WIVU WA WATUMISHI WA MUNGU

Na Askofu Mkuu Zakaria Kakobe, FGBF


T
unaendelea tena kujifunza Kitabu cha YOHANA katika Biblia zetu.  Leo tunajifunza YOHANA 3:24-36.  Kuna mengi ya kujifunza katika mistari hii, ingawa kichwa cha somo letu ni “WIVU WA WATUMISHI WA MUNGU“.  Tutayagawa mafundisho yote tunayoyapata katika mistari hii katika vipengele vinane:-

(1)KUTIWA GEREZANI KWA WAAMINIO (Mst. 24);
(2)MASHINDANO YA WANAFUNZI WA YOHANA (Mst. 25-26);
(3)WIVU WA WATUMISHI WA MUNGU (Mst. 26-27);
(4)YESU KAMA BWANA ARUSI (Mst. 28-29);
(5)YESU KUZIDI SISI KUPUNGUA (Mst. 30);
(6)YESU KRISTO YU JUU YA YOTE (Mst. 31-33);
(7)ALAMA KUU YA MTUMISHI WA MUNGU (Mst. 34);
(8)JINSI YA KUPATA UZIMA WA MILELE (Mst. 35-36).

(1)      KUTIWA GEREZANI KWA WAAMINIO (Mst. 24)
Katika msitari huu tunasoma kwamba Yohana alikuwa hajatiwa gerezani.  Hata hivyo, hatimaye siku ilifika, akatiwa gerezani.  Sababu ya kutiwa gerezani ilikuwa ni kuikemea dhambi (MATHAYO 14:3-4; MARKO 6:17-18).  Tukihubiri kwamba watu watubu dhambi, na kuacha dhambi, hiyo itakuwa ni sababu ya sisi kutiwa gerezani., hata ikibidi, kuuawa (MATENDO 26:20-21).  Mtu yeyote aliyeokoka, lazima atakuwa ni mtu wa kuikemea dhambi, na kuichukia.  Kwa sababu hii ulimwengu lazima utamchukia (YOHANA 7:7).  Ulimwengu ukituchukia, watu wake, yaani watu wasiookoka, watatutia gerezani.  Siyo lazima kututia gerezani katika uhalisi wake, lakini pia wanaweza kututesa, kutuvurugia amani, kutupiga mijeledi au makofi, kutunyima hiki au kile au kututenga kabisa katika ukoo n.k.  Hii siyo ajabu.  Yesu Kristo alituambia waziwazi kwamba, hakuleta amani kati yetu na mataifa, bali mafarakano (LUKA 12:51-53).  Inatupasa kuwa waaminifu na kuishikilia imani ya wokovu hata ikibidi kufa kwa mateso.  Tukifanya hivyo, taji kubwa inatusubiri mbinguni (UFUNUO 2:9-10).

(2)      MASHINDANO YA WANAFUNZI WA YOHANA (Mst. 25-26)
Wanafunzi wa Yohana walishindana na Myahudi mmoja juu ya utakaso.  Utakaso unaozungumziwa hapa, ni jinsi gani ya kuwa safi mbele za Mungu.  Myahudi huyu, aliamini kwamba mtu anakuwa safi, kwa kuzishika sheria za Musa za kuwawadha na kuondoa unajisi, na kushika mapokeo ya wazee (HESABU 19:13; KUTOKA 30:18-21; MARKO 7:1-5; WAEBRANIA 9:10).  Wanafunzi wa Yohana walishindana naye na kusema ni lazima mtu auendee ubatizo wa Yohana au siyo hawezi kuwa safi.  Ndipo Myahudi huyo akawaambia wanafunzi wa Yohana “Kama ni hiyo, mbona Yesu naye anabatiza na WATU WOTE wanamwendea?  Tuuamini ubatizo upi?”  Wanafunzi wa Yohana waliposikia Yesu naye anabatiza, wakachukizwa sana, wakaona wamwendee Yohana ili amkataze!  Wanafunzi hawa wa Yohana walikuwa bado wachanga.  Hawakujua kwamba Yohana alikuja tu kuitengeneza njia ya Bwana Yesu.  Walipofanya mashindano na mpinzani wao, WALISHINDWA kuisimamia imani.  Tunajifunza hapa kwamba mtu aliyeokoka wakati bado ni mchanga, siyo vizuri kujiingiza katika mashindano na Mashahidi wa Yehova, Wasabato, Wanafunzi wa William Branham wanaosema ni Ubatizo wa Yesu tu siyo Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, au Waislamu wanaosema Mtume Paulo alikosea kusema hivi na vile n.k; katika mihadhara yao.  Ni rahisi kushindwa kuishindania imani kama wanafunzi wa Yohana.  Ili kushindana na watu wa jinsi hii, wanatakiwa wanafunzi wa Yesu waliobobea au kukomaa katika maandiko.

