SHIKA SANA WOKOVU ULIONAO ASIJE MTU AKAITWAA TAJI YAKO.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
Bwana YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU.
Bwana YESU ndiye Mfalme wa ufalme wa MUNGU.
Bwana YESU ndiye pekee anayeweza kumpeleka mwanadamu uzima wa milele.
Leo Bwana YESU ana Neno kwako Uliyeokoka ili ushike sana Wokovu asije Mtu akaitwaa taji yako.
Shika sana utakatifu katika yeye ili asije mtu akaitwaa taji yako.
Uking'ang'ania katika Wokovu huku ukiishi maisha matakatifu hakika kuna taji utapewa siku ile akija na taji kuu ni taji ya uzima.
Bwana YESU pia ana Neno juu yako wewe ambaye hujampokea Kama Mwokozi wako ili sasa umpokee na kuanza kuishi maisha matakatifu ya Wokovu wake.
Kwa kinywa chake Bwana YESU anasema leo kwamba ''Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako. Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la MUNGU wangu, wala hatatoka humo tena kabisa, nami nitaandika juu yake jina la MUNGU wangu, na jina la mji wa MUNGU wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa MUNGU wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya. Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo ROHO ayaambia makanisa-Ufunuo 3:11-13''

Ndugu, shika sana utakatifu katika KRISTO asije kaka au dada muovu akakunyang'anya taji yako ya uzima kwa kukushawishi mtende dhambi.
Shika sana wokovu na utakatifu katika KRISTO.
Shika sana Utauwa wako kwa MUNGU Baba ili asije mtu akaitwaa taji yako.
Shika sana ulichonacho kwa YESU asije mtu mwovu akakunyang'anya.
Inawezekana utapitia magumu kidogo katika safari yako ya wokovu lakini hayo magumu yasikufanye ukose uzima wa wa milele, ndio maana Bwana YESU anasema shika sana Wokovu wako na utakatifi ili asije mtu akaitwaa taji yako.
Hata kama una vita au una magumu bado Bwana YESU anasema ''Usiogope mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima.-Ufunuo 2:10''
 
Ndugu ukivumilia hakika kuna uzima wa milele.
Yatupata sana tuvumilie hadi mwisho huku tukiishi maisha matakatifu ya Wokovu wa KRISTO.
Ndugu usikubali Mume/Mke wako akakuondolea uzima wako wa milele.
Usikubali wazazi wako au ndugu zangu wakakuondoa kwa YESU hata ukose uzima wa milele.
Usikubali Mchumba wako akakuondolea utakatifu wako.
Usikubali mabinti wenzako waovu wakakuambukiza uovu wao hata ukamkosea MUNGU.
Usikubali marafiki zako wakakuondolea utakatifu wako kwa Bwana YESU.
Shika sana utakatifu katika Wokovu ili asije muovu akakuondolea taji yako ya uzima.
Hakikisha hakuna mwanadamu yeyote anayekuondolea utakatifu wako kwa MUNGU.
Usikubali kazi yako ikakuondoa kwa YESU KRISTO.
Usikubali ndoa yako ikakuondoa katika kundi la waenda mbinguni, shika sana utakatifu ulionao katika KRISTO ili asije yeyote akakuondolea.
Nakuomba sana ng'ang'ania Utakatifu, wokovu na utii kwa MUNGU maana ukishinda kuna taji isiyokauka baada ya YESU KRISTO kuja kuchukua Kanisa lake.
1 Petro 5:4-11 '' Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka. Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu MUNGU huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa MUNGU ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu. Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani. Na MUNGU wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika KRISTO, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu. Uweza una yeye hata milele na milele. Amina.''

Ndugu nakuomba shika sana ulichonacho asije muovu akakunyang'anya.

VYANZO VYA MTU KUPISHANA NA UZIMA WA MILELE.

