MAKUNDI MATANO(5) YA WATU AMBAO GHADHABU YA MUNGU IMEWAKALIA.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
 Bwana YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tena karibu sana tujifunze Neno la MUNGU.
Neno ghadhabu lina maana zifuatazo.
=Ghadhabu ni  kushikwa na hasira ya ghafla.
=Ghadhabu ni hisia anazokuwanazo mtu baada ya kupata maudhi.
=Ghadhabu ni kunigiwa na hasira kali sana au ni kuwa na hasira kali sana.
Sasa wapo pia watu ambao Ghadhabu ya MUNGU inawakalia, ni hatari sana.
Ghadhabu ya MUNGU kukukalia ina maana ya kwamba hasira ya MUNGU iko juu yako na muda wowote inaweza kutimia.
Kuna ghadhabu zinatimia wakati mtu husika akiwa hai lakini kuna ghadhabu hutimia baada ya mtu kufariki, ni hatari sana ghadhabu ya MUNGU kukukalia.
Jinsi ya kuiondoa ghadhabu ya MUNGU juu yako ni mambo matatu tu ya kufanya ambayo ni wewe KUTUBU TOBA YA KWELI, KUACHA DHAMBI na KUUFUATA MPANGO WA MUNGU ANAOKUAMURU
Usipoamua kufuata hayo matatu hakika ghadhabu ya MUNGU inaweza kukukalia daima.
Zaburi 85:3-4 ''Umeiondoa ghadhabu yako yote, Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako. MUNGU wa wokovu wetu, uturudishe, Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu.''
Baada ya utangulizi huo, ndugu sasa jikague katika makundi haya matano ya watu ambao ghadhabu ya MUNGU iko juu yao.
Makundi 5 ya watu ambao ghadhabu ya MUNGU inawakalia ni:

1. Wanaokataa kuokolewa na YESU KRISTO.

Hili ndilo kundi la kwanza la watu ambao ghadhabu ya MUNGU inawakalia.

Yohana 3:35-36 ''Baba(MUNGU) ampenda Mwana(YESU), naye amempa vyote mkononi mwake. Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya MUNGU inamkalia.''
Inawezekana wewe unajiona uko sawa tu na unaendelea na maisha yako lakini kama YESU KRISTO sio  Mwokozi wako hakika ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Biblia hapo juu inasema kwamba MUNGU alimpa YESU KRISTO vyote na hata Bwana YESU Mwenyewe anathibitisha akisema ''Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.-Mathayo 28:18'' Hivyo kwenda kinyume na YESU KRISTO ni kwenda kinyume na MUNGU mwenyewe.
Kumkataa YESU ni kumkataa MUNGU na ni kuukataa mpango wa MUNGU wa uzima wa milele kwa wanadamu,  na watu wa namna hiyo Biblia inasema ghadhabu ya MUNGU inawakalia.
Watu wa namna hiyo wanaweza wasiielewe sasa hiyo ghadhabu ya MUNGU lakini watakapokuwa jehanamu ndipo watajua kwa usahihi, ndugu, Neno la KRISTO la leo lipo kwa ajili ya kukujulisha ili uchague vyema usiende jehanamu.
Kumbuka ni Bwana YESU ndiye atatangaza kwenda jehanamu kwa watu wote wanaokataa kuokolewa na yeye na waovu wote, Mathayo 25:41 '' Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake;''
Je ni wewe ndugu ndiye ambaye ghadhabu ya MUNGU iko juu yako kwa sababu tu umekataa kuokolewa na YESU KRISTO?
Ndugu nakuomba leo jitenge na ghadhabu ya  MUNGU kwa kumpokea YESU KRISTO kama Mwokozi wako, tubu katika yeye na acha dhambi zako zote, fanyika mtoto wa MUNGU na anza sasa kutembea katika Neno la MUNGU.

