shuhuda na maswali

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana  YESU
Naendelea kukupa shuhuda chache kama nilivyoandikiwa na wahusika.

Ushuhuda wa kwanza 
salamu Peter Mabula mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU KRISTO. Asante sana mtumishi ubarikiwe sana sana maana karibia kila somo utakalotoa linanigusa sana kuhusiana na maisha yangu kwa hakina MUNGU amekuleta hapa kwa kusudi uitie nguvu mioyo minyonge, niliteswa sana na vifungo vya kipepo lakini sasa YESU amenifungua ahsante kwa maombi yako UBARIKIWE.

Majibu yangu.
MUNGU akubariki sana.
Songe mbele na YESU na hakika wewe u mshindi.
Ubarikiwe sana


Shalom mtu wa MUNGU.
Ngoja nikupe ushuhuda wa rafiki yangu mmoja toka Arusha. Nauleta ushuhuda huo kama alivyoandika mwenyewe.


USHUHUDA WA PILI.
Mwinjilisti Peter Mabula, MUNGU azidi kukupa maono, hakika ni MUNGU ndiye aliyenifanya niweze kushinda hili, kwani ni muda sana nilianza kupanga kuombewa na Wewe lakini adui alinizuia sana kila nikisema nikupigie fikra zinakuja mbona Eliya uko vizuri, nikapanga tena niweke hela kwa ajili ya kununua kitabu cha MAOMBI YA KINA kila nikiweka hela nakaa kidogo naamua kuitumia wazo likinijia kuwa "utanunua ukipata hela nyingi" hizo hela nyingi nikizipata zinakoenda hata sielewi, mpaka adui alipotaka kunirudisha nyuma na kuanza kufikiria "Mimi naenda kanisani nimeomba kwa muda mrefu sijibiwi kwenda kanisani kwafaa nini, likaja wazo ivi unaokoka halafu unanyimwa vitu vizuri si heri uachane na wokovu, Ukweli huwezi amini Mwinjilisti Peter Mabula namba ya kupata kitabu nilikuwa nayo lakini kumbukumbu sikuwa nayo kabisa, ninamshukuru MUNGU kwani ulivyoniombea nikajisikia mwepesi, na nilikuwa na shilingi 8,000 tu, nikasema hii hela nanunua vocha ili niombewe na kesho nitaenda kununua kitabu, hakika MUNGU ni wa ajabu namaliza maombi natoka nje nakutana na boss wangu ananiongeza hela sikumuomba wala sikumwambia neno lolote, na MUNGU amekuwa nami, hivi ninavyoandika ujumbe huu kitabu nimeshakinunua na nimekisoma kwa ufupi nimejikuta kama nimeokota dhahabu chini ya mpapai, ijapo kabla sijakinunua hiki hapo nilipokuaga na mpango wa kununua kitabu nilikua nawaza unawezaje kununua kitabu 8000, lakini hapo nilipo nahisi hiki kitabu nimekichukua bure hakika namuona MUNGU akianza kunifungua, Nimekisoma sura ya 1: KUOMBA KATIKA ROHO MTAKATIFU. nimebarikiwa sana na Maneno ambayo Mimi mwenyewe kama Eliya natamanigi sana ninene kilugha lakini maswali mengi huwa yananijia ambayo hayana utofauti na uliyokuwa unawaza, nami kupitia kitabu hiki nitapokea kitu cha tofauti sana. Mimi sina la kukwambia au kukupa zaidi ya kukuombea MUNGU azidi kukutumia kuwafunguwa wengine na akufikishe pale alipokusudi Yeye. Ninatamani pia uwe Baba yangu wa kiroho, nikupe ushuhuda mfupi ni Wewe Peter Mabula kupitia somo lako moja ulinifanya nami nikaachana na kuumia moyoni mwangu kwa ajili ya msichana mmoja pia Wewe ndiye uliyenifanya nikijiona nimeokoka kila nikatamani kukirishwa, japo kuanzia hilo somo nilimuacha huyo msichana kwani nilimpenda afu yeye akawa hanipendi, hakika hilo somo lilinifungua na masomo yako mingine mengi ninatamani niseme mengi kuhusu Wewe lakini naona haitoshi, Roho wa MUNGU azidi kukuongoza, pia niombee mdogo wako nina kiu ya kuwaokoa vijana wenzangu.
By Elisha kutoka Arusha mjini.