1. Kufanya Dhambi bila kutubu na kuziacha.
 
Mithali 28:13 ''Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema. ''
Dawa ya dhambi ni kutubu na kuziacha.
Watu wengi hutubu na kuendelea na dhambi lakini Kanuni ya Biblia ni kutubu na kuziacha dhambi hizio.

2. Kufuata mafundisho ya mashetani yaani mafundisho yaliyo kinyume na Biblia.
 
1 Themotheo 4:1-2 '' Basi ROHO anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe; ''

3. Kufuata mambo ya kidunia yaliyo machukizo kwa MUNGU.
 
1 Yohana 2:15-17 ''Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba(MUNGU) hakumo ndani yake.Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya MUNGU adumu hata milele. ''

4. Kumwacha YESU na Wokovu wake.
2 Yohana 1:7-9 '' Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea duniani, wasiokiri ya kuwa YESU KRISTO yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu na mpinga Kristo. Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu. Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya KRISTO, yeye hana MUNGU. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba(MUNGU) na Mwana(YESU) pia.''
 
Asiyedumu katika mafundisho ya KRISTO huyo hana MUNGU.
Ukimwacha yeye wewe unakuwa umemwacha MUNGU na kwa njia hiyo huwezi kuingia uzima wa milele.
Dawa ni kutubu na kurudi kwa YESU na kuishi maisha matakatifu.

5. Kumkataa ROHO MTAKATIFU na maongozo yake.
 
Warumi 8:14 '' Kwa kuwa wote wanaoongozwa na ROHO wa MUNGU, hao ndio wana wa MUNGU.''
 
Waliookoka hao wana ROHO MTAKATIFU na hao ndio wanatakiwa kuongozwa na ROHO MTAKATIFU.
Ukimkataa ROHO MTAKATIFU maana yake umemkataa MUNGU.
Ukikataa Kuongozwa na ROHO MTAKATIFU maana yake humtaki MUNGU na hutaki kumpendeza MUNGU na kwa njia hiyo huwezi kuingia katika uzima wake wa milele.

6. Kuwawekea tumaini wanadamu na sio MUNGU.
 
Yeremia 17:5-6 '' BWANA asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha BWANA. Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu.''
 
Unaweza ukabishana na uzima wa milele kwa kuwategemea tu wanadamu.
Wanadamu walioanzisha dini zao na madhehebu yao sio wote walikuwa wanamtii KRISTO bali wengine ni ajenda ya shetani na ndio maana hata waliowafuata na kufuata mafundisho yao ya uongo wako kinyume na KRISTO na Biblia, ni hatari sana , ni heri kulitegemea Neno la MUNGU na sio wanadamu.

7. Kumtii shetani na mambo yake yote.
 
Yakobo 4:7-10 '' Basi mtiini MUNGU. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni MUNGU, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za BWANA, naye atawakuza.''
 
Wa kumtii ni MUNGU tu na sio vinginevyo.
Wanadamu wengi leo hata hawamtii MUNGU bali wanamtii shetani.Shetani sio wa kumtii bali ni wa kumpiga.
Wengi leo huabudu mizimu na kumtii shetani, wengi huenda kwa waganga kwa sababu ya kumtii shetani.
Wengi wanatoa mimba kwa sababu ya kumtii shetani.
Wengi huiba na kutoa rushwa.
Wengi huroga na kuwawekea madawa wapendwa wao kwa sababu tu ya kumtii shetani.
Shetani ana mambo mengi sana sana na hayo yote Biblia inatukataza kuyatii wala kuyafuata.
Ni heri kumtii MUNGU Muumba wetu.
Kumtii MUNGU ni kulitii Neno lake Biblia.
Kumtii MUNGU ni kuokoka na kuishi maisha matakatifu.

Ndugu shika sana wokovu na utakatifu asije yeyote akakuondoa kwa YESU.
MUNGU akubariki na pia Ukipenda kunisapoti kwa sadaka katika huduma yangu karibu sana na pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa BWANA YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
0714252292.
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments