VIPINDI SABA VYA MAONGOZI YA MUNGU

Na Askofu Mkuu Zakaria Kakobe


Leo tunajifunza somo muhimu sana kwa kila mtu anayependa kuyafahamu mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Tutaligawa somo letu katika vipengele vitano:-
( 1 ). MUNGU KAMA MFANYA SHERIA
( 2 )  UMUHIMU WA KUTAMBUA MAJIRA AU KUJUA NYAKATI
( 3 )  VIPINDI SABA VYA MAONGOZI YA MUNGU
( 4 )  TOFAUTI YA MAONGOZI KATIKA VIPINDI HIVI SABA
( 5 )  YATUPASAYO KUFANYA KATIKA MAJIRA TULIYONAYO
( 1 ).  MUNGU KAMA MFANYA SHERIA.
      Mungu wetu ndiye mfanya sheria wetu na mwamuzi wetu (ISAYA 33:22). Kwasababu yeye ndiye mfanya sheria, ana haki  kuweka sheria fulani au kuiondoa na kuweka nyingine. Hatupaswi kushindana naye wala kumuuliza  kwa nini anaiondoa sheria hii na kuiweka nyingine. Uamzi wake ni wa mwisho. Yeye ndiye mwamzi wetu. Ole wake ashindanaye naye ( ISAYA 45;9 ; WARUMI  9:19-20). Kazi yetu wanadamu , ni kuitekeleza sheria ile anayotupa.
( 2 ).  UMUHIMU WA KUTAMBUA MAJIRA AU KUJUA NYAKATI
     Sheria anazotupa Mungu wetu hubadilika kulingana na wakati kama apendavyo yeye. Kazi yetu wanadamu kama watekelezaji wa sheria ni kujua nyakati tulizonazo na mambo yapi tunayopaswa kuyatenda katika nyakati tulizonazo ( 1NYAKATI 12:32 ). Serikali ya Tanzania siku za nyuma iliweka sheria kwamba ni mabasi ya UDA tu yanayotakiwa kutoa huduma  za usafiri Dar es salaam. Kwa wakati ule, ilikuwa ni kosa kwa gari lolote kufanya huduma hizo. Sheria hii baadaye ilibadilishwa na kile kilichokuwa si halali kwa wakati ule, sasa ni halali. Hatupaswi kushikiria tu sheria ile ya mwanzo wakati tayari imebadilishwa. Ni kazi ya raia wa Tanzania kujua wakati au majira na kujua ni sheria ipi inayohusiana na wakati wa sasa. Sura za noti zetu pia hubadiilishwa kulingana na wakati. Noti ya sh: 100/= ya mwaka 1966, ilikuwa ina thamani wakati ule lakini sasa mtu aliyenayo, ni kama ameshikilia karatasi tu! Vivyo hivyo wanadamu, tunapaswa kuyatambua majira ya Mungu na sheria zinazotenda kazi katika kila majira. Hatupaswo kuzidiwa maarifa na koikoi, mbayuwayu au korongo ambao ni ndege tu wa angani (YEREMIA 8:7; LUKA 12:54-56).
( 3 ).  VIPINDI SABA VYA MAONGOZI YA MUNGU.
Mungu wetu, mfanya sheria weti ameweka vipindi saba katika maongozi yake, na kila kipindi kina sheria zake zinazotenda kazi. Vipindi  hivi saba, ni hivi vifuatavyo:-
 1.Siku zile zilizokuwa  kabla ya Gharika ( MATHAYO 24:38 )
Kuanzia Uumbaji wa mbingu na Nchi na vyote viijazavyo pamoja na Adamu na Hawa mpaka wakati wa Gharika  kuu wakati wa Nuhu.  
  2. Siku za Wazee wetu au siku za Mababa ( MATENDO 7:8-9; YOHANA 7:22; WAEBRANIA 7:4 ).
 Kuanzia baada ya Gharika  mpaka siku ile wana wa Israeli walipotoka Misri.
  3. Siku za Torati na Manabii au Sheria ya Musa ( MATHAYO 22:40; WAEBRANIA 10:28;  MATENDO 28:23 )..
Kuanzia siku ile wana wa Israeli walipotoka Misri mpaka siku ile Yesu  Kristo  alipokuja  duniani mara ya kwanza  kwa kuzaliwa na Mariamu.
   4. Majira ya Mataifa  au Majira ya Neema au Majira ya Kanisa ( LUKA 21:24; MATENDO 14:26-27; WARUMI 6:14 ).
 Kuanzia siku ile Yesu  alipozaliwa duniani  mpaka siku atakapokuja kulinyakua Kanisa .
   5. Wakati wa Dhiki Kubwa ( MWANZO 24:21 ).
Kuanzia siku ile ya kunyakuliwa kwa Kanisa  mpaka kuja kwa Yesu Kristo mara ya pili duniani.
   6. Utawala wa Yesu Miaka 1,000 Duniani ( UFUNUO 20:4-7 )
Kuanzia  wakati wa kuja kwa Yesu mara ya pili Dunuani mpaka wakati wa Vita vya Gogu na Magogu.
   7. Maskani ya Mungu na Watu wake-Mbingu Mpya na nchi Mpya (UFUNUO 21:1-3).
Kuanzia baada ya Hukumu ya Kiti cha Enzi Kikubwa Cheupe cha Hukumu         ( UFUNUO 20:11 ), itakayofanyika mara baada ya vita ya Gogu na Magogu mpaka milele.
( 4 ).  TOFAUTI YA MAONGOZI KATIKA VIPINDI HIVI SABA.
Sheria ya Mungu juu ya jambo fulani  hubadilika toka majira hadi majira mengine. Kwa mfano angalia juu ya sheria kuhusu:-
( a ). Vyakula
  1.  Siku kabla ya Gharika-Adamu na Hawa-usile matunda ya mti wa kati ya bustani       ( MWANZO 2:16-17 ).
  2. Siku za Wazee wetu-Kuleni vyote ( MWANZO 9:1-4 ).
  3. Siku za Torati na Manabii-Msile vyakula fulani fulani ( WALAWI 11 yote ).
  4. Majira ya Mataifa-Kuleni vyote ( LUKA 10:8; 1 WAKORINTHO 10:25-27 ).
Hata hivyo kula damu kumekatazwa mfululizo ( MWANZO 9:4; WALAWI 17:10; MATENDO 15:28-29 ).
( b ).  Kuchinja sadaka mbele za Mungu kwa ajili ya Toba n.k.
  1. 1.      Siku kabla ya Gharika– MWANZO 4:4
  2. 2.      Siku za Wazee wetu    – MWANZO 8:20-21; 48:1; 31:53-54
  3. 3.      Siku za Torati na Manabii-WALAWI 5:6-13
  4. 4.      Majira ya Mataifa        -YOHANA 1:36; WAEBRANIA  10:1-12
( c ).  Kushika Sabato- Sheria ya kushika sabato, haikuwako kwa wanadamu katika Siku kabla ya Gharika wala Siku za wazee wetu. Ililetwa wakati wa Siku za Torati na Manabii kwa sababu maalumu ( KUMBUKUMBU LA TORATI 5:12-15 ). Baada ya hapo, Mfanya sheria alisema ataikomesha ( HOSEA 2:11). Yesu kama Mfanya sheria aliivunja sababu na hakuitaja katika sheria au amri za Mungu ( MARKO 2:27-28; YOHANA 5:16-18; 9:16; MATHAYO 19:16-19 ).
( d ). Kuoa na kutoa talaka
  1. 1.      Siku kabla ya Gharika-Mume mmoja mke mmoja, walioasi kama Lameki wote waliangamizwa na Gharika ( MWANZO 2:24; 4:19; 7:13 ).
  2. 2.      Siku za Wazee wetu-Mume mmoja mke mmoja. Wengine waliooa wake wengi zaidi ya mmoja Mungu alichukuliana nao ( MWANZO 25;1; 26:34 ).
  3. 3.      Siku za Torati na Manabii-Talaka zinaruhusiwa na Musa kwa ugumu wa mioyo ya watu. Mungu anachukuliana nao,( KUMBUKUMBU LA TORATI 24:1-2; MATHAYO 19:7-8 ).
  4. 4.      Majira ya Mataifa-Mume mmoja mke mmoja, Hakuna Talaka ( LUKA 16:18; 1 WAKORINTHO 7:10-11,39; WARUMI 7:2-3 ).Mungu hachukuliani na yeyote tena ( LUKA 9:41).
  5. 5.      Wakati wa Dhiki Kubwa-Hamu ya kuoa au kufanya uasherati itamalizwa na Dhiki Kubwa ( ISAYA 4:1 ).
  6. 6.      Utawala wa Yesu Kristo Miaka 1,000 Duniani-Watawaliwa wanaoa na kuolewa, watawala hawaoi wala kuolewa  ( ISAYA 65:23 ).
  7. 7.      Mbingu Mpya na Nchi Mpya-Hakuna kuoa wala kuolewa ( MATHAYO 22:30 ).
( e ). Kutawadha kabla ya kuingia ndani ya hema ya kukutania.
  1. 1.      Siku za Torati na Manabii- (KUTOKA 30:17-20; 40:30-32 ).
  2. 2.      Majira ya Mataifa-             ( WAEBRANIA 9:10 )
( 5 ).  YATUPASAYO KUFANYA KATIKA MAJIRA  TULIYO NAYO LEO.
Majira tuliyo nay oleo, ni Majira ya Mataifa au Majira ya Neema. Tukitaka kufahamu la kufanya leo, tunaangalia Yesu amesema nini au Agani Jipya linasema nini kuhusu jambo hilo. Pale ambapo kuna kubatilika kwa amri iliyotangulia, basi tunashika iliyo mpya kwa mfano katika MATHAYO 5:33-37 na YAKOBO 5:12 tunajifunza kwamba sheria ya zamani iliwaambia watu kutimiza viapo vyao, lakini leo, haturuhusiwi kuapa kabisa. Pale ambapo sheria haikubadilika, inabaki ilivyo ( KUTOKA 20:12; WAEFESO 6:2 ). Ndiyo maana inatubidi kulinganisha maandiko ya Agani la Kale na maandiko ya Agano Jipya ili kufahamu yatupasayo kufanya katika majira haya tuliyo nayo.
              JE UNAPENDA KUINGIA MBINGUNI ?
Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni?  Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14).  Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).  Kinyonge ni kipi?  Ni yule anayetenda dhambi.  Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge!  Je, wewe ni mtakatifu?  Jibu ni la!  Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13;  YOHANA 14:6).  Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii?  Najua uko tayari.  Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni;  Mungu Baba asante kwa ujumbe huu.  Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi.  Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha.  Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo.  Bwana Yesu niwezeshe.  Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu.  Amen.  Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni.  Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu.  MUNGU AKUBARIKI !!!
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .      
Zipo Baraka nyingi kwa yeyote atakaye “share “ ujumbe huu katika Facebook, Twitter n.k,  kwa ndugu, jamaaa na marifiki ili nao wapate nafasi ya kusoma ujumbe huu na kubarikiwa kama wewe ulivyo barikiwa. Kwasababu hii share ujumbe huu kwa kubonyeza neno“ share” lililopo chini ya “note” hii, kwa kufanya hivyo ujumbe huu utafika kwa watu wengi. Hakika, Baraka za Mungu zitakuwa nawe.
                                                         UBARIKIWE NA BWANA YESU!!!

Ukitaka Neno la Uzima kutoka kwa  Askofu Zachary Kakobe Fungua       
Tovuti       : www.bishopzacharykakobe.org
Facebook : www.facebook.com/bishopkakobeministries
Youtube   : www.youtube.com/user/bishopkakobe

Comments