HISTORIA YA MAISHA YA BAHATI BUKUKU (Sehemu ya 2)




  • Bahati Bukuku.
    Nilipenda kwenda shule kusoma, na hii ilikuwa njia mojawapo ya kuepuka kufanya kazi za nyumbani, hasa kuosha vyombo kitu nilichokuwa nikikichukia mno. Japokuwa nilikuwa mtoto mdogo lakini mama alijitahidi sana kuniweka katika mazingira ambayo mtoto wa kike anatakiwa kuwa. Achukia kuosha vyombo Kila siku alikuwa akinitaka nioshe vyombo, hii ilikuwa kazi pekee niliyokuwa nikiichukia mno. Kila nilipokuwa nikirudi nyumbani, mama alikuwa akinipa maziwa na kiporo cha jana, nikimaliza kula, alikuwa akiniambia nioshe vyombo nilivyovitumia. Nilikereka mno lakini sikuwa na jinsi, nilibaki nikilalamikalalamika lakini mwisho wa siku niliosha vyombo mbele yake huku akionekana kuwa na furaha.

                     AWA KIONGOZI WA KUIMBA

    Ijulikane kwamba kuimba ni kipaji nilichozaliwa nacho. Nakumbuka kipindi hicho mimi ndiye nilikuwa kiongozi wa nyimbo mbalimbali tulizokuwa tukiimba shuleni. Sauti yangu haikuwa nzuri, ilikuwa ni ya kukoroma sana lakini kila nilipokuwa nikiimba walimu waliipenda na ilikuwa ni lazima ujue kwamba ‘huyo anayeimba ni Lusako’.

                     AANZA DARASA LA KWANZA

    Baada ya kusoma shule ya chekechea kwa miaka miwili, mwaka 1990 nilitakiwa kwenda kuanza darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Muungano ambayo haikuwa mbali kutoka tulipokuwa tukiishi. Kama kawaida yangu, siku hiyo niliamka asubuhi sana huku nikiwa na hamu ya kuanza darasa la kwanza. Moyo wangu haukuweza kusahau, bado niliendelea kukumbuka miaka miwili iliyopita ambapo nilishindwa kulishika sikio langu la upande wa kushoto kwa kutumia mkono wangu wa kulia kwa kuupitisha kichwani. Kwanza kabla ya yote, hapohapo nyumbani, nikajaribu kulishika sikio langu, nikafanikiwa.

    ACHEKELEA KUJIUNGA NA SHULE YA MSINGI

    Naweza kusema kwamba katika mwaka huo, siku hiyo ndiyo nilikuwa na furaha kupita kawaida. Nilipenda sana shule, kila nilipokuwa nikiwaona wanafunzi wakipita nyumbani huku wakiwa wamevalia sare zao za shule, niliona wivu moyoni. Leo hii na mimi nilitakiwa kwenda kuanza darasa la kwanza! Asubuhi ya siku hiyo, mama akaniletea sketi na shati huku chini nikivalia soksi za pundamilia. Sikuwa na sare za shule hivyo siku hiyo nilivalia nguo za nyumbani ila miguuni nilikuwa na soksi hizo za pundamilia. Baada ya kutembea kwa umbali mdogo, nikaelekea shuleni huku nikiongozana na baba, mzee Bukuku. Watoto waliokuja kuanza shule walikuwa wengi na zoezi lilikuwa lilelile la miaka yote, kushika sikio lako. Wapo walioshindwa ambao walilia kama nilivyofanya miaka miwili iliyopita lakini pia walikuwepo wale waliofaulu na kutakiwa kujiunga na shule hiyo kwa ajili ya kuanza na elimu ya msingi huku nikiwa nimeandikishwa jina jingine na kuitwa Bahati.

                                   AANZA MASOMO

    Niliipenda masomo, niliipenda shule kwa jinsi majengo yake yalivyokuwa. Yalipendeza na kuvutia sana. Siku hiyohiyo ambayo baba alikuwa amenipeleka shuleni hapo, tukaingizwa darasani na kupangwa, siku iliyofuata, tukaanza masomo huku tukiwa watoto zaidi ya arobaini katika darasa moja. Kila mmoja alionekana kuwa na furaha kama nilivyokuwa. Hakukuwa na utulivu, kila wakati wanafunzi walikuwa wakipiga kelele, nadhani kwa walimu au kwa watu waliokuwa katika mitaa yenye watoto wengi watakuwa wanalitambua hili, jinsi watoto wanavyopiga kelele zenye kuleta kero.

                                AONGOZA KWA UTUNDU

    Kati ya wanafunzi wote waliokuwa darasani, mimi ndiye nilionekana kuwa mtundu. Kwanza sikutulia sehemu moja, nilionekana kama mtu aliyekuwa akitafuta kitu fulani, muda huu unaweza kuniona hapa na baadaye kuniona kule.

                            UTUNDU WAMPA UMONITA

    Kutokana na utundu wangu wa muda mfupi, hata mwalimu wa darasa hilo aitwaye Rugemilila alipoingia darasani, akanichagua niwe ‘monita’ yaani kiongozi wa darasa lile. Maisha ya nyumbani yaliendelea kuwa vilevile kwamba kila nilipokuwa nikirudi na kula chakula, mama alinitaka nioshe vyombo. Bado mama alinifundisha mambo mengi huku akitamani sana niwe kama wasichana wengine, nadhani mbele ya maisha yangu aliyaona kwani kwa kile alichokuwa akikitaka ndicho kimeweza kunisaidia sana kipindi hiki.

                         AKAMUA NG’OMBE MAZIWA

    Kazi zote za nyumbani ambazo alikuwa akizifanya mama, ilikuwa ni lazima na mimi nizifanye. Siku ambayo sikuwa nikienda shule, ilikuwa ni lazima nipike japo chai na kufanya usafi nyumbani hapo huku nikisaidiana naye. Nyumbani kulikuwa na ng’ombe, kila siku, hata kabla ya kwenda shule ilikuwa ni lazima niamke asubuhi sana, nikamue maziwa na kisha mtu ambaye alikuwa akihusika kwa ajili ya kwenda kuwachunga akiwatoa zizini na kwenda nao machungoni.

                                 ACHUNGA NG’OMBE

    Hayo ndiyo yalikuwa maisha yangu ya kila siku. Siku ambazo sikuwa nikielekea shuleni, pia nilikuwa nikichukuliwa na kupelekwa machungoni. Nilichukia kazi nyingine lakini hii ya kuwapeleka ng’ombe machungoni niliipenda kwa sababu ilinipa nafasi ya kuondoka nyumbani hapo kwenda kuzurura na ng’ombe hao.

                                       AUZA CHIPSI

    Kutokana na utundu niliokuwa nao na ujanja wa hapa na pale, mwalimu wangu wa darasa akanichagua niuze chipsi zake. Wanafunzi wengi walikuwa wakiitamani kazi hii kwani walijua fika kwamba mara unapouza na nyingine kubaki, walimu huwa na kawaida ya kukupa mfuko mmoja ule.

    MUNGU akubariki na kama hukusoma sehemu ya kwanza ya ushuhuda huu FUNGUA HAPA


     

Comments

Muyabaga said…
Duuuh! Umetoka Mbali aisee,
Nimefurahi kuona nami nilisoma shule ya Msingi ya Muungano ambayo ulisoma na wewe Pia, nabahati njema zaidi, nilipata kusoma na mdogo wako aitwaye Erasto Bukuku.

Mungu akubariki kwa huduma yako ya uimbaji, mana huwa nabarikiwa sana napo sikiliza nyimbo zako.
Muyabaga said…
Duuuh! Umetoka Mbali aisee,
Nimefurahi kuona nami nilisoma shule ya Msingi ya Muungano ambayo ulisoma na wewe Pia, nabahati njema zaidi, nilipata kusoma na mdogo wako aitwaye Erasto Bukuku.

Mungu akubariki kwa huduma yako ya uimbaji, mana huwa nabarikiwa sana napo sikiliza nyimbo zako.