BAKI KWENYE TUMANI KATIKA BWANA YESU.

Na Mtumishi Peter Mabula.
BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU la uzima.
Inawezekana watu wamekuvunja moyo sana, umekata tamaa na umechoka kuendelea mbele katika tumaini la uzima.
lakini Neno la MUNGU kwako leo linasema mtetezi wako yuko hai na atasimama kukushindia.


Ayubu 19:25 '' Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.''

Inawezekana watu wanasema hutapona.
Inawezekana watu wanasema hutaolewa.
Inawezekana watu wanasema hutashinda kesi.
Inawezekana watu wanasema hutafaulu masomo.
Inawezekana watu wanasema hutabarikiwa.

Neno, nasema tena Neno la MUNGU kwako leo linasema ''Mtetezi wako MUNGU BABA yuko hai na atakutetea tu.''
Jina la YESU liko kazini ili kuwaharibu wanaokuzuia.
Omba tu ndugu na BWANA atakushindia muda sio mrefu.


Yeremia 1:19 '' Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.''

Inawezekana kuna wanaokutisha na kukuzomea.
Wewe simama imara katika maombi na katika tumaini la kutumainia BWANA YESU aliye na uzima wako.
Wanaweza wakashindiana na wewe kwa muda lakini hawatakushinda maana MUNGU atakushindia.
Naongea na mteule aliyeokoka na yuko katika wokovu. Simama imara maana MUNGU aliyeshinda  atashinda tena na leo kwa ajili yako.
Kama kuna mkuu wa giza anakutisha wewe ita damu ya YESU maana hiyo wanaiogopwa wote kuanzia na shetani mwenyewe.
Kama kila siku wanakutamkia laana wewe ita damu ya YESU inayoweza kufuta laana zote haijalishi zilinenwa lini na wapi.
Jina la BWANA ni ngoma imara hivyo ukikimblia leo utakaa salama.

Wakolosai 4:2 ''Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani;'' 

Nampenda BWANA YESU maana jina lake ni msaada wetu.
Nampenda BWANA YESU maana damu yake ya agano ni ulinzi na uzima kwetu.
 Ndugu, Unapoona dalili za ushindi kwenye hitaji lako mshangilie BWANA YESU.
Kumbuka jambo hili kwamba;
 Tangu utotoni mwako umekutana na matatizo mengi sana, lakini yote yalipita. Ndugu hata hili tatizo la sasa litapita tu.
Endelea kumtegemea BWANA kwa maombi na utakatifu.


Zaburi 9:9-10 ''BWANA atakuwa ngome kwake aliyeonewa, Naam, ngome kwa nyakati za shida. Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, Maana Wewe, BWANA hukuwaacha wakutafutao.''

MUNGU anajua ni lini, ni wapi na kwanini.
=MUNGU anajua ni lini utapokea baraka yako.
=MUNGU anajua ni wapi utapokea baraka yako.
=MUNGU anajua ni kwanini utapokea baraka hiyo.

Muhimu kwako ni kuishi maisha matakatifu pamoja na kuendelea kuomba. huku Wokovu wa KRISTO ukiwa ni vazi lako la kudumu.

Mithali 10:22 '' Baraka ya BWANA hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.''
 
 Omba kupitia jina la YESU KRISTO.
omba kwa imani.
omba kwa kutumia Neno la MUNGU.
Maombi yote yawe katika jina la YESU KRISTO.


Wafilipi 3:20-21 '' Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana YESU KRISTO; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.''
 
Dunia inakuambia '' Mimi nitakutenga '',
shetani anakuambia ''Nitakuangamiza'', Mwili
wako unakuambia ''Nitakusaliti'' Lakini Uko
salama kwa sababu MUNGU mwenyewe
anakuambia '' Sitakupungukia kabisa, Wala
sitakuacha kabisa(Waebrania 13:5)


Warumi 8:37-39 ''Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa MUNGU ulio katika KRISTO YESU BWANA wetu.'' 
 
Wakati wengine wanapopitia magumu kidogo wanaacha wokovu, nakuomba wewe songa mbele maana mbeleni kuna baraka zako kubwa sana.
Mbeleni kuna ushindi wako na pia mbeleni kuna uzima wako wa Milele katika BWANA YESU.
Inawezekana kwa sasa unajaribiwa lakini uko wakati wa ushindi wako.
Inawezekana wakati huu unalia lakini hata wakati wa kusheka utafika tu. Baki katika tumaini la BWANA YESU.
Inawezekana waliookoka juzijuzi tu wameolewa na wewe bado, nakuomba usinung'unike wala kulaumu bali songa mbele maana ushindi wako ni wako tu na ushindi huo utakuja kwako.
Inawezekana ndoa za marafiki zako zimejaa furaha na amani lakini ndoa yako ni vita kila siku. Ndugu nakuomba endelea mbele kwa maombi na kumngoja BWANA.
MUNGU ni mwaminifu na wa haki hivyo atakubariki tu.
Akisema atakubariki hakuna ambaye anaweza kuzuia.
Baraka yako ni ya kwako tu ing'ang'anie kwa kuomba na kumngoja BWANA .
Siku ya ushindi iko na itakuja tu kwako.
Kama kwako sasa ni usiku na huoni tumaini nakuomba tu ndugu songa mbele maana asubuhi yako ya baraka itakuja.
Hakuna haja ya kujilinganisha na wengine ambao hawajaribiwi kwa sasa bali songa mbele wewe kama wewe huku ukiishi maisha matakatifu ya Wokovu.

  3 Yohana 3:11 ''Mpenzi, usiuige ubaya, bali uige wema. Yeye atendaye mema ni wa MUNGU, bali yeye atendaye mabaya hakumwona MUNGU.''
 
 Naamini kabisa kuna kitu umejifunza, lakini lengo la kwanza la MUNGU ni wewe uokoke. Kama unaishi maisha ya dhambi ndugu nakuomba tubu na okoka.
Kama hujampokea YESU nakuomba umpokee leo na uanze kuanzia leo kuishi maisha matakatifu ya wokovu.
Kama wewe ni mtu wa kanisani lakini maisha yako yamejaa dhambi nakuomba okoka upya na amua kumpendeza MUNGU kuanzia leo.
Kama wewe umegeuza kanisa kama kichaka chako cha kuficha uovu wako , nakusihi sana umche MUNGU maana kuna ziwa la moto kwa waovu, lakini pia kuna uzima wa milele kwa wateule wa KRISTO wanaoishi maisha matakatifu.
MUNGU wangu akubariki sana na akupe
ufahamu wa kumjua yeye na Neno lake, akupe
ufahamu wa kuliishi kusudi lake jema kwako.
ubarikiwe sana pia kwa kujifunza masomo
yangu.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
0714252292.
mabula1986@gmail.com
Ubarikiwe sana kwa kusoma somo hili.

Comments