UJUMBE WA MUNGU KWA KANISA, KAMA ULIVYOPOKEWA KWA NJIA YA MAONO NA MRS MARIAMARTHA C. KAILEMBO

 

Bwana Asifiwe! Huu ni ujumbe kwa kanisa la Mungu, pia kuna ujumbe maalum kwa waimbaji wa nyimbo za injili. Leo nikiwa nimeamka, Bwana ameujaza wivu wake ndani yangu! Huku akinikumbusha Ezekiel 3:18, 33:8, inayosema,
*_"18 Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo, wala husemi na huyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa roho yake; mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako."_*


Ni maono ya kusikitisha sana, pale nilipopata kibali machoni mwake, ili kunishirikisha siri hii ambayo sikuijua. Nilikuwa kwenye maombi ya masafa marefu, nikiombea mambo yangu na uamsho wa kanisa. Ndipo nikiwa nimepumzika wala (si kwa muda mrefu), mara nikafunikwa na usingizi mzito huku nikijitambua, kuwa huu ni usingizi kutoka kwa Bwana (Mwanzo 2:21). Mara nikaona akitokea mtu wa pekee chumbani kwangu, mwenye mvuto wa ajabu mpole sana!. Alisogea karibu na kitanda changu, na nilimfurahia sana. Si mara ya kwanza kunitembelea mtu huyu, hivyo nilimjua na sikuwa na shaka kuwa ni Bwana! Maana kondoo anaijua sauti ya mchungaji (Yohana 10:4ff). Alinyoosha mkono wake kuuleta kwangu, nami niliunyoosha wangu ili anishike! Ilikuwa tayari nikitoka katika mwili wangu pale kitandani nikiwa katika roho.
Ni vigumu kueleza mambo ya rohoni yafahamike vizuri kimwili (1 Korintho 2:13-14, 15). Lakini nilikuwa nimejaa ufahamu, wa kujua mambo hata bila ya kuambiwa ndivyo nilivyojua! Aliniambia kwa upole, *"Sasa tunaondoka!"*. Malaika tayari walikuwa mahari pale, kwa mwendo wa rohoni ni kufumba na kufumbua, nilikuwa katika eneo jingine silijui hata kidogo. Nikaona Makanisa saba 7, na sikujua nini kinaendelea mpaka hapo. Lakini unajua mimi ni furaha yangu, kuwa na Bwana. Si mara ya kwanza, Kristo Yesu kunichukuwa na kunionyesha mambo makubwa, magumu nisiyoyajua! (Yeremia 33:3).
Lakini kwangu huwa ni wakati wa furaha sana, amani ya ajabu hunifunika hata nasahau shida za dunia. Ni hilo lilinifanya nisitake sana kujua nini kinaendelea pale. Nilijiambia maadamu niko na Bwana, sina shaka!. Nampenda na ninapenda kuwa naye milele. Unajua nini! uwepo wa Bwana ni starehe ya ajabu, usingetamani uondoke kwako!. Nilitazama huku na huku nikaona tu hayo makanisa. Tunapokutana na Bwana wa utukufu, hakuna kuongea ovyo ovyo!. Ijapokuwa mimi ni muongeaji kidogo, lakini maneno hapo hayaruhusiwi. Mara nyingi uso wa Bwana umejaa uzuri wa ajabu, hutatamani kusema kitu, bali uso wake unaachilia tu furaha ndani yako. Natabasamu tu! maongezi ni yale yanayoruhusiwa na Yeye. Kama maswali ya muhimu, kwa Mungu kuna adabu ya kutosha!. Basi nilikuwa kimya, ndipo huyo malaika mmoja aliruhusiwa kunitembeza..mahari pale penye makanisa saba!! Yule malaika alinponishika mkono, tukaelekea kwenye yale makanisa. Mpaka hapo sikuwa nimeambiwa chochote, ila tu akili yangu ilikuwa nyepesi ya kuelewa mambo, nilijua yale ni makanisa bila hata kuambiwa!. 
Tulifika, nakaingia:-

*Kanisa la Kwanza*

Niliona kitu cha ajabu! Niliona watu wako ndani ya kanisa, ni Wakristo wa mwilini sana. Wanafanya ibada lakini hawako rohoni. Mambo yote juu juu tu hawajamaanisha kabisa! Nikashangaa mbona wako hivi? Yule malaika kabla sijamwambia kitu alijua ninachowaza na kuongea moyoni, alinitazama kwa huzuni kisha akaniondoa kwenda kanisa lingine. 


