USIKUBALI KUKOSA MAARIFA YA MUNGU.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU

Bwana YESU KRISTO atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU.
Watu wengi wanaangamizwa kwa kukosa maarifa ya MUNGU.
Hosea 4:6" Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya MUNGU wako, mimi nami nitawasahau watoto wako."
Maarifa ni nini?
Maarifa ni njia inayotumiwa kujitoa katika shida.
Maarifa ni njia ya kupata kitu.
Maarifa ni Elimu au ujuzi. 
Biblia inazungumza hapo juu kwamba watu wengi wanaangamizwa kwa kukosa maarifa, maarifa yanayozungumzwa hapa ni elimu na ujuzi sahihi wa Neno la MUNGU.
Maana ya kwanza ya maarifa ni njia inayotumiwa kujitoa katika shida. Shetani ameleta shida nyingi sana na vifungo vingi sana kupitia mawakala zake wachawi, waganga na mizimu na watu wengi sana wameangamia kwa sababu tu wamekosa maarifa ya kuwatoa katika shida hizo. Biblia inajulisha ikisema kwamba Kumcha MUNGU ndio chanzo cha maarifa sahihi yanayoweza kumsaidia mtu ili atoke katika shida mbalimbali za kiroho, Hiyo iko Mithali 1:7 '' Kumcha BWANA ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu.''
Biblia inasema Ni wajinga peke yao ndio wanaoweza wakadharau Neno la MUNGU la kuwapa maarifa sahihi ya kutoka katika matatizo ya kuonewa na shetani.
Maana ya pili ya Maarifa  ni njia ya kupata kitu.
Neno la MUNGU ni njia ya uzima, Neno la MUNGU ndio taa pekee ya kweli inayotakiwa kumuongoza mtu hata akafanikiwa katika kumshinda shetani na mawakala zake na ni Neno la MUNGU pekee ndio taa inayoweza kukumlikia hata ufike uzima wa milele.
Kumbuka Neno la MUNGU analo YESU KRISTO, hivyo kumpokea YESU kama Mwokozi ni kupokea Neno la MUNGU la uzima, hiyo iko Warumi 10:17 '' Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la KRISTO.''
Maana nyingine ya maarifa ni ujuzi na elimu hivyo kujifunza Neno la MUNGU na kulitafakari ndio kuyapata maarifa yakukusaidia katika maisha yako siku zote. 

Ndugu, unahitaji tu maarifa ya MUNGU na kumbuka kwamba Maarifa ya MUNGU ni Neno la MUNGU.
Sasa wengi  leo Wanaangamizwa kwa kutokulijua Neno la MUNGU.

Maarifa sahihi yanaanza na kumjua YESU KRISTO kama Mwokozi wako, sasa watu wengi leo Wanaangamizwa kwa kutokumjua YESU KRISTO Mwokozi.
Ukitaka kumjua YESU Biblia inakujulisha vyema kabisa kwamba "Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa MUNGU, naye Neno alikuwa MUNGU.-Yohana 1:1"


Kumjua YESU na kazi zake ni kujua njia ya uzima wako wa milele.
Kumjua YESU ndio kumjua MUNGU Muumbaji wako.
YESU alikuja kwa ajili yako binafsi.
Luka 19:10 "Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea."


Inawezekana kabisa dini ya wazazi wako ilikupoteza.
Inawezekana kabisa dini ya babu zako ndio inakupoteza.
Ndugu yangu, Bwana YESU alikuja kukuokoa.
YESU hakuja kuanzisha dini wala dhehebu bali alikuja kutafuta waenda mbinguni.
Ndugu mpokee YESU leo kama Mwokozi wako.
Ukikataa kuokolewa na YESU hakika utaangamia kwa sababu umekosa maarifa sahihi.
Ukimkataa YESU utaangamia kwa kokosa maarifa ya MUNGU.
Ndugu usikubali kuangamia kwa kukosa maarifa na wala usikubali kuangamizwa na dini yako kwa sababu tu umekosa maarifa sahihi ya MUNGU.
Usikubali kuangamizwa na dhehebu lako kwa kukosa maarifa ya Wokovu wa MUNGU ambayo ni KUOKOKA.
YESU alikuja kukuokoa hivyo hakikisha unaokoka kwa kumpokea YESU KRISTO kama Mwokozi wako na kisha kuanza Kuishi maisha matakatifu ya Wokovu wake.

Yohana 3:16-18 ''Kwa maana jinsi hii MUNGU aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana MUNGU hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa MUNGU.''

Hayo ndio maarifa namba moja ya MUNGU yaani Wokovu.
Ukiokoka unahitaji kulijua sana Neno la MUNGU na kuliishi.
Ukiokoka unaweza ukakutana na watu ambao hawajampokea YESU kama wewe, wengine katika hao watu lengo lao ni kutaka kuokoka lakini wengine ni kutaka kukuondoa wewe kwa YESU.
Kumbuka hakuna anayekuuliza swali kama hana sababu.
Ukiona mtu anakuuliza swali lolote ujue kuna sababu ya kukuuliza swali.
Kwa waliookoka ni kawaida kuulizwa maswali kuhusu tumaini la Wokovu wao.
1 Petro 3:15 " Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu."

Lakini ndugu sio kila swali lazima ujibu kwa sababu sio wote wanaokuuliza swali la kiroho wanataka kujua.
Wengine hukuuliza swali ili kuupeleleza Uhuru wako kwa YESU.

Wagalatia 2:4 '' Bali kwa ajili ya ndugu za uongo walioingizwa kwa siri; ambao waliingia kwa siri ili kuupeleleza uhuru wetu tulio nao katika KRISTO YESU, ili watutie utumwani;''
Hapa ndipo baadhi ya watu waliookolewa na Bwana YESU hurudishwa utumwani na watu wanaopeleleza uhuru wa mteule wa MUNGU aliyeokoka. 
Uwe makini ndugu baada ya kuokoka maana wapo pia ambao hutaka kukurudisha utumwani.
Wengine watakuuliza ili wakukosoe kulingana na ufahamu wao, hata kama wewe uko sahihi wao watataka wajionyeshe kwamba wanajua kupitia swali walilokuuliza.
Sio kila swali unajibu. Mimi binafsi kuna maswali mengi mno ya watu sikuwahi kuyajibu kwa sababu waulizaji hawakuuliza ili wajue kitu wasichokijua Bali wanauliza ili wajaribu kukushusha na wao kupanda kwa kupitia swali wanalouliza.

Unahitaji kujibu maswali ya watu lakini lazima ujue muuliza swali alikusudia nini.

Ukiwa tayari umeokoka unahitaji kuishi kama waliookoka wanavyotakiwa kuishi.
Waefeso 6:17 ''Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa ROHO ambao ni neno la MUNGU;''

Katika kukupa maarifa ya MUNGU ni vyema ukajua mfano huu kwamba Askari huwa hawaishi kama wanavyopenda wao Bali huishi kama linavyopenda jeshi.
Kwa mfano huo naomba Mteule wa KRISTO ujue kwamba hutakiwi kuishi kama unavyotaka wewe Bali ishi kama KRISTO YESU Mwokozi wako anavyotaka.
Kama utaishi Kama unavyotaka ujue KRISTO hatakuwa na wewe. Na siku ya mwisho ikifika huna KRISTO ujue hauwezi kuingia uzima wa milele.
Ndugu usiishi kama unavyotaka wewe Bali ishi kama KRISTO YESU anavyotakaka.

1 Petro 1:14-15 "Kama watoto wa msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye(YESU) aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote;"

Kumbuka Anayeweza kumpeleka mtu uzima wa milele ni YESU KRISTO pekee. Na kumbuka kwamba Bwana YESU alikuja kutafuta waenda mbinguni.
  Mathayo 11:28 ''
Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.''
Ndani ya YESU KRISTO kuna njia ya mbinguni iitwayo Utakatifu.
Ndani ya YESU KRISTO kuna Neno la MUNGU.
Ndani ya YESU KRISTO kuna ROHO MTAKATIFU na nguvu zake.
Ndani ya YESU KRISTO, MUNGU amejifunua na amefunua ahadi zake za milele.
Ndani ya YESU KRISTO kuna njia ya uzima wa milele iitwayo Wokovu wa KRISTO.
Bwana YESU alikuja kutafuta waenda mbinguni ukiwemo wewe. Hebu mpokee kama Mwokozi na kama umeshampokea kama Mwokozi wako basi endelea kuishi maisha matakatifu ayatakayo yeye Bwana YESU.

 Warumi 8:38-39 '' Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa MUNGU ulio katika KRISTO YESU BWANA  wetu. ''

  Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa BWANA YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
0714252292.
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu

Comments