MAMBO MNAYOTAKIWA KUFANANA WEWE NA MCHUMBA WAKO.

Watumishi wa MUNGU, Peter  na Scholar Mabula.




Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu.

Karibu tujifunze Neno la MUNGU la uzima.

Mtu yeyote akitaka kuoa au kuolewa huchagua mtu sahihi kulingana na mtazamo wake.

Wakati huo ndio wakati wa kuchagua mtu sahihi maana mkishafunga ndoa hakuna kuachana kamwe.

Watu wa MUNGU siku zote wanahitaji kutafuta wachumba wa kufanana nao, hiyo ni siri na ni fumbo kabisa kwa baadhi ya watu.

Mwanzo 2:18 '' BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.''

Ni vyema sana wewe mteule wa KRISTO ukampata mchumba wa kufanana na wewe hilo ndilo kusudi la MUNGU.

Na kila mtu hutaka kutaka mchumba wa kufanana naye.

Lakini kwa sababu upendo una nguvu kama mauti (Wimbo 8:6 ...  Kwa maana upendo una nguvu kama mauti  ....) watu wengi wamesukumwa na upendo na kusahau kuangalia kitu kinachoitwa ‘’Kufanana’’

Kwa nini kufanana ni muhimu?

Haiwezekani Simba dume akaoana na ng’ombe jike, hao hawafanani na kitakachofuata ni hatari kuu kwa ng’ombe.

Haiwezekani Nyoka na ng’e wakaoana, japokuwa wote ni wakali  lakini mmoja atakufa maana hawafanani.

Ndugu nimesema hayo nikiwa na maana kwamba hata wanadamu wapo walio kondoo kiroho hivyo haiwezekani hao kuoana na wanadamu walio na roho za nyoka, haiwezekani kondoo kuoana na mbwa mwitu, kuna watu wana roho za mbwa. Inawezekana mifano hiyo ikawa migumu kwa watu wasiojua ulimwengu wa roho lakini ndugu chunguza mnafanana nini na mchumba wako.

Usichunguze kimwili bali chunguza kiroho maana ukichunguza kimwili utaona tu kwamba mchumba wako ana macho mawili kama wewe, ana miguu miwili kama wewe lakini anaweza akawa na roho mbili au 3 au 4  na kwa njia hiyo akawa hafanani na wewe.

Anaweza akawa na roho  yake lakini akawa na roho ya shetani pia na akawa na roho ya uchawi au uganga ili  kukufunga wewe.

Je mnafanana nini na mchumba wako?

Adamu alipewa Eva wa kufanana naye kabisa, hata wewe mteule wa MUNGU unahitaji kupata Mchumba wa kufanana na wewe.

Sitasahau siku moja Dada mmoja alinipigia simu akiniambia kwamba amekuja Kanisani kwao kijana mmoja mtanashati na ana kama mwezi mmoja tangu aokoke, Kaka yule akataka kumuoa  huyu dada na kabla ya yote yule dada akakutana na somo langu mtandaoni akajifunza na kuchukua namba yangu ili nimshauri na kumuombea. Aliponipigia simu kabla hajaniambia rohoni nilijulishwa kwamba nimwambie yule dada aachane na huyo kijana, dada yule nilimwambia lakini kwa sababu upendo una nguvu kama mauti{Wimbo 8:6) alinidharau na kukata simu, ilipita kama miezi 7 akanipigia simu akisema ‘’Ni heri ningekusikiliza Mtumishi Mabula’’ 
Mimi wakati huo hata sikuwa nakumbuka lakini akaniambia juu ya yeye baada ya  kuongea na mimi walifunga ndoa lakini baada tu ya  kufunga ndoa kumbe yule kijana alikwenda Kanisani pale ili tu ampate dada yulee hivyo baada ya ndoa yule kaka akarudi katika dini yake, akarudi kunywa pombe na kuvuta bangi. Ndoa ikageuka ndoana na hadi siku Dada yule ananipigia simu alisema mume wake humpiga kila siku na amemvunja mguu kwa kipigo.

Ndugu unahitaji kupata Mchumba wa kufanana na wewe.

Ukimcha MUNGU hakika utaletewa Mchumba wa kufanana na wewe kama ambavyo Adamu aliletewa Eva wa kufanana na yeye.

Je unataka  Mchumba wa kufanana na wewe?

Zingatia haya ambayo mnatakiwa kufanana 

1  1. Fananeni katika imani ya Wokovu. 

Waefeso 4:4-6 ''Mwili mmoja, na ROHO mmoja, kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. Bwana(YESU) mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. MUNGU mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote. ''

Hapa sizungumzii dhehebu bali imani ya kweli ambayo ni Wokovu wa Bwana YESU.

Biblia inakataza Mteule wa KRISTO kuoa au kuolewa na MpingaKristo. 
Ona mfano huu ambapo Mtumishi wa MUNGU anawaonya watu wa MUNGU katika kuoana na wapinga Kristo
Nehemia 13:25-27 '' Nikagombana nao, nikawalaani, nikawapiga baadhi yao, na kuwang'oa nywele zao; nikawaapisha kwa MUNGU, nikasema, Msiwaoze wana wao binti zenu, wala msiwatwae binti zao ili waolewe na wana wenu, wala na ninyi wenyewe. Je! Sulemani, mwana wa Daudi, hakufanya dhambi kwa kutenda hayo? Lakini katika mataifa mengi hapakuwa na mfalme mwingine mfano wake. Tena alipendwa na MUNGU wake, naye MUNGU akamfanya mfalme juu ya Israeli; walakini wanawake wageni walimkosesha hata yeye. Basi, na sisi, je! Tuwasikilize ninyi kutenda neno hili baya, hata kumhalifu MUNGU wetu kwa kuwaoa wanawake wageni? ''
Wanawake wageni au wanaume wageni wale walio nje ya imani ya Wokovu wa KRISTO, hao usikubali kugunga nao ndoa kama hujaingia katika ndoa bado. Kama uko katika ndoa ya namna hiyo basi muombee Mwenzi wako ili apate Neema ya MUNGU, Lakini kama hujaingia katika ndoa basi kama una mchumba Mpinga Kristo achana naye haraka. Yakumbuke maandiko hapo juu ambayo yanasema kwamba Suleimani mwenye hekima lakini wenzi wake wa ndoa walimgeuza moyo, ni hatari sana.

Hivyo msipofanana imani hakika ni hatari kwako.

Unajisikiaje sasa mtakuwa katika ndoa na wewe unamtaja YESU huku mwenzi wako anamtaja shetani,mizimu au anayataja majini kuwa ndio msaada wake?

Wewe unajua kabisa kabisa kwamba katika ndoa tendo la ndoa litakuwa katika utaratibu wa kawaida lakini mwenzi wako kwa sababu hana hofu ya MUNGU wako yeye  anataka mfanye mapenzi kinyume na maumbile, kwanza ni dhambi maana unaweza hata ukakosa uzima wa milele kwa sababu ya kufanya mapenzi kinyume na maumbile hata kama uko katika ndoa yako kabisa.

Unajisikiaje wewe unataka kwenda kwenye mkesha wa maombi kanisani huku mwenzi wako anakuomba wakati ule ule umsindikize kwa mganga wa kienyeji?

Ni hatari sana sana sana, ndio maana Biblia inakutaka uwe makini na uchague Mchumba wa kufanana na wewe imani.

Wewe unaamini katika YESU KRISTO, ROHO MTAKATIFU na MUNGU muumbaji lakini mwenzako hata ukianza maombi tu usiku anakukataza maana unakuwa unachokoza madhabahu zake za giza.

Ndugu, hapa sasa nakutegulia fumbo la kumpata wa kufanana na wewe, hakikisha ameokoka kama wewe, hakikisha unampata Mchumba ambaye yuko safarini kwenda mbinguni, na sio kumpata Mchumba ambaye yuko safarini kwenda ziwa la moto, huyo anaweza kukushawishi hata na wewe ukamkana YESU na kuungana na Mwenzi wako jehanamu, haipasi kuwa hivyo kwa watu wa MUNGU.

Sasa kama mnafanana tu urefu na elimu ukalidhika basi ni hatari kuu kama hamfanani imani ya Wokovu wa Bwana YESU. Nimekuambia leo ili upone.

Hakikisha mnafanana jambo muhimu sana la kwanza kwamba wote YESU KRISTO ni Bwana na Mwokozi wa Maisha yenu, ili iwe baada ya ndoa ufuate uzima wa milele.

   2. Fananeni maisha matakatifu na ya haki.

1 Petro 1:15 '' bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; ''

Ni agizo la MUNGU kabisa kwamba kila Mteule wa KRISTO aishi maisha matakatifu.

Ni agizo la KRISTO mwenyewe  kwamba kila mtu aliye Kanisa la MUNGU aishi maisha matakatifu.

Sasa maisha yako matakatifu yanaweza yakaathiriwa na mwenzi wako kama yeye hayaishi hayo maisha matakatifu yanayoagizwa na Biblia takatifu iliyo Neno la MUNGU pekee.