*Kanisa la Pili*

Lilikuwa linawatu wengi sana, lakini nilishangaa kuona kanisa lile walikuwa ni watu wanaojihesabia haki!. Niliwaona wakijivuna sana, kuwa wao ndio wenye haki na safi, hawataki kuchangamana na wengine. Na waliyasema makanisa mengine vibaya! Walikuwa wamejiwekea wigo/fence kuwa wao ndio wako sawa, lakini walikuwa dhaifu kabisa!. Nilishangaa nikasema bora kanisa la kwanza kuliko hili! Yule malaika akanichukua tena tukaenda kanisa jingine.


*Kanisa la Tatu*

Nilikuta wakristo wamekaa mafungu mafungu kanisani! Wengine wameipa madhabahu mgongo. Masengenyo yamejaa, wanasengenyana humo ndani ya kanisa, nami nikakumbuka lile andiko kwamba nyumba ya Baba yangu, itakuwa ya sala. Kulikuwa na bishara zingine kabisa watu wamekaa kwa gredi zao (uwezo), wanawake wamekaa kwa namna hiyo wenye uwezo kwa wenye uwezo, na masikini kwa masikini, (hii ilinisikitisha zaidi), nikasema bora kanisa la kwanza na la pili kuliko la tatu.


*Kanisa la Nne*

Nilipelekwa kanisa jingine, ndipo nilishangaa tena katika ibada, madhabahuni wamesimama watu wasiosafi! Niliwaona waimbaji wanaimba sauti nzuri za kuvutia, na kuwafanya watu wawafurahie. Lakini nilipofunguliwa macho tena nikaona muimbaji yule hodari mwenye umbo la kiume, alikuwa na umbo la ajabu!. Kifua chake kimepinda yaani ni mlemavu, na mikono yake mmoja mrefu mwingine mfupi. Lakini naliona watu wa hilo kanisa hawakuwa wakiona kuwa ni mremavu, bali ni mzima tu, walikuwa vipofu hawaoni! Na hapa ndipo nitasema kidogo tafsiri ya hao waimbaji. Ni waimbaji wa kisasa, waliojaa hisia za dunia hii, watafuta pesa, hawana kiu ya Mungu ndani yao, hawana neno, na ule ulemavu wao ni dhabihu kilema. Bwana alikuja kunitafsiria sana kuhusu hawa waimbaji nilibaki nalia. Akasema waimbaji sasa wanaua muziki wa injili. Unajua hii iko wazi kwamba sasa waimbaji wa injili wanaenda kufanana na waimbaji wa dunia kama wale wa bongofleva n.k. Wanaimba hivyo hivyo, na wanacheza kama watu wa dunia. Bwana alinipa lile andiko lisemalo, *_"23 Niondoleeni kelele za nyimbo zenu; kwa maana sitaki kuzisikia sauti za vinanda vyenu"._* Ilikuwa ngumu sana kwangu, maana nami ni muimbaji..Nilianza kujihoji nakuona uharibifu mkubwa tulioufanya kwa kanisa la Bwana.
Tumeileta dunia kanisani, stahili zote za kidunia ,na kuwaharibu watu wa Mungu. Tunavaa ovyo kama watu wa dunia, wakati imeandikwa, "Msifuatishe namna ya dunia hii (Rumi 12:2)". Bwana aliniambia kuwa, lazima kila kitu kinachofanyika kanisani kiwe tofauti na cha dunia. Ili iwe ushuhuda, hapa ni lpamoja na
kuimba. Leo waimbaji tumehama kwenye msingi wa neno, hatuimbi neno la Mungu ila hisia zetu na tamaa zetu, ili tuwapendeze watu na kujipatia mambo ya mwilini. Ole kwa waimbaji maana mtatoa hesabu mliimba nini?. Mpaka sasa nyimbo za injili zinazidi kuishia gizani kufanana kabisa na zile za dunia video zilizojaa uasi na ukahaba. Mapambo yasiyo na kiasi yametawala, na kuwafanya watazamaji wasisikie hata jumbe zinazoimbwa, bali kuwaka tamaa za mwili . Nilipofunguliwa macho juu ya muziki wa injili, niliumia zaidi kwamba mpaka hapa tulipo mmmh! tunaenda wapi?. Watu wanajifurahisha kwa sauti tu nzuri, pasipo msingi wa imani. Na kanisa la Bwana linafurahia kupokea waimbaji wenye sauti za mvuto huku wakiliacha neno..
Swali: Ukiutazama muziki wa injili unavyoendelea, baada ya miaka kumi utakuwa wapi? Tafakari, ombea waimbaji..ni hatari!


*Kanisa la Tano*

Niliona watu waliofanya ibada mapema asubuhi, na kumaliza haraka, na kuondoka. Walienda kutimiza wajibu tu, kisha wakiondoka huendea maisha yao ya anasa. Na watumishi wao hubaki wakifurahia sadaka zao..


*Kanisa la Sita* 

Lilikuwa limefunikwa na mapokeo..walifanya yale tu waliyopangiwa na dini yao..hawakumpa Roho mtakatifu nafasi..


*Kanisa la Saba*

Lilikuwa kanisa limejaa giza, malumbano, ugomvi kwa viongozi wakigombania vyeo na sadaka. Mpaka hapo nilikuwa nimeumizwa sana, kwa kadri nilivyoendelea kutoka kanisa moja kwenda jingine ndivyo hali ilivyokuwa mbaya?. Ndipo Bwana akaniambia ndivyo hivyo mwanangu. Nimekuja kukuonesha uone, kanisa langu lilivyopoa na linvyozidi kupoa na kurudi mwilini. Yalikuwa maneno yenye huzuni sana. Aliniambia siku zinakuja, mtatamani kububujika na kunena kwa lugha hamtaweza, maana ukame umelifunika kanisa. Tatizo kubwa ni roho ya mazoea inafukuza uwepo wa Mungu katikati yetu. Kuacha maombi, kukataa maonyo yaliyo ndani ya neno la Mungu. Nakutaka kuisikia injili, tunayoitaka sisi wenyewe yaani mafanikio ya mwilini pekee, na kutabiriwa uongo na manabii. Bwana aliniuliza, "Je ni kizazi gani mnakiacha baada yenu?". Akasema nawashangaa watu wangu wanavyokimbizana na maisha ya kisasa(digital) na kuacha msingi. Wazazi wakikristo wanawanunulia watoto wao simu (smartphones), ili wazitumie kwa anasa na kuwastarehesha kwenye sehemu za starehe za kila namna beach nk. Lakini hawawafundishi neno, wala kuomba, hapa nilikumbuka Yeremia 9:26 wawafundishe binti zao kuomboleza. Hata mikesha hawawapeleki ili kuwarithisha nguvu za Mungu, bali wanawarithisha mambo ya dunia. Ni kizazi dhaifu kisicho na nguvu zangu! Baada yenu unaona ni kanisa la namna gani litabaki duniani? Nilielewa kwamba litabaki kanisa lisilo na nguvu za Mungu, ambapo hata sasa hii hali ndio imeshika kasi makanisani. Ibada zimekuwa za mazoea..waabudu halisi wanazidi kuadimika, Yohana 4:23-4. Anawatafuta waabudu halisi wamwabudu katika roho na kweli. Ndugu tubu, badilika, Yesu amekaribia, nimeonyeshwa unyakuo mara mbili wengi wakibaki wakiwemo maaskofu na wachungaji..kwa sababu ya kuipenda dunia. Inatisha sana kuanguka kwenye mkono wa Bwana, wenye hasira!! Badilika kabisa viwango vya kuingia viko juu, usidharau makosa madogo madogo, yatakukwamisha. Nimeona kuzimu ilivyojaa wakristo ambao walipuuzia maonyo. Pia nilipelekwa mbinguni kushuhudia uchache wawanaoingia mbinguni wanapokufa kati ya wakristo elfu Tano (5000) niliona wameingia saba tu (7)wengine wote walipotea. Naomba usipuuze haya, maono mengine nitayaongelea siku nyingine maana ni jumbe ndefu. Asante sana , omba bila kukoma (1Thes 5:17).

NI mimi wenu katika Imani MARIAMARTHA C.KAILEMBO.

Comments