MAOMBI YA KUHARIBU FALME ZA PEPO WABAYA.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.

Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU kisha tuombe maombi ya ushindi.
Kuna aina nyingi za maadui katika ulimwengu wa roho.
Leo tunahusika kimaombi kuharibu falme za pepo wabaya.
Shetani ndiye mfalme wa ufalme wa giza wote, katika huo ufalme wa giza kuna wafalme walio chini ya shetani ambao nao ni wafalme wa giza. Biblia inaonyesha kwamba wako watu bado wanatawaliwa na ufalme wa giza na wako watu ambao walishatoka katika ufalme wa giza na sasa wako katika ufalme wa nuru unaongozwa na YESU KRISTO Mwokozi.
Waefeso 2:2 ''ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi;''

Sisi haitusumbui kuona kwamba tuna vita na wafalme wa giza bali tunajua tuna nguvu kuu katika KRISTO YESU ya kuwashinda wafalme wa giza wote.

Falme za giza ni nini?
Falme za giza ni utawala wa kishetani unaofanya kazi kinyume na watu wa MUNGU.
Ufalme wa giza ni eneo ambalo liko chini ya mfalme wa giza.
Sasa katika vita ya kiroho wakati mwingine huwa unajulishwa kupitia ndoto au maono ili ujue ni vita ya namna gani unapigana kiroho.
Biblia inasema kwamba vita yako inaweza kuwa kati ya wewe na falme za giza au kati ya wewe na mamlaka za kipepo, au kati ya wewe na wakuu wa giza na au kati ya wewe na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.
Waefeso 6:12-13 '' Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za MUNGU, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.''

Kwa sababu leo nazungumzia tu vita na falme za giza ngoja tuone kwa uchache vita ya falme ikoje.
Jambo la kwanza unatakiwa kujua wewe muombaji ni kwamba unapopigana vita na falme ujue unapigana vita ya kiroho iliyo kubwa sana yaani unapigana na utawala  nzima ya ufalme wa giza hivyo unaweza ukawa unazuilika katika kila eneo unalohitaji ushindi kiroho.
Kama ndoa yako iko katika vita na falme za giza  ujue vita hiyo ni kubwa lakini katika jina la YESU KRISTO ushindi ni rahisi tu kuupata.
Kama suala lako la kufunga ndoa linazuiliwa na falme za giza ujue uko katika vita kubwa lakini kama wewe ni muombaji, umeokoka na unaishi maisha matakatifu ya Wokovu hakika ushindi dhidi ya falme za giza ni jambo rahisi sana.
Kuna tofauti kati ya kupigana kiroho na adui mmoja  na kupigana na falme.
Kumbuka wewe uliyeokoka umewekwa juu ya falme za giza zote hivyo ukiijua nafasi yako kiroho na ukaitumia vyema kimaombi hakika hakuna falme ya giza itakuzuilia baraka yako au fursa yako au afya yako n.k
Yeremia 1:10a '' angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung'oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza;''

 Kama unapigana vita ya kiroho na falme za giza ujue kwamba vita yako itahusisha kila eneo unalohitaji kufanikiwa, hapo ndipo unagundua tofauti ya vita ya kiroho inayohusisha falme za giza na ile inayohusisha adui mmoja.
Mfano inawezekana kuna adui jini ametumwa kukuzuilia kupata mchumba, huyo jini unaweza kumpiga kwa maombi mara moja akakimbia na wewe ukapata mchumba maana vita yako na adui huyo jini iliisha alipokimbia baada ya wewe kumpiga kimaombi kupitia jina la YESU KRISTO.
Lakini kama uko katika vita na ufalme wa giza ujue vita inakaba kote.
Kwa hiyo ukiwa katika vita ya kiroho inayohusika kila eneo la maisha yako kuhusu baraka fulani wakati mwingine hapo unatakiwa kugundua kwamba unapambana na ufalme wa giza na sio adui mmoja tu.  Lakini haijalisha adui zako ni falme au ni kikundi au ni wawili au watano bado maombi kupitia jina la YESU KRISTO utawashinda wote.
Maadui wako wengi katika ulimwengu wa roho lakini kwa damu ya YESU KRISTO na kwa jina la YESU KRISTO tunashinda na zaidi ya kushinda.
Inawezekana maadui zako wanakupangia mabaya sana, ndugu wala usihofu maana MUNGU wa mbinguni ndiye mkuu kuliko wote katika ulimwengu wa roho hivyo kimbilia kwake kupitia YESU KRISTO utakaa salama.
Zaburi 41:5 ''Adui zangu wananitaja kwa maneno mabaya, Atakufa lini, jina lake likapotea?''

Ngoja nikupe mifano hai wa namna ambavyo unaweza kujua kama unapambana na falme  na sio adui mmoja.
Unaweza ukapigana sana kiroho dhidi ya maadui ambao wanakuzuilia kupata mchumba, ukiwashinda kiroho unapata Mchumba lakini unashangaa vita kubwa mpya inatokea upande wa wazazi wako au wazazi wa mchumba wako, ni vita isiyo na maana kabisa na hao wazazi wanasimama kidete kuhakikisha wewe na mchumba wako hamfungi ndoa. Ukifanikiwa kuomba na kushinda vita hiyo na wazazi wanawakubali na kuwapenda sana unashangaa vita inahamia kwenye mahari, unashangaa unapangiwa mahari  kama unaenda kununua gari jipya la gharama, ili tu ushindwe kutoa mahari na uchumba ufe, ukifanikiwa kutoa mahari, unashangaa kuna vita kwa baadhi ya ndugu wakitaka kugomea harusi ili tu wewe usifunge ndoa. Unashangaa uchumi wako unapigwa, unashangaa kila mtu anakuwa hayuko upande wako, yaani hadi siku ya ndoa inafika mlio pamoja ni nyie tu wawili yaani wewe na mchumba wako. Wakati mwingine ukiona vina inayoendana na hiyo kwenye maisha yako ujue unapigana na falme za giza, wala usiwalaumu watu au kuwachukia kwamba wanataka kukukwamisha kupata baraka yako, bali pigana vita ya kiroho dhidi ya falme za giza na utashinda kupitia maombi yako ya imani katika KRISTO YESU.
Unashangaa unapambana sana kupata kazi, wengine wanafunga na kuomba siku moja tu kisha wanapata kazi lakini wewe umefunga na kuomba hata mara 20 na sifa za kupata kazi hiyo unazo kuliko hata hao waliopata kazi eneo hilo hilo, ukifanikiwa kushinda vita hiyo ya kiroho unapata kazi na unadhani vita imeisha lakini hapo hapo unashangaa unaanza kupigwa vita kazini kwako na kila mtu bila hata kosa, unashangaa kupata mshahara inakuwa mtihani kwako japokuwa wengine mlioajiriwa nao pamoja wao wanapokea mishahara yao,  ukishinda vita hiyo unaanza kupata mshahara wako lakini unashangaa kila ukipata mshahara wanaokuhusu wanaumwa sana hivyo mshahara wako unaishia kuwatumia wao ili wakatibiwe hospitalini, ukiona mambo kama hayo wakati mwingine tambua kwamba unapambana na falme za giza, hivyo usiishie tu kuomba maombi kwamba ''Ewe mchawi ushindwe", omba vita ya kuharibu falme za giza.
Zaburi 38:19 ''Lakini adui zangu ni wazima wenye nguvu, Nao wanaonichukia bure wamekuwa wengi.''

UTAJUAJE KAMA UNAPAMBANA NA FALME NA SIO ADUI MMOJA?

1. Kufununuliwa kwa kupitia ndoto au maono.
Kuona ndotoni au kwenye maono ukipambana na maadui wengi.
Ayubu 33:14-15  ''Kwa kuwa MUNGU hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali. Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani; ''
Maadui hao unaweza kuwaona ndotoni wakiwa ni wanadamu au wanyama wakali wa aina tofauti tofauti. Mfano unaona unafukuzwa na nyoka, mara anatokea mamba akitaka akumeze, mara ng'ombe au paka akitaka kufanya kitu kibaya kwako, mara unaona panya wanakula vitu vyako n.k

2. Unapokutana na vita katika kila eneo la mchakato wa kuipata baraka yako.
Zaburi 42:10-11 '' Watesi wangu hunitukana mithili ya kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi MUNGU wako? Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini MUNGU; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na MUNGU wangu. ''

 3. Unapojikuta katika hali halisi uliyonayo una maadui wengi sana.
Zaburi 69:4 '' Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.''

5. Unapokimbiwa na watu wako wa karibu wengi.
Zaburi 69:8 '' Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu.''

 Maombi unayotakiwa kuomba ili uzishinde falme za giza.

1. Tubu mbele za MUNGU kwa kila kilichosababisha milango kufunguliwa ya madui kutoka falme za giza kukuonea.
Isaya 59:1-2 '' Tazama, mkono wa BWANA haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na MUNGU wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia. ''

2. Funga milango yote wanayoitumia pepo wabaya kuingia maishani mwako na kufanya uharibifu.
Mathayo 18:18 ''Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.''
 
 3. Bomoa na kuharibu falme za kipepo zote dhidi yako, zitaje kwa majina.
Yeremia 18:7 '' Wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung'oa, na kuuvunja, na kuuangamiza; ''

 4. Mpige kwa moto wa jina la YESU KRISTO kila mshirika wa ufalme wa giza anayekufuatilia.
Zaburi 2:9 ''Utawaponda kwa fimbo ya chuma, Na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.''

5. Komboa baraka zako zote kwa damu ya YESU KRISTO, zitaje baraka hizo unazozikomboa.
Hosea 13:14 ''Nitawakomboa na nguvu za kaburi; nitawaokoa na mauti; ewe mauti, ya wapi mapigo yako? Ewe kaburi, ku wapi kuharibu kwako? Kujuta kutafichwa na macho yangu.''

 Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane na nitakujulisha jinsi ya kukipata na Naamini kitakusaidia sana.
Hapa chini ni
MAOMBI YA KUHARIBU FALME ZA GIZA UNAZOPIGANA NAZO.
 Maombi haya naomba yamsaidie mtu yule ambaye hajui kuomba ili katika kuomba kwa kutumia hayo basi atakumbuka mahitaji yake na kuyataja katika maombi yake. Haya hapa chini ni maombi ya kuanzia tu katika maombi yako ili uendelee zaidi kuomba
Kwa waombaji wazoefu naamini baada tu ya kulisoma somo na kulielewa basi anajua aombee nini maana alikuwa anaandika points za kuombea. Kumbuka pia fundisho ni muhimu kuliko maombi hivyo wewe ambaye huwa unahusika na maombi tu hakikisha unajifunza kwanza somo lote ndipo utapata nguvu za kuomba na kushinda. 


 MAOMBI YA KUHARIBU FALME ZA GIZA UNAZOPIGANA NAZO.