(3)      WIVU WA WATUMISHI WA MUNGU (Mst. 26-27)
Wanafunzi wa Yohana katika hali ya chuki na wivu, walimwendea Yohana na kumwambia “Yeye ULIYEMSHUHUDIA, tazama huyo anabatiza na WATU WOTE wanamwendea”.  Walifikiri ingemfanya Yohana kuchukizwa, na kutafuta jinsi ya kumpinga vikali na kumwita “PEPO” au majina mbalimbali ya kumharibia sifa, ili watu wasimwendee, lakini yeye hakufanya hivyo.  Yohana alijibu “Hawezi mtu kupokea neno lolote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni”.  Ni vigumu mtu anayemhubiri Yesu Kristo katika kweli, kujitwalia mwenyewe tu heshima na kuwavuta wengi kumfuata, ni mpaka awe amepokea kutoka mbinguni (WAEBRANIA 5:4).  Yohana hakuona wivu bali alifurahi kwamba ufalme wa mbinguni unaongezeka.  Ni muhimu kwa sisi watumishi wa Mungu, kujifunza kwa Yohana Mbatizaji aiyekuwa Mtumishi wa Mungu wa kwanza katika Agano Jipya.  Kwa nini tuwe na wivu kwa Mtumishi wa Mungu mwenzetu,tunapoona watu wote wanamwendea?  Ikiwa watu wote wanamwendea Mtumishi huyowa Mungu ina maana karama ziko kwake kwa kipimo kilicho zaidi ya kwetu.  Kuna ubaya gani Mtoa Karama Mungu mwenyewe anapochagua ampe huyu hivi na huyu hivi?  Hata kama anampa karama zaidi yule TULIYEMSHUHUDIA na KUMBATIZA kuna ubaya gani kwa Mungu?  Tunapompiga vita mtumishi wa Mungu mwenzetu ambaye watu wote wanamwendea, eti kwa sababu ni mtu wa juzi juzi tu, tunampiga vita MUNGU aliyempa karama hizo na hatuwezi kufanikiwa.  Je, si halali yake Mungu kutumia karama zake kama apendavyo?  (MATHAYO 20:15).  Tuwe kama Paulo Mtume aliyefurahi kuona wale waliokuwa kinyume chake wakimhubiri Kristo (WAFILIPI 1:15-18).  YADHURU NINI?  Tutamani wote wawe kama tulivyo na kuzidi.  Huo ndiyo Ukristo (HESABU 11:27-29; LUKA 9:49-50).

(4)      YESU KAMA BWANA HARUSI (Mst. 28-29)
ZABURI 45, ni Zaburi inayomtabiri Yesu kama Bwana Arusi.  Siyo ajabu bibi arusi kumfuata kipenzi chake Bwana Arusi.  Kanisa la Mungu, ni bibi arusi wa Kristo.  Ikiwa WOTE WANAMWENDEA Yesu, ni kwa sababu Kristo ni Bwana Arusi na watu hawa ni bibi arusi wake.  Yohana Mbatizaji anajifananisha na rafiki wa Bwana Arusi (BESTMAN).  Rafiki wa Bwana Arusi hufurahia kila mafanikio ya Bwana Arusi.  Humtumikia na kumsaidi katika kila jambo ili afanikiwe.  Mtumishi wa Mungu ni rafiki wa Yesu, Bwana Arusi (YOHANA 15:15-16).  Kazi yetu ni kutumika na kufurahia kuongezeka kwa Ufalme wa Yesu, siyo ufalme wetu!

(5)      YESU KUZIDI SISI KUPUNGUA (Mst. 30)
Yohana Mbatizaji, ni mfano kwetu.  Hatuna budi kufurahi Yesu anapozidi na sisi kupungua.  Ikiwa sisi tutaonekana hatufai, ni duni au dhaifu, lakini kwa jinsi hiyo Yesu akatukuzwa, hakuna kubwa zaidi la kutufurahisha kama hilo.  Tutandike nguo zetu azikanyage na sisi tuwe punda wa kupandwa na Yesu (MARKO 11:7-8).
(6)      YESU KRISTO YU JUU YA YOTE (Mst. 31-33)
Yesu Kristo amepewa mamlaka yote mbinguni na duniani (MATHAYO 28:18).  Nguvu zozote za majini au mapepo, malaika wote na chochote mbinguni na duniani, vyote viko chini ya miguu ya Yesu Kristo (WAEFESO 1:20-23).  Tunapokuwa na Yesu, ni salama salimini.  Maadui watakuja kwetu kwa njia moja na kukimbia mbele yetu kwa njia saba (KUMBUKUMBU 28:7).  Hatuna haja ya kubabaishwa na mapepo au wachawi.  Aliye ndani yetu, Yesu Kristo ni mkuu kuliko aliye katika ulimwengu yaani Shetani.  Huyu hana kitu kwa Yesu (1 YOHANA 4:4; YOHANA 14:30).  Tunaposema “Kwa Jina la Yesu pepo toka”, tunaliitia Jina la Yesu aliye juu ya yote.  Tumepewa jina hili, inatupasa kulitumia kikamilifu katika uvamivi wowote.

(7)      ALAMA KUU YA MTUMISHI WA MUNGU (Mst. 34)
Mtumishi wa Mungu, HUYANENA MANENO YA MUNGU.  Katika kila jambo analofundisha au kuhubiri, husema “KAMA YANENAVYO MAANDIKO“ (1 WAKORINTHO 15:2-4).  Ikiwa Mhubiri, anashindana na tafsiri sahihi ya Neno la Mungu na kuwaambia watu washike sheria za Kanisa au yaliyoandikwa katika Katiba ya Dhehebu, yaliyo mbali na Neno la Mungu; huyu siyo Mtumishi wa Mungu.  Tunapaswa kumpuuza katika lolote alisemalo.  Ni Kiongozi kipofu.  Tuwaache hao (MATHAYO 15:14).

(8)      JINSI YA KUPATA UZIMA WA MILELE (Mst. 35-36)
Kumwamini Yesu, Mwana wa Mungu, na kuyafuata maneno yake, ndiyo njia pekee ya kupata uzima wa milele.  Yesu ndiye Njia, Kweli na Uzima (YOHANA 14:6).  Wengine wote tukiwafuata tunapotea njia, tunaufuata uongo, na kutafuta mauti ya milele.  Maneno ya Yesu ni roho, tena ni uzima (YOHANA 6:63).  Uzima wa milele umo katika Mwana wa Mungu (1 YOHANA 5:11-13).
…………………………………………………………………………………………………………………………………..
Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni?  Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14).  Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).  Kinyonge ni kipi?  Ni yule anayetenda dhambi.  Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge!  Je, wewe ni mtakatifu?  Jibu ni la!  Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13;  YOHANA 14:6).  Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii?  Najua uko tayari.  Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni;  Mungu Baba asante kwa ujumbe huu.  Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi.  Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha.  Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo.  Bwana Yesu niwezeshe.  Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu.  Amen.  Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni.  Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu.  MUNGU AKUBARIKI !!!
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . 

Zipo Baraka nyingi kwa yeyote atakaye “share “ ujumbe huu katika Facebook , Twitter n.k, kwa ndugu, jamaaa na marifiki ili nao wapate nafasi ya kusoma ujumbe huu na kubarikiwa kama wewe ulivyo barikiwa. Kwasababu hii share ujumbe huu kwa kubonyeza neno“ share” lililopo chini ya “somo” hili, kwa kufanya hivyo ujumbe huu utafika kwa watu wengi. Hakika, Baraka za Mungu zitakuwa nawe..


Kwa Neno la Uzima kutoka kwa  Askofu Zachary Kakobe fungua       
Tovuti       : www.bishopzacharykakobe.org
Facebook : www.facebook.com/bishopkakobeministries
Youtube   : www.youtube.com/user/bishopkakobe

Comments

Unknown said…
Kama kuna eidha somo au ushuhuda ama habari yoyote ya kikanisa na nikataka kuituma kwenu nitatumia anuani ipi au nifanyeje?. ushauri na kama aiwezekani bado ni vyema tu nifahamishwe, mmbarikiwe na Bwana @ all
Unknown said…
Somo la WIVI WA WATUMISHI WA MUNGU limenibariki sana , nimejifunza mambo mengi