( Kumbukumbu ya Torati 14:24)


ii) Kutokuishiwa wakati wa hali ngumu ya uchumi ( 1Wafalme 17:8-14)


iii) Amani nyumbani ( Luka 10:5-7)


iv) Mungu kuwaonya na kuwaepusha na hila za kina "Herode" wanataka kumwangamiza Yesu aliyewasaidia (Mathayo 2:12,13)


Kwahiyo kumbuka ujumbe wetu kwako "Krismasi" hii tunaokuambia hivi; Usisahau kuwapelekea sadaka akina "Mariamu na Yusufu" waliombeba na kumtunza Yesu anayehusika na maisha yako.
Ni sisi Christopher na Diana Mwakasege, tukiwa na watoto wetu, na wajukuu zetu, na timu nzima ya huduma ya Mana.

Comments