Nimebarikiwa na ujumbe wa rafiki yangu huyu alioniandikia.
Aliandika hivi, naleta kama ulivyoandikwa.

USHUHUDAWA TATU.
Shalom Mtumishi Peter, hongera sana kwa Kazi njema ya kutulisha Neno la Uzima.
Ni mda sana sijakusalimia lakin isikupe shida huduma yako ni njema sana bado inaendelea kunibariki, ni mafundisho yako mema yenye maonyo ndiyo yanayonilinda mpaka wakati huu tunapoenda kumaliza mwaka, umenibariki sana kwenye masomo ya ujana yanayohusiana na mahusiano na ngono kabla ya ndoa kiasi kwamba nakuwa mkali kwenye eneo hili ambalo limejaa vishawishi mno bila kukaa ndani ya Neno na Maombi huenda ningeshaanguka dhambini.

Natumaini pia ni maombi yako kwa Mungu yanayobadilisha mienendo yetu. Lakini pia kwenye mafundisho yako huwa naomba vipengele mbali mbali hata kama vilishapita naunganisha na ambavyo nimevipata siku za karibun maombi yanaendelea.
UBARIKIWE.

USHUHUDA WA TANO Mtumishi Peter Mabula Nakusalimu katika jina la Yesu, ila bado sijakuwa mkristo kamili yaani wa kweli, sababu, kuna dhambi (Uzinifu na kuvuta Bhangi) ambayo naona imenifakuwa mbali na Muumba Wangu Baba Yetu wa Mbinguni, nami nipo nchini Kenya, Taita-Taveta county, Mbale. (Niliona maombi yako ndipo nikaamua kumpenda page yako), Naomba usaidizi

Majibu yangu kwa ndugu huyo.
Nakuomba jitahidi tu kuacha dhambi hizo na amua tu ndugu kumpendeza MUNGU.
Tafuta MUNGU na sio mambo ya dunia.
Mpokee YESU KRISTO kama Mwokozi wako na amua tu kuichukia jehanamu.
Amua tu kuacha dhambi hizo na utaweza.
Jiunge na kanisa na uwe wazi kwa Mchungaji wako ili usaidike.
Tii Neno la MUNGU na jifunze sana Neno na kulitafakari.
MUNGU akubariki sana na soma 1 Petro 1:14-15 kisha soma 1 Yohana 2:15-17.
MUNGU akubariki sana.




Rafiki yangu mmoja aliniandikia ujumbe mgumu sana na nawiwa nikushirikishe kama ulivyo huo ujumbe kisha ujifunze kitu.

