Jinsi ambavyo Roho Mtakatifu anavyotumia kiashiria cha moto wa Mungu, kama njia moja wapo ya kumuongoza mtu.

Na Mwl Christopher Mwakasege
Bwana Yesu Asifiwe!
Wiki iliyopita tulijifunza kwa kuangalia mfano wa 1, jinsi ambavyo Roho Mtakatifu anavyotumia kiashiria cha moto wa Mungu, kama njia moja wapo ya kumuongoza mtu.
Leo tuendelee kujifunza juu ya jambo hili, kwa kuangalia mfano wa 2 ufuatao: “Kijiti kilichowaka moto ili Mungu apate utayari na usikivu wa moyo wa Musa katika kile alichotaka kuzungumza naye wakati ule”.
Musa alikuwa anaendelea na kazi ya kuchunga kundi la kondoo la baba mkwe wake, wakati alipoona: “mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea” (Kutoka 3:2) .
Ukiifatilia habali hii kwa makini utaona ya kuwa Mungu hakujifunua na kusema na Musa, hadi Musa “alipogeuka” kutaka kujua, kwa nini “kijiti….. hakiteketei”, ingawa kilikuwa kinawaka moto!
Na Musa “alipogeuka” na “Bwana alipona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti akasema, Musa! Musa! Akasema, mimi hapa” (Kutoka 3:4)
Mungu alizungumza mambo kadha wa kadha kabla Musa “hajakubali” kuupokea na kuutekeleza wito aliyoitiwa. Utayapata mambo hayo ukisoma (Kutoka 3:4-22) na (Kutoka 4:1-29).
Ninachotaka tujifunze hapa si ile hatua ya Mungu ya kujifunua na kusema na Musa! Ninachotaka tujifunze katika habari hii ni kutaka kujua juu ya sababu iliyomfanya Mungu ajifunue jinsi alivyojifunua – Yaani – ya kutumia moto!
Sababu hiyo tunaipata tunaposoma maneno ambayo Mungu alisema na Musa – mara tu baada ya Musa kuitika alipoitwa jina lake.
Biblia inatueleza maneno ambayo Mungu aliyasema “kutoka katikati ya kