![]() |
| Na Mwl Peter Mabula Mtenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi |
Bwana YESU KRISTO Mwokozi atukuzwe rafiki.
Karibu Tujifunze Neno la MUNGU.
◼️Ukisoma Matendo 12:3-17 unaona Nguvu ya Maombi inavyofanya kazi.
◼️Unaona Petro akiwekwa gerezani na Mfalme wakati wa Pasaka na Lengo la Mfalme lilikuwa baada ya Pasaka amtoe na kumsulubisha mbele za watu.
◼️Tunaona Kanisa likiomba kwa juhudi kwa ajili ya Petro.
Matendo 12:5 "Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba MUNGU kwa juhudi kwa ajili yake."
◼️Tunaona Maombi yakasababisha Malaika aje kumtoa Petro gerezani (Matendo 12:7)
◼️Wakati Petro ameshatolewa gerezani Kanisa liliendelea kuomba bila kujua kwamba Petro wanayemuombea ameshatoka gerezani tayari(Matendo 12:12)
◼️Ingawa Kanisa walikuwa waombaji wazuri waliomba Petro atoke gerezani lakini hata walipomuona Petro hawakuamini kama ndiye Petro na kama kweli ametokea gerezani(Matendo 12::14-15)
◼️Hawa waliomba ila mashaka yalikuwa mengi kwao.
Hata Leo Kanisa na watu wa MUNGU katika KRISTO YESU Kila mahali wanafanya Maombi Kila mara ila ni vizuri pia Kila Muombaji kutambua mitindo au style za MUNGU kujibu Maombi.
➡️Nimetafuta neno la kiswahili lenye maana ya "Style" ili nieleweke zaidi nimepata neno "Mitindo" hivyo kama hujaelewa "Mitindo ya MUNGU kujibu Maombi" basi maana yake ni "Style/Staili ya MUNGU kujibu Maombi"
Zaburi 118:5 "Katika shida yangu nalimwita BWANA; BWANA akanijibu akaniweka panapo nafasi."
✔️Maana ya mtindo ni namna ya kufanya jambo, hivyo Mitindo ya MUNGU kujibu Maombi maana yake atafanyaje wakati wa kujibu.
◼️MUNGU husikia Maombi ya Wateule wake katika KRISTO YESU.
Zaburi 66:20 "Na ahimidiwe MUNGU asiyeyakataa maombi yangu, Wala kuniondolea fadhili zake."
➡️Mfano hai ni hapa ambapo MUNGU alisikia Maombi ya Yona akiwa ndani ya tumbo la Nyangumi chini ya maji baharini.
Yona 2:7 "Roho yangu ilipozimia ndani yangu, Nalimkumbuka BWANA; Maombi yangu yakakuwasilia, Katika hekalu lako takatifu."
◾Mitindo ya MUNGU kujibu Maombi ya Wateule wake katika KRISTO YESU.
1. Kujibu Maombi muda ule ule unaomba.
➡️Mfano hai ni Maombi ya Paulo ya kutoa mapepo ndani ya kijakazi mmoja yalijibiwa wakati ule ule na mapepo yakatoka muda ule ule.
Matendo 16:18 "Akafanya hayo siku nyingi. Lakini Paulo akasikitika, akageuka akamwambia yule pepo, Nakuamuru kwa jina la YESU KRISTO, mtoke huyu. Akamtoka saa ile ile."
◼️Maombi ya kuondoa Nguvu za giza ndani ya watu mengi hujibiwa wakati ule ule.
Marko 1:27 "Wakashangaa wote, hata wakaulizana, wakisema, Nini hii? Ni elimu mpya! Maana kwa uweza awaamuru hata pepo wachafu, nao wamtii!"
➡️Kuna Maombi hujibiwa wakati ule ule unaomba, Mfano hai Mwingine ni Maombi ya Eliya ya kushusha moto yalijibiwa muda huo huo anaomba.
1 Wafalme 18:36-38 " Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee BWANA, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe MUNGU katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. Unisikie, Ee BWANA, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, BWANA, ndiwe MUNGU, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. Ndipo moto wa BWANA ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji."
2. Kujibiwa kabla hujaomba.
Isaya 65:24 "Na itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia."
◼️Hapa ni ile Nia tu ya kuhitaji Kitu fulani ukasema moyoni " ngoja nije niombe kwa MUNGU au nifunge kwa ajili ya kitu fulani" yaani wakati unawaza tu kutafuta muda wa kuomba MUNGU anajibu.
Mathayo 6:8 "Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba."
◼️MUNGU anaweza akajibu hata mawazo Yako tu kabla hata hujaomba.
◼️Kabla hujaomba MUNGU anaweza akakujibu maana yeye anajua yote.
◼️MUNGU anaweza akatenda mambo makubwa kuliko hata ambayo utaomba.
Waefeso 3:20 "Basi atukuzwe yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo, kwa kadiri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu;"
3. Kujibiwa baada tu ya kumaliza kuomba.
➡️Mfano hai ni huu
2 Wafalme 6:17 "Elisha akaomba, akasema, Ee BWANA, nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. BWANA akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote."
➡️Elisha aliomba Maombi ya kufumbua macho ya Gehazi na alipomaliza tu kuomba MUNGU akajibu pale pale, alipomaliza tu kutamka majibu ya MUNGU yakatokea.
➡️Mfano Mwingine MUNGU alimsikia Hezekia akajibu kwa kuwaponya watu.
2 Nyakati 30:20 "BWANA akamsikia Hezekia, akawaponya watu."
➡️Mfano Mwingine ni Hezekia na Isaya waliomba na MUNGU siku hiyo hiyo akamtuma Malaika kuwaangamiza adui zao.
2 Nyakati 32:20-21 " Na kwa ajili ya hayo Hezekia mfalme, na Isaya nabii, mwana wa Amozi, wakaomba, wakalia hata mbinguni.
Naye BWANA akatuma malaika aliyewakatia mbali mashujaa wote, na majemadari, na maakida, matuoni mwa mfalme wa Ashuru. Basi akarudia nchi yake mwenye haya ya uso. Naye alipoingia nyumbani mwa mungu wake, wale waliotoka viunoni mwake mwenyewe wakamwangamiza humo kwa upanga."
◼️Ndugu omba kwa MUNGU katika Jina la YESU KRISTO ukiamini maana Maombi mengine MUNGU hujibu mara tu Wewe ukimaliza kuomba.
4. Kujibiwa Maombi wakati wa tendo la Imani la maelekezo ya ROHO MTAKATIFU rohoni.
◾Ngoja nikupe mifano hai 4 ili unielewe vizuri.
➡️Petro alimuombea kilema lakini alipofanya tendo la Imani la kumnyanyua ndipo kilema kikaondoka.
Matendo 3:6-7 "Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la YESU KRISTO wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu."
➡️Hamani ili apone ukoma mahitajio ya ulimwengu wa roho ilikuwa aende mtoni kujichovya mara Saba.
2 Wafalme 5:14 "Ndipo akashuka, akajichovya mara saba katika Yordani, sawasawa na neno lake yule mtu wa MUNGU; nayo nyama ya mwili wake ikarudi ikawa kama nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi."
◾Unaweza ukajiuliza kwanini hadi aende mtoni ndipo apone, kwanini asiwekewe tu mkono na Watumishi wa MUNGU akapona? Hata Mimi Peter Mabula sijui ila ni vizuri sana tukamwelewa MUNGU.
◾Ndugu mwelewe MUNGU na Mitindo yake ya kujibu Maombi, Ufunuo wa ROHO MTAKATIFU ni wa Muhimu sana katika Maombi.
➡️Wakoma hawakupona wakati ule ule ila walipoenda kujionyesha kwa kuhani kama walivyoambiwa ndipo walipona.
Luka 17:12-14 " Na alipoingia katika kijiji kimoja, alikutana na watu kumi wenye ukoma; wakasimama mbali, wakapaza sauti wakisema, Ee YESU, Bwana mkubwa, uturehemu! Alipowaona aliwaambia, Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani. Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika."
➡️Hata Waisraeli wakati wa Yehoshafati ilibidi wakafanye tendo la Imani la Ufunuo ili kushinda vita( 2 Nyakati 20:13-17"
◾Hata wewe unaweza Mfano ukaombewa na baada ya Maombi ukasikia msukumo wa kushuhudia Injili mitaani kumbe tendo hilo la Imani limebeba Muujiza wako.
◾Mfano unaweza ukaombewa na ndani Yako ukasikia msukumo wa Sadaka fulani ya kipekee kumbe hilo ni tendo la Imani linaloleta majibu Yako ukizingatia.
Somo litaendelea kesho katika sehemu 3 zilizobaki za Mitindo ya MUNGU kujibu Maombi, usikosea hapa hapa.
Naamini umejifunza jambo zuri na utafanyia kazi.
Asante kwa kujifunza Neno la siku ya leo, Kabla sijamaliza nakuomba Wewe ambaye hujaokoka au uliokoka ukarudi nyuma, nakusihi sana amua Leo kumpokea YESU KRISTO kama Mwokozi wako na Jina lako litaandikwa katika kitabu Cha uzima Mbinguni, katika maeneo Yako tafuta Kanisa safi la kiroho linalohubiri Wokovu wa KRISTO YESU nenda kamweleze Mchungaji atakuongoza Sala ya Toba utaokoka Kisha baada ya hapo fuata mafundisho ya Neno la MUNGU hapo Kanisani.
MUNGU wa Mbinguni akubariki sana.
By Mwl Peter Mabula
Mtenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi.
+255714252292 ( kwa Ushauri, maombezi, pamoja na Whatsapp)
Ubarikiwe.

Comments