Hakikisha unampata Mchumba ambaye mnafanana aina  ya maisha ambayo mnaishi, kwa sababu wewe unaishi maisha matakatifu basi hakikisha unampata Mchumba ambaye anaishi maisha matakatifu pia.

Ukimpata mtu ambaye yeye haishi maisha matakatifu na wewe unaishi maisha matakatifu ya wokovu hakika hujampata wa  kufanana na wewe.

Wengine wengi sana hudanganyana kwamba wawakubalie tu wachumba zao wapagani lakini watawabadilisha. Ndugu nisikilize kwa makini sana sana.

Neno la MUNGU  Linasema kwamba hakuna mtu hata mmoja anayeweza kumpokea YESU  KRISTO kama Mwokozi wake kama mtu huyo asipovutwa na nguvu za MUNGU.
Yohana 6:44 ''Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. '' 
 Hivyo ili mtu aokoke kama wewe ni lazima nguvu za MUNGU zimvute na nguvu hizo zinaletwa na MUNGU na sio mwanadamu hivyo unaweza ukaishia kuingia katika ndoa na mtu ambaye kwa akili zako za kibinadamu unadhani utambadilisha na matokeo yake ikashindikana. Kumbuka pia Biblia inasema  1 Kor 7:16 '' Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? Au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo? ''
Ndugu kwani katika Kanisa la MUNGU  nchi nzima  hakuna watu wa MUNGU sahihi wa kukufaa hata utake mpagani?

Siwasemi vibaya wapagani ila kwenye suala la ndoa siwezi hata siku moja kumshauri mtu kuoana na mtu asiyemcha MUNGU, nimeyaona matatizo mengi kwa watu wengi sana ndio maana nina ujasiri mkuu wa kukushauri ndugu kwamba tafuta wa kufanana na wewe, na Neno la MUNGU pia linakataza wateule wa KRISTO kuoana na wasio na KRISTO.

Ndugu unahitaji kumpata wa kufanana na wewe katika aina ya maisha ya kuishi ambayo ni maisha matakatifu ya Wokovu.

Ukimpata asiyeishi maisha matakatifu ujue baada ya kukuoa ikapita miaka mitatu ataongeza mke wa pili au wa tatu maana kwake jambo hilo ni sawa kabisa.

Ikiwa hivyo ujue Kibiblia inakuwa ni wazinifu wamekutana, sasa wewe utakuwa kundi gani?

Ndio maana nakushauri tafuta wa kufanana na wewe. Wengine husema kwamba ndege wafananao ndio huruka pamoja, sasa kama nyie hamfanani mtaingiaje katika ndoa takatifu na iwe ni kwema hadi mwisho, ndugu kama ulishaingia tayari katika ndoa ya namna hiyo omba toba na muombee Mwenzi wako huku ukihakikisha hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kukutoa katika Wokovu wa KRISTO.

Lakini kwa ambaye hujaingia katika ndoa nakuomba chagua wa kufanana na wewe.

Tuko katika kipindi kibaya sana na maasi yameongozeka sana hivyo ukimpata asiyeishi maisha matakatifu kukusaliti ni jambo dogo sana kwake, kukutoa kafara kwa waganga ni jambo la kawaida tu, mtu huyo anajiangalia mwenyewe tu na hakuangalii wewe, akili yake inawaza kwamba hata ukifa ataoa mwingine au ataolewa na mwingine maana wako wengi sana.

Maisha matakatifu yanatakiwa kuwa vazi la kudumu la kila mtu. Wanandoa fulani walikuwa kila wakikosana  kipindi mimba iko changa basi mama yule anaitoa ile mimba, yaani akikwazwa kidogo tu mimba ikiwa changa anaitoa, ni ushetani uliovuka mipaka huo. Wakati mwingine inawezekana watoto wanaouawa na mama zao wakiwa tumboni inawezekana ikavuka hata robo ya watu wote duniani maana kutoa mimba katika jamii ya leo  imekuwa jambo la kawaida kabisa, ni hatari ukimpata mtu asiye na hofu ya MUNGU moyoni mwake.

Ndugu hakikisha unampata wa kufanana na wewe  katika hali ya kuishi maisha matakatifu safi na ya haki.

Ni muhimu sana ukiwa umempokea YESU KRISTO kama Mwokozi kisha umpate  Mchumba aliyeokoka kama wewe, huko ndiko kufanana.

    3.  Fanana na Mchumba wako katika vitu unavyopenda.

Wimbo 1:3,5 ''Manukato yako yanukia vizuri; Jina lako ni kama marhamu iliyomiminwa; Kwa hiyo wanawali hukupenda. Mimi ni mweusi-mweusi, lakini ninao uzuri, Enyi binti za Yerusalemu, Mfano wa hema za Kedari, Kama mapazia yake Sulemani. ''
 Mhusika anaposema kwa Mchumba wake kwamba ''Manukato yako yanukia vizuri '' haina maana kwamba kila mtu atayapenda Manukato hayo. 
Inaposemwa kwamba ''Mimi ni mweusi-mweusi, lakini ninao uzuri'' Haina maana kwamba uzuri wa mhusika utamvutia kila mtu.
Ndugu inawezekana hadi muda huu hujanielewa naelekea wapi katika point hii muhimu.

Ndugu, Baada ya kuhakiki mambo mawili ya kwanza hapo juu jambo lingine lizingatie hili kama unataka kuwa ndoa iliyo na amani.

Najua sio kila kitu unachopenda na mchumba wako apende bali kagua  vitu vichache ambayo hukuchukiza sana hakikisha basi Mwenzi wako unamweleza mapema kabisa ili ajue na ujilidhishe kwamba hatavipendelea na yeye yaani ataachana navyo au hata yeye hahusiki navyo.

Ngoja nikupe mfano wangu mwenyewe ila kama nitakukwaza nisamehe bure. Mimi kabla sijaoa, nilipokuwa sina Mchumba nilikuwa na mambo muhimu sana kwangu ambayo sikutaka yahusike kwa mke wangu ni pamoja na haya ukiacha sababu 2 kuu hapo juu.

Mimi binti ambaye anapenda kutoboa pua, kuvaa mahereni hasa makubwa au marefu, kuvaa chochote kile shingoni, kuvaa mabangili, kuvaa vimini, kuacha matiti nje, kuvaa wigi, kujichubua n.k. Mtu wa aina hiyo hata kama ningefunuliwa kwenye maono mara kumi nisingeweza kumuoa bali angeishia kuwa rafiki yangu wa kawaida tu na sio Mchumba,Namshukuru MUNGU Baba maana sikuwahi kufunuliwa iwe kwa ndoto au maono mtu wa aina hiyo. 
Mtu wa aina hiyo ningemjali kama rafiki na ningekuwa na upendo kwake kama rafiki au mpendwa na sio upendo wa uchumba. Huyo ni mimi, watu wanaovaa hivyo au kuvaa mapambo hayo na mengine zaidi wapo wengi sana na hao ni marafiki zangu sana lakini  upendo wa mtu wa kuoa nisingeweza kuwa nao. Yaani binti  wa aina hiyo hata kama ningeambiwa ni mzuri na ananifaa ningesema ni kweli ni mzuri na ni mtu wa MUNGU mzuri sana lakini kwenye suala la mimi kumchumbia nisingeweza.  Huyo ni mimi, nasema tena huyo alikuwa ni mimi, wewe je?

Sasa katika kumpata Mchumba ni vyema sana ukajitambua maana kuna ndoa nyingi sana zina migogoro kwa sababu tu ya mambo kama hayo.

Unajisikiaje wewe unaoa mke ambaye asipoenda beach weekend anaumwa, wewe hupendi beach lakini mwenzako bila kwenda beach hainogi, mtajikuta mnakosana bila sababu kila muda wa beach ukifika.

Najua kabisa wewe kijana wa kiume kuna mambo huyapendi kabisa kwa ambaye utataka mfunge naye ndoa hata kama ameokoka, ndugu katika kuchagua hakikisha unachagua chaguo lako ambaye mnafanana.

Binti najua kabisa kuna mambo ambayo huyapendi hivyo hakikisha unampata mtu ambaye mnafanana.

Kuna wengine hawezi kukaa nyumbani hata saa moja kwa siku, habanwi na majukumu ya kazi ya namna yeyote lakini yeye ni misele, kama hupendi mtu wa jinsi hiyo na ndio huyo mkafunga naye ndoa ujue itakusumbua sana, hivyo kabla hujaamua kutafuta mwenzi basi tambua mambo  ambayo huyapendi ili isikusumbue baadae.

Naamini umenielewa.

Weka vipaombele vyako vya kwanza kabisa kwamba wewe  na mwenzi wako mko katika kumwabudu MUNGU mmoja yaani YAHWEH, Mko katika Bwana mmoja yaani YESU  KRISTO, Mna ROHO MTAKATIFU, mko imani moja ya Wokovu na mnatumia Biblia moja.
   Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
0714252292(Hadi whatsapp).
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments