SAUTI YA NENO LA MUNGU.



Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU
 

Bwana YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU.
Neno la MUNGU lina sauti.
Watu wengi hulisikia Neno la MUNGU lakini hawaisikii sauti iliyo ndani ya Neno la MUNGU.
Tofauti ya waliohudhuria ibada  ya Neno la MUNGU huwa inaonekana  kati ya walioisikia sauti ya Neno la MUNGU na waliosikia tu Neno la MUNGU. Walioisikia  sauti ya Neno la MUNGU ni wale ambao hufanyia kazi walichokisikia.
Walioisikia sauti ya Neno la MUNGU ni wale watendaji wa Neno na sio wale wasikiaji tu.
Yakobo 1:22 '' Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu.''
Maana yake unaweza ukalisikia Neno la MUNGU lakini usiisikie sauti ndani ya hilo Neno la MUNGU. Unaweza ukalisikia Neno lakini usielewe katika usahihi, unaweza ukalisikia Neno Lakini kama hutaisikia sauti ya Neno la MUNGU hakika hutazaa matunda mema.
Mathayo 13:23 '' Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini. ''
 
Kumbuka kuna tofauti ya Neno na andiko.
Andiko ni andiko lolote kutoka ndani ya Biblia.
Neno ni ufunuo anaokupa ROHO MTAKATIFU  kutoka ndani ya maandiko. Wengine huita rhema na Logos, yaani Rhema ni Neno la Ufunuo analokupa ROHO MTAKATIFU kwa ajili ya muda maalumu na kwa watu waliokusudiwa.
Logos ni kila andiko la Biblia.
Ukimuona Mtumishi wa KRISTO yeyote anafundisha ujumbe wa Neno la MUNGU ujue huyo anafundisha rhema yaani Neno la Ufunuo alililolipata kutoka ndani ya maandiko.
Sasa watu wengi sana hulisikia Neno la MUNGU lakini hawaisikii sauti iliyo ndani ya hilo Neno.
Kuna vitu viwili hapa, kuna kulisikia Neno la MUNGU na kuna kuisikia sauti iliyo ndani ya Neno la MUNGU.
Kila mtu kanisani au kwenye semina au kwenye mkutano wa injili hulisikia Neno la MUNGU lakini walioisikia sauti iliyo katika Neno hilo tu ndio wale ambao hufanyia kazi walichokisikia.
Mfano unaweza ukahubiri toba na baada ya kumaliza ukiuliza aliye tayari kumpokea YESU utawaona baadhi wakitaka kumpokea YESU kama Mwokozi wao. Kuna wengine japokuwa wana dhambi na wanatakiwa kumpokea YESU wao watashindwa kwenda mbele kumpokea YESU maana wao wamelisikia Neno la MUNGU tu lakini hawakuisikia sauti iliyo katika hilo Neno la MUNGU. Anyesababisha watu wasiisikie sauti iliyo katika Neno la MUNGU ni wao wenyewe.
Kwa mfano Unaweza ukahubiri na kabla hujamaliza kuhubiri unamuona mtu analia kwa uchungu maana anasikia sauti ikisema ‘’Tubu kwa sababu hujui siku wala saa  ya kufa kwako, tubu na wasamehe waliokukosea, achilia tu maana sasa utafanyika mtoto wa MUNGU’’
Sasa katika ibada hiyo hiyo kuna mtu kwa miaka zaidi ya 10 hajamsamehe mtu aliyemkosea na wala hana haja ya kutubu, wengine wanatubu kwa kosa kama hilo hilo lakini yeye wala hana habari na kutubu, huyo kalisikia Neno la MUNGU lakini hajasikia sauti iliyo ndani ya Neno la MUNGU.
Ndugu, unayenisikiliza muda huu nakuomba sana kwamba katika kila ibada ya Neno la MUNGU unayohudhuria hakikisha unakuwa unaisikia sauti ya Neno la MUNGU na sio kuishia kulisikia tu Neno la MUNGU.
Kuna watu wanaweza kuwa ni watu wa kushangilia tu ibadani kila mtumishi akisema maneno machache ya Neno la MUNGU. Mfano mtumishi anaweza akakemea uzinzi na uasherati na kusoma Neno la MUNGU linalosema kwamba ‘’Hakuna mbingu ya wazinzi wala waasherati’’ unashangaa mtu anapiga   kelele na kusema ‘’Amen amen’’ wakati hata yeye anatakiwa kutubu maana anaifanya dhambi hiyo hiyo lakini kwa sababu ya kutokuisikia sauti ya Neno la MUNGU analiona Neno lile kuwa ni la kawaida tu na anajiona kama halimhusu kabisa.
Neno la MUNGU lina sauti ndani yake na wanaoisikia sauti hiyo ni wale walio na njaa na kiu ya haki ambayo ni kui ya Neno la MUNGU.
Unaweza usiisikie sauti ya Neno la MUNGU kwa sababu ya kutokuwa makini kwako ibadani.
Kuna watu wakati wa Neno la MUNGU ndio wakati wake wa kupanga mipango yake ya maisha, hizo ni hila za shetani kumtoa katika kuisikia sauti ya Neno la MUNGU.
Kuna mtu wakati wa Neno la MUNGU ndio wakati wake wa kusinzia, hizo ni hila za shetani.
Ndugu, hakikisha unaisikia sauti ya Neno la MUNGU, usiishie tu kulisikia Neno la MUNGU bali isikie pia na sauti ndani ya hilo Neno la MUNGU.
Hakikisha unaifanyia kazi sauti ya Neno la MUNGU unalifundishwa.
Yohana 8:47 '' Yeye aliye wa MUNGU huyasikia maneno ya MUNGU; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa MUNGU.''