 Niko mbele zako BABA wa mbinguni na nahitaji msaada wako wewe MUNGU Muumbaji wangu.
Nakushukuru umenilinda na kunipa uzima hata sasa.
Naomba unisamehe dhambi zangu zote, makosa yangu yote na maovu yangu yote, ninatubu mbele zako Bwana YESU na ninaomba damu yako ya thamani sana  ya agano jipya initakase na kunifutia dhambi zangu zote.
Ninatubu pia kwa ajili ya kila nilichokifanya hata nikaruhusu ufalme wa giza kuvamia maisha yangu na baraka zangu.
Ninatubu kwako JEHOVAH MUNGU mweza yote naomba BWANA unirehemu na kunisamehe na sasa milango hiyo waliyoitumia maadui kutoka falme za giza, hiyo milango ijifunge  sasa na hawatakuwa na uhalali tena wa kunionea au kuonea lolote katika maisha yangu.
Eee MUNGU Muumbaji wangu niko mbele zako sasa ninaomba ''Maneno ya kinywa changu, Na mawazo ya moyo wangu, Yapate kibali mbele zako, Ee BWANA, Mwamba wangu, na mwokozi wangu. ''  kama Zaburi 19:14 inavyosema.
''Ee BWANA, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao shimoni, Ikiwa umeninyamalia. Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu. '' Kama Neno lako linavyosema katika Zaburi 28:1-2
'' Unitegee sikio lako, uniokoe hima. Uwe kwangu mwamba wa nguvu, Nyumba yenye maboma ya kuniokoa. Ndiwe genge langu na ngome yangu; Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge.  Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri, Maana Wewe ndiwe ngome yangu.'' Kama Neno lako linavyosema katika Zaburi 31:2-4  
Maombi yangu ya leo nataka kukomesha kila kusudi la ufalme wa giza dhidi ya maisha yangu, familia yangu, biashara yangu, uzao wangu, kazi yangu, huduma yangu na uchumi wangu.
Bwana YESU Mwokozi wangu ulinipa kibali ukisema ''yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni;''
Hivyo sasa kwa mamlaka iliyo katika jina lako Bwana YESU ninafunga milango yote waliyoitumia mawakala wa shetani kutoka falme za giza kuja katika maisha yangu. Ninaifunga milango hiyo ya kipepo, kwa damu ya YESU KRISTO.
Kila iliko hiyo milango ninaifunga kwa damu ya YESU KRISTO. Milango ya kipepo  iliyo katika fahamu zangu, na milango iliyo katika mwili wangu, yote naifunga kwa jina la YESU KRISTO.
Milango iliyo katika maagano ya ukoo au katika ardhi naifunga hiyo milango kwa damu ya YESU KRISTO.
kokote iliko milango inayowapa uwezo mawakala wa shetani kuingilia baraka zangu na maisha yangu, hiyo milango naifunga kwa damu ya YESU KRISTO Mwokozi aliye hai.
Sasa nawapiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO kila maadui zangu kutoka ulimwengu ufalme wa giza unaoshindana na mimi.
Neno la MUNGU linanipa kibali likisema ''''Utawaponda kwa fimbo ya chuma, Na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.''  ''
Sasa Maadui wote walio mapepo/majini na mizimu wanaotoka ufalme wa giza kuja kwangu au kwenye baraka zangu, nawaponda na kuwapiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO.
 Maadui wachawi wote na wakuu wa giza  wote wanaotoka ufalme wa giza kuja kwangu au kwenye baraka zangu, nawaponda na kuwapiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO.
Maadui washirikina wote wa wanga wote  wanaotoka ufalme wa giza kuja kwangu au kwenye baraka zangu, nawaponda na kuwapiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO.
Maadui wote waliovaa sura za nyoka, paka au kiumbe yeyote wanaotoka ufalme wa giza kuja kwangu au kwenye baraka zangu, nawaponda na kuwapiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO.
Kila adui kutoka falme za giza anayefuatilia maisha yangu, ndoa yangu, uchumba wangu, afya yangu, kipato changu, kazi yangu, uzao wangu na kila baraka yangu yeyote, huyo adui namponda na kumpiga kwa moto wa jina la YESU KRISTO.
Sasa naikomboa kila baraka yangu iliyokuwa imezuiliwa na mawakala wa shetani wote.
Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya kiuchumi.
Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya ya ndoa
 Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya uchumba
 Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya kazi na biashara.
 Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya kununua kiwanja na kujenga nyumba.
 Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya uzao, nawakomboa ndugu zangu na watoto wangu.
 Kwa damu ya YESU KRISTO na katika jina la YESU KRISTO naikomboa baraka yangu ya afya, nafuta kila ugonjwa ulioletwa na falme za giza, naufuta ugonjwa huo kwa damu ya YESU KRISTO ya agano.
Nakushukuru MUNGU wangu maana katika wewe ni leo nimeshinda falme za giza zote.
Kuanzia sasa sitazuilika katika kufanikiwa katika maisha yangu sawasawa na kusudi la MUNGU.
Katika jina la YESU KRISTO nimeomba na sasa ninashukuru
 Amen Amen Ameeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeen.
Hakika umeshinda. Ukiweza kufunga unaweza kufunga hata siku 1 au 3 au 4 au hata 5 au zile ambazo wewe utaona unaweza ukihusika kila siku na kipengele kuombea na kumbuka baada ya maombi ya kufunga au hata maombi ya bila kufunga fanya tendo la imani kwa MUNGU kwa kutoa sadaka nzuri itakayoambatana na maombi juu ya ukomo wa kuteswa na maadui zako katika ulimwengu wa roho
Nawaonya pia wanaotumia masomo yangu vibaya na kwa manufaa yao waache tabia hiyo.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
Bwana YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na Bwana YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee Bwana YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
+255714252292(Hadi whatsap).
+255786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.


Comments