USHUHUDA WA  6.
Mwinjiristi Peter shalom.
Nina mke ambae nimezaa nae mtoto mmoja. Ninampenda YESU na nilishawahi kukuuliza mambo mengi mwaka uliopita kuhusu MUNGU kwa ajili ya mtu ambae hana ndoa(Yaani walichukuana tu) na mkewe nashukuru ulinijibu vizuri tu nami nikawa nimetoa taarifa kanisani ili waniandike katika watu wanaohitaji kufunga ndoa(kubariki ndoa).
Tatizo lilikuja kujitokeza wiki moja baada kutoa taarifa hiyo, mke wangu nilimfumania ndani ya nyumba ya mtu akizini na hapo ilibidi aniambie kundi lote la wanaume aliokwisha kutembea nao hapo mwanzo kabla ya kumfumania. Ameniomba msamaha kwa kulia nami nikamsamehe na ninaendelea kuishi nae ila ilibidi suala kufunga ndoa tulisimamishe na hata viongozi wangu kanisani wameniashauri kwamba nisimamishe ili nimtazamie ila nashukuru kama amebadirika kwa kiasi fulani.
Fumanizi hili lilitokea usiku wa sikukuu ya Eid elhaj katika nyumba ya jirani na ninapoishi akiwa na kijana mmoja mgeni alietoka Dar es salaam. na aliyeniletea taarifa ni kijana ambae alikuwa na mahusiano mwanzoni na wakakorofishana na huyu msichana akitongoza na kutembea na wanaume wengine. Amekwisha kuwa uhusiano na wanaume wapatao nane ambao wawili kati yao walimtongoza ilĂ  hawa sita ni yeye msichana ndio aliwatongoza na kuwahonga pesa kidogo sasa kuna ndoto nimeota nahisi ndoto hii inahusiana na hasira kwa yaliotokea maana ni muda mfupi tu tangu yatokee na ndoto ilipotokea. Naomba ushauri na tafsiri ya ndoto hii. Nakusihi pindi ukipata ujumbe huu usiupuuzie maana inanichanganya kuniweka katika ulinzi wa hali ya juu kwa mke wangu nikhisi labda hii ndoto ni ya kweli au la.
Dhumuni hasa la kuandika ujumbe huu kwako ni kwamba baada ya sakata hilo la fumani kuisha tulipanga tukatembelee Tanga mjini (baharini) siku ya sikukuu ya christmass. Leo hii katika kuperuzi facebook nimeona somo lako kuhusu ndoto, nami juzi tu nimeota ndoto katika hiyo safari yetu baharini tulipitia uwanja wa ndege tukaangalia ndege na mambo fulani kama tour vile wakati tunaondoka nafika kwenye gate naangalia nyuma mke simuoni nkamtafuta sana nikamkuta akibakwa na vinne vyenye nguvu hivyo nikamkuta yuko hoi hajitambui ila katka kuita sana alinitambua na akaniaga kwa kuniambia kwamba nimuache maana hatapona, lakini nikambeba nikamtoa ndani ya kile chumba nikamuweka sehemu nikaenda kuita tax narudi nikakuta wale wanaume wamembeba tena wakaondoka nae wakidai wanaenda kumuua nikawakimbiza lakini sikufanikiwa.
Na safari ile tulikuwa watu wanne mimi, mke na watoto wawili sasa katika juhudi zangu za kumtafuta mke maana tumeshatoka nje ya gate na watoto ndipo mimi nilirudi ndani ili kumtafuta mke na niliwaacha nje hivyo nikawa nimepoteza mke pamoja na watoto ndipo nikashtuka kutoka usingizini. Sasa naomba unisadie inamaana gani nakemea kila usiku ili isiwe na uhakisia. Naomba msaada wako


Majibu yangu kwa ndugu huyu yalikuwa ni haya.
Pole sana kwa hayo ndugu yangu, nisamehe maana kwa sababu ya majukumu nimejikuta ni siku nyingu sijafungua inbox ya page.
ninachokuomba Ndugu yangu, kama mkeo amebadilika msamehe na mweke kwenye angalizo kwa muda. Kuhusu ndoto ni kwamba kuna maroho ya kuzimu yanamfuatilia mkeo ili tu akosee na msifunge ndoa. Husika na maombi haya.
1. Karibu nguvu za Giza zinazomtumikisha kipepo.
2. Haribu madhabahu ya uharibu iliyomfunga.
3. Kataa connection kati yake na ulimwengu wa roho wa Giza.
4. Komboa ufahamu wake ili usitumike kipepo.
5. Utiishe mwili wake kwa damu ya YESU KRISTO.
6. mpeleke kuombewa ili kuondoa majini mahapa.

Lakini mchunguze sana sana ili kujua chanzo cha ushetani anaofanya.
Ninachotaka ujifunze wewe unayesoma Ujumbe kutokana na tukio hili ni haya.
1. Usaliti ni mbaya sana.
Kama wewe ni msaliti acha Mara moja.

2. Aliyekukosea akitubu msamehe.
Nimeona nguvu ya msamaha katika ushuhuda huu wa maumivu.

3. Usikubali kutumika kishetani.
Maana utaleta majeraha kwa wasiostahili.

4. Uwe makini wewe ambaye hujaingia kwenye ndoa.
Usitegemee akili zako Bali omba sana na mche MUNGU sana.

5. Kuoa/Kuolewa na mtu asiye na hofu ya MUNGU ni hasara kubwa.
6. Jifunze kuachilia na kusamehe.
Sio kutokujibiwa meseji moja tu unavunja uchumba.

7. Usikubali kuwa Mali ya shetani kwa sababu ya tamaa zako za kishetani.
Madhara ni mengi sana.
Unaweza ukaongeza hapo juu madhara zaidi kutoka katika ushuhuda huu mgumu.
Mwisho kabisa usiache kuwaombea wahusika wa ushuhuda huu mgumu.
MUNGU akubariki sana.

By Mwinjilisti Peter Mabula.

Comments