UFANYEJE ILI UISIKIE SAUTI YA NENO LA MUNGU?

    1.  Omba toba kwa kilichosababisha usiwe unaisikia sauti ya Neno la MUNGU . 
Matendo 3:19 '' Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake BWANA; ''

     2.  Zingatia Neno la MUNGU bila kuangalia hali ya mwanadamu anayelisema Neno hilo.
 Isaya 35:8 ''Na hapo patakuwa na njia kuu, na njia, nayo itaitwa, Njia ya utakatifu; wasio safi hawatapita juu yake; bali itakuwa kwa ajili ya watu hao; wasafirio, wajapokuwa wajinga, hawatapotea katika njia hiyo.''
Watu wa MUNGU au Watumishi wa MUNGU wajapoonekana wajinga au wa kawaida tu hiyo haina maana kwamba sio watumishi wa MUNGU wanaopewa Neno na ROHO MTAKATIFU ili kukusaidia.

   3.   Uwe na moyo wa kulitii Neno la MUNGU linapozungumza na wewe. 
Kumb 28:1 '' Itakuwa utakaposikia sauti ya BWANA, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo BWANA, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; ''

    4.  Zikatae njia za shetani za kuliondoa Neno la KRISTO ulilolisikia.  
Mathayo 13:19,22 '' Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia. Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai. ''

    5.  Andika kila unachotakiwa kufanyia kazi kinachotoka ndani ya Neno la MUNGU ulilojifunza.  
Habakuki 2:2 '' BWANA akanijibu, akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. ''
Habakuki aliposemeshwa na MUNGU aliandika hicho alichosemeshwa, hata wewe hakikisha unaandika Neno la MUNGU unalofundishwa ili ije ikusaidie baadae.
Hata MUNGU aliposemeshwa na MUNGU aliandika, hivyo Neno la MUNGU analokuambia MUNGU ni vyema kuliandika ili usisahau na ili uje ulitumie Baadae, mfano kwa Musa ni huu  Kutoka 24:4 ''Basi Musa akayaandika maneno yote ya BWANA, akaondoka asubuhi na mapema, akajenga madhabahu chini ya mlima, na nguzo kumi na mbili, kwa hesabu ya kabila kumi na mbili za Israeli,''

    6.  Kataa roho ya mazoelea kwenye Neno la MUNGU
Zaburi 119:130 ''Kufafanusha maneno yako kwatia nuru, Na kumfahamisha mjinga.''
Mjinga ni mtu yeyote ambaye ahafahamu kitu  fulani ila akifundishwa kitu hicho anaelewa. Hata wewe ni mambo mengi sana ya MUNGU huyaelewi ndio maana inakupasa kujifunza Neno la MUNGU kila mara, hivyo ukiwa mtu wa mazoelea ujinga wa kiroho hautaondoka kwako. Hivyo kataa mazoelea katika Neno la MUNGU ili upate kuisikiliza na kuifanyia kazi sauti ya Neno la MUNGU uliyoisikia ndani ya Neno la MUNGU.

    7.  Lipe Neno la KRISTO thamani ya kwanza kwenye maisha yako. 
Mithali 30:5-6 '' Kila neno la MUNGU limehakikishwa; Yeye ni ngao yao wamwaminio. Usiongeze neno katika maneno yake; Asije akakulaumu, ukaonekana u mwongo.''
Neno la MUNGU limehakikishwa na ni la thamani sana hivyo hakikisha unalipatia thamani ya kwanza katika maisha yako ndipo itakuwa rahisi sana kwako kuisikia sauti ya Neno la MUNGU ndani ya Neno la MUNGU.

.   8.  Jitenge na dhambi na kila mambo ya dhambi. 
Yakobo 1:21 ''Kwa hiyo wekeeni mbali uchafu wote na ubaya uzidio, na kupokea kwa upole neno lile lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa roho zenu. ''

    9.  Kubali kufunguliwa vifungo vya giza  vilivyokufunga ili usizingatie  Neno la MUNGU.
 Mathayo 11:28 ''Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.''
Kuna watu wanateswa na vifungo vya giza vinavyowazuia kulielewa Neno la MUNGU.
Mimi Peter Nimewahi kukutana au kuwasiliana na watu ambao kila Neno la MUNGU likianza kufundishwa yeye anasinzia, mWingine kila akianza kusoma Neno la MUNGU kichwa kinakuwa kizito na usingizi wa ghafla unamujia hata kama ni muda mfupi uliopita ametoka kulala. Mtu  pia kama ana mapepo au anateswa na mizimu ya ukoo au maroho ya kurithi ya kipepo hakika huyo anahitaji kufunguliwa hivyo vifungo ndipo atakuwa na kiu ya Neno la MUNGU na atakuwa anaisikiliza sauti ya Neno la MUNGU na hatakuwa mtu wa kusahau sahau Neno la MUNGU.
Bwana YESU kwa upendo wa ajabu anamtaka kila mtu aliye na kifungo cha kipepo amkimbilie yeye ili yeye YESU amweke huru mtu huyo. Ndugu kama unateswa na vifungo vya giza hakikika unakimbilia maombezi ili ufunguliwe katika jina la YESU KRISTO.

    10. Usipingane na Neno nla KRISTO kwa sababu ya mitazamo yako na misimamo yako binafsi.   
1Petro 5:5 '', ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu MUNGU huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.''
Kwenye suala la unyenyekevu kwa MUNGU ndiko wengi sana wamekwamba.
Watu wengi wamejaa vizuri kiasi kwamba wako tayari kubishana hata na Biblia.
Ndugu, ukitaka uwe unaisikia sauti ya Neno la MUNGU katika Neno la MUNGU ulilosikiliza hakikisha unakuwa huna misimamo binafsi au mitazamo binafsi inayopingana na Neno la MUNGU.
Leo kuna hadi wanaojiita Kanisa lakini hawataki mafundisho kuhusu ROHO MTAKATIFU na hawamhitaji kabisa, wakati ukweli ni kwamba Bila ROHO MTAKATIFU hakuna mtu anayeweza kushinda ya dunia hata aupate uzima wa milele.
Bila ROHO MTAKATIFU huwezi kumpendeza MUNGU kamwe. Sasa mtu Mwenye mtazamo wa kumpinga ROHO MTAKATIFU hawezi huyo kuisikiliza sauti ya Neno la MUNGU la kweli.
Kuna watu hadi wanampinga YESU, Hao hawajaamua kwenda uzima wa Milele maana Bila YESU KRISTO hakuna mwanadamu hata mmoja ataupata uzima wa milele, ndivyo maandiko yasemavyo.
Kuna hadi mtu mmoja alinitukana akilalamika kwanini kila somo langu nikianza kufundisha Nasema ''Bwana YESU atukuzwe'' au ''Bwana YESU asifiwe'' yeye anaona nakosea sana na hadi kuna siku aliniambia kwamba ''Mbona unamfagilia sana YESU tu''
Mtu wa msimamo kama huo mbaya hakika anaweza kuipinga kweli ya MUNGU kila siku kwa sababu tu ya misimamo yake binafsi aliyofundishwa.
Kuna hadi Wakristo ambao wamewekewa misimamo na mitazamo mibaya na viongozi wao wa kiroho.
Mtu kama huyo kwa sababu ya mitazamo yake na misimamo yake aliyofundishwa anaweza kushindwa siku zote kuisikia sauti ya Neno la MUNGU ndani ya Neno la MUNGU analojifunza.
Ndugu yangu, kwenye suala la kujifunza Neno la KRISTO hakikisja misimamo ya kidini, kidhehebu haikufanyi usiizingatie sauti ya Neno la MUNGU.
aAchana na itikadi za kifalisayo na achana na itikaddi za kisadukayo. achana na udhehebu na achana na upinga Kristo.


Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
0714252292(Hadi whatsapp).
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.


Comments