SIFA ZA MTUMISHI ALIYEITWA NA MUNGU.

Na Mwl Peter Mabula 
Mtenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi 



Bwana YESU KRISTO atukuzwe ndugu zangu wote.
Karibuni tujifunze neno la MUNGU.

✓✓Tunafahamu ya kwamba MUNGU anaweza kumwita yeyote ili amtumikie katika Injili.

✓✓MUNGU anaweza kumwita mtu ambaye anajiona hawezi.

✓✓MUNGU anaweza kumwita mtu asiyestahili na sasa akamsitahilisha.

Mfano ni mtume Paulo ambaye kabla hajaokoka alikuwa hastahili maana alikuwa muuaji na katili, lakini YESU akamwita,akamuokoa na akamfanya kuwa mtenda kazi katika kazi ya injili.
Lakini aliitwa kutokea kwenye kundi la mtu asiyestahili.

✓✓MUNGU anaweza kukuita hata wewe uliyekataliwa.

✓✓MUNGU anaweza kumwita hata mtu asiyeaminika mbele za watu.

Mfano ni Musa ambaye aliitwa na MUNGU lakini wakati  anaitwa alijijua kabisa kwamba yeye haaminiki mbele za watu.

Kutoka 4:1 "Musa akajibu akasema, Lakini, tazama, hawataniamini, wala hawataisikia sauti yangu; maana watasema, BWANA hakukutokea."

✓✓Hata wakatia mwingine MUNGU anaweza kumwita hata mtu mnyonge ili awe mtumishi wake katika KRISTO YESU.

✓✓MUNGU anaweza kuwaita hata watu wasio na ushawishi.

Mfano ni Yeremia ambaye alijiona ni mdogo kiumri hivyo hawezi kuwashawishi watu wazima, wenye mamlaka, wafalme na watu wote maana alijiona hana ushawishi.
MUNGU anaweza kumwita hata mtu asiye na ushawishi.

Yeremia 1:6 "Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto."

✓✓MUNGU anaweza kumwita hata mtu asiye na kitu.

✓✓MUNGU anaweza kumwita hata mtu asiyesoma.

Lakini kama ni MUNGU amemwita mtu huyo basi ni MUNGU katika KRISTO YESU atamstahilisha mtumishi huyo maana ni MUNGU ndiye hufanya kazi ndani ya watumishi wake hivyo kila kitu huwezekana.

Wafilipi 2:13 "Kwa maana ndiye MUNGU atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema."

✓✓Sasa, japokuwa kuna watumishi wengi wa kweli wa MUNGU katika KRISTO YESU lakini pia ni muhimu kujua kwamba hata shetani naye ana watumishi wake.

Kuna watumishi wa MUNGU na kuna watumishi wa shetani.

✓✓Kuna watumishi walioitwa na MUNGU na kuna watumishi waliojiita.

✓✓Kuna watumishi waliotumwa na KRISTO lakini pia kuna watumishi waliotumwa na dhehebu hivyo wao hufanya kazi ili kulipendeza dhehebu na sio kumpendeza MUNGU katika KRISTO YESU.

Kuna watumishi wengi lakini sio wote ni watumishi wa MUNGU hivyo ni vyema tukawajua watumishi wa kweli wa MUNGU katika KRISTO YESU ili iwe rahisi kuwajua watumishi walijiingiza kwa siri.

Ukiambatana na watumishi waliojiingiza kwa siri kwenye mambo ya kiroho utapotezwa, hao ni watumishi feki, ni watumishi wa shetani na sio watumishi wa YESU KRISTO.

Yuda 1:4 "Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya MUNGU wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu YESU KRISTO."

Kaa mbali sana na watumishi ambao hawajaitwa na MUNGU katika KRISTO YESU Mwokozi. 

Sasa ili uwatambue watumishi feki ni vyema ukazijua kwa usahihi sifa za watumishi wa kweli wa MUNGU katika KRISTO YESU Mwokozi.

Sifa za watumishi wa MUNGU walioitwa na MUNGU mwenyewe ili wamtumikie katika KRISTO YESU ni hawa ;

1. Ameokoka na YESU KRISTO ni Bwana na Mwokozi wake.

Wagalatia 1:15-16 " Lakini MUNGU, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake, alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu; ."

Mtume Paulo ni mfano hai wa mtumishi aliyeitwa na MUNGU ili amtumikie.
Hapo anasema kwamba ni MUNGU alimdhihilisha YESU kwa Paulo hata Paulo akampokea YESU kama Mwokozi wake na tangu hapo Paulo akawa mtumishi wa Bwana YESU daima.

◼️Hata sasa mtumishi yeyote wa kweli wa MUNGU ni lazima awe ameokolewa kwanza na YESU KRISTO, ukiona mtu hajaokoka harafu ajiita mtumishi ujue huyo bado hajaitwa na MUNGU bali amejiita.

✓✓Mtumishi wa kweli wa MUNGU ni lazima awe ameokolewa kwanza na YESU KRISTO.

2. Ana Neno la MUNGU.

Wakolosai 3:16-17 " Neno la KRISTO na likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkifundishana na kuonyana kwa zaburi, na nyimbo, na tenzi za rohoni; huku mkimwimbia MUNGU kwa neema mioyoni mwenu. Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana YESU, mkimshukuru MUNGU Baba kwa yeye."

✓✓Mtumishi wa MUNGU lazima awe na neno la MUNGU.

✓✓Neno hilo la MUNGU ndio pia Neno la KRISTO na kwa hilo tunafundishana na kuonyana.

◼️Mtumishi mwenye Neno la MUNGU hufundisha Neno la MUNGU.

Ukiona mtumishi anafundisha vitu vya ajabu ajabu ujue huyo hana Neno la MUNGU.

Watumishi wa MUNGU wa kweli MUNGU huwapa Neno lake katika Wokovu wa KRISTO YESU.

3. Analitangaza jina la YESU KRISTO kama Mwokozi.

Matendo 9:15 "Lakini BWANA akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli."

Andiko hili linamzungumzia mtume Paulo alipoitwa na MUNGU.

Andiko hili ukilisoma katika tafsiri ya BHN linamaanisha kwamba Mtume Paulo amepewa jina la YESU KRISTO ili alitangaze kwa mataifa yote.

◼️Kumbe mtumishi wa kweli wa MUNGU analibeba jina la YESU KRISTO Mwokozi na kulitangaza kwa watu ambao anawahubiria yaani ambao anatumika kwao.

◼️Kila mtumishi wa kweli wa MUNGU amepewa jina la YESU KRISTO ili kulitangaza hata watu wote wafanyike wateule wa KRISTO walio tayari kwa uzima wa milele.

✓✓Ukiona mtumishi anatangaza vitu vingine na sio jina la YESU KRISTO ujue huyo sio mtumishi aliyeitwa na MUNGU.

4. Ana ROHO MTAKATIFU na anaenenda katika ROHO MTAKATIFU.

Mfano hai ni huu.

Isaya 42:1-2 " Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu."

✓✓Ni MUNGU ndiye anasema anapomwita mtu katika utumishi, MUNGU anasema kwamba "Nitatia roho yangu juu yake"

◼️Ni lazima watumishi wote wa kweli wa MUNGU, ni lazima watumishi hao wawe na ROHO MTAKATIFU.

Warumi 8:14 "Kwa kuwa wote wanaoongozwa na ROHO wa MUNGU, hao ndio wana wa MUNGU."

◼️YESU KRISTO ndiye msingi wa imani yetu kama Wakristo na ROHO MTAKATIFU ndiye hutupa hakikisho la Wokovu wetu.

◼️ROHO MTAKATIFU ndiye humfunua KRISTO kwetu, hivyo mtumishi asipokuwa na ROHO MTAKATIFU hawezi kuwa mtumishi wa kweli wa MUNGU.

1 Wakorintho 12:3 "Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika ROHO wa MUNGU, kusema, YESU amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, YESU ni Bwana, isipokuwa katika ROHO MTAKATIFU."

5. Anafanya kazi ya MUNGU aliyoagizwa na MUNGU katika KRISTO YESU.

1 Wakorintho 12:4-7 "Basi pana tofauti za karama; bali ROHO ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana(YESU) ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali MUNGU ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa ROHO kwa kufaidiana."

6. Anaishi maisha matakatifu na ni kielelezo katika utakatifu.

1 Petro 1:14-16 " Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu."

7. Anakaa ndani ya KRISTO na kuzaa matunda mema.

Yohana 15:4-8 "Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.
Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu."

Mche MUNGU katika KRISTO YESU Mwokozi na utaitwa heri.
Kama pia unatumia Facebook ni follow maana itafika kipindi nitakuwa napost tu katika page yangu na profile yangu.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
Bwana YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na Bwana YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee Bwana YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
By Mwl Peter  Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi.
+255714252292(Ni namba hii kupiga, sadaka ya kuipeleka Injili,kuandika meseji na  whatsapp).
Ubarikiwe sana.

Comments