2. Wanaolipiza visasi.

Hili ni kundi la pili la watu ambao ghadhabu ya MUNGU imewakalia.
Warumi 12:19 ''Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya MUNGU; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena BWANA.''
Inawezekana ni wewe ndugu na umeshaokoka kabisa na Kanisani unaenda lakini wewe ni mtu wa kulipiza kisasi, ndugu kama ni hivyo hakika dhaghabu ya MUNGU inakukalia.
MUNGU hajaagiza watu kulipa kisasi, ukilipa kisasi unakuwa unamfanya MUNGU awe na hasira juu yako.
Biblia inakukataza kulipa kisasi hivyo watu wanaokukosea penda kuwasamehe na kusonga mbele.
Waefeso 4:32 '' tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na MUNGU katika KRISTO alivyowasamehe ninyi. ''
Unaweza kuwa na hasira na watu fulani waliokukwaza tu kidogo na ukawa hata unatamani wapatwe na mabaya lakini ndio kabisa ukaona wanainuliwa, kwa sababu tu wewe umebeba kisasi.
Kisasi ni kitu kibaya sana ipishe ghadhabu ya MUNGU kwa kutokulipiza kisasi.
Ukilipa kisasi ujue hata kama ni wewe ndiye ulikosewa basi hakika hutapata msaada wa MUNGU.
Unapolipa kisasi ujue unatengeneza mambo yafuatayo.
=Utakuwa unatengeneza kushindwa kwako.
=Mabaya hayataondoka kwako.
Mithali 17:13 ''Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, mabaya hayataondoka nyumbani mwake '' 
=Utakuwa unamzuia MUNGU kukupigania.
=Kulipa kisasi ni dhambi.
''Kila amchukiaye ndugu yake ni muuaji: nanyi mnajua ya kuwa kila muuaji hana uzima wa milele ndani yake-1 Yohana 3:15 ''
Hivyo usikubali badala ya ghadhabu ya MUNGU kuwa juu ya aliyekukokoea basi sasa inakuwa juu yako kwa sababu ya kisasi.

3. Wanaofanya ibada ya sanamu.

Hili ni kundi la tatu la watu ambao ghadhabu ya MUNGU inawakalia yaani iko juu yao, yaani MUNGU ana hasira nao.
Zaburi 78:56-59 '' Lakini walimjaribu MUNGU Aliye juu, wakamwasi, Wala hawakuzishika shuhuda zake. Bali walirudi nyuma, wakahaini kama baba zao; Wakaepea kama upinde usiofaa. Wakamkasirisha kwa mahali pao pa juu, Wakamtia wivu kwa sanamu zao. MUNGU akasikia, akaghadhibika, Akamkataa Israeli kabisa.'
Huu ni mfano hai kwamba MUNGU alighadhabika yaani alipata ghadhabu au hasira kali kwa sababu watu hawa waliziandamia sanamu hivyo MUNGU akawakataa.
Hivyo unaweza ukadhani MUNGU yuko pamoja na wewe lakini kumbe wala hayuko pamoja na wewe kwa sababu wewe unafanya ibada ya sanamu na unaziabudu au kuziheshimu sanamu.
Ndugu inawezekana ni wewe ghadhabu ya MUNGU iko juu yako kwa sababu unafanya ibada ya sanamu.
Leo ni nafasi yako ya kutubu na kuacha kufanya ibada za sanamu na kisha kuanzia leo mtii MUNGU katika KRISTO YESU.
Kama uko katika ibada ya sanamu hakikisha unaikimbia ibada hiyo ya sanamu, jitenge nayo ili ghadhabu ya MUNGU isiwe juu yako.
Matendo 17:29 "Basi, Kwa Kuwa Sisi Tu Wazao Wa MUNGU, Haipasi Kudhani Ya Kuwa Uungu Ni Mfano Wa Dhahabu Au Fedha Au Jiwe, Vitu Vyote Vilivyochongwa Kwa Ustadi Na Akili Za Wanadamu."
- Haipasi Kudhani Kwamba Uungu Unaambatana Na Sanamu Wala Jiwe. 
-Fanya Maamuzi Mazuri Hata Kama Waumini Wenzako Watakushangaa. 
-Amua Kumpendeza MUNGU Wa Mbinguni Na Sio Kupendezesha Sanamu Na Midoli.

1 Kor 10:14-15 '' Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu. Nasema kama na watu wenye akili; lifikirini ninyi ninenalo.''

4. Wanaoipinga kweli ya MUNGU kwa uovu.

Hili ni kundi la nne la watu ambao ghadhabu ya MUNGU inawakalia.
Warumi 1:18 '' Kwa maana ghadhabu ya MUNGU imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu.''
Inawezekana ni wewe ndio unaipinga siku zote kweli ya MUNGU ya injili ya KRISTO, hiyo ni hatari mno kwako na ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Inawezekana mafundisho yako siku hizi ni wewe kuwakataza watu kuokoka, hiyo ni hatari mno kwako na ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Inawezekana ni wewe unamkataa ROHO MTAKATIFU na humhitaji kabisa, hiyo ni hatari mno kwako na ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Inawezekana ni wewe kwa sasa unapingana na Biblia na unaiona Biblia kuwa ina mapungufu, hiyo ni hatari mno kwako na ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Inawezekana kwa sasa umefuata mafundisho ya mashetani na umejaa kiburi na kulitukana Neno hai la MUNGU wa mbinguni, hiyo ni hatari mno kwako na ghadhabu ya MUNGU inakukalia.
Ndugu hakikisha  ghadhabu ya MUNGU inayotokana na jambo hili haikupati wewe.
Kama ni mhusika tubu dhambi zako, mpokee YESU na anza kumtii ROHO wa MUNGU.

 5. Wanapanga mabaya kwa ajili ya MUNGU na kwa ajili ya Mtumishi wa MUNGU.

Hili ni kundi la tano la watu ambao ghadhabu ya MUNGU inawakalia.
Zaburi 2:2-5 ''Wafalme wa dunia wanajipanga, Na wakuu wanafanya shauri pamoja, Juu ya BWANA, Na juu ya masihi wake. Na tuvipasue vifungo vyao, Na kuzitupia mbali nasi kamba zao. Yeye aketiye mbinguni anacheka, BWANA anawafanyia dhihaka. Ndipo atakaposema nao kwa hasira yake, Na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake.''
Wako wako kwenye vita na watumishi wa MUNGU kwa uonevu kabisa,  hao hawajitambui na ghdhabu ya MUNGU inawakalia.
Wako watu hujaribu kupanga mabaya juu ya kazi ya MUNGU, hao hawajitambui na ghdhabu ya MUNGU inawakalia.
Akina Miriamu walijaribu kupanga mabaya dhidi ya Musa Mtumishi wa MUNGU lakini waliambulia tu ukoma maana ghadhabu ya MUNGU ilikuwa juu yao.
Hesabu 12:1-10 '' Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. Wakasema, Je! Ni kweli BWANA amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? BWANA akasikia maneno yao.   .............................. Hasira za BWANA zikawaka juu yao; naye akaenda zake. Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma.''
Wako watu kwa sababu ya utajiri, ufahari au vyeo hujaribu  kutengeneza bifu(Kuanzisha vita na Watumishi waaminifu wa MUNGU) lakini huishia pabaya sana maana ghadhabu ya MUNGU imewakalia.
Ndugu usiwe ni wewe ndio ghadhabu ya MUNGU inakukalia kwa sababu una vita na watumishi wa MUNGU kwa sababu tu wanahubiri injili ya KRISTO YESU iokoayo.

"Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo ROHO ayaambia makanisa.-Ufunuo 3:22 ''
Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
Bwana YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na Bwana YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee Bwana YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
+255714252292(Hadi whatsapp).
+255786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu. Ukiweza pia toa copy na kuwasambazia watu wengi zaidi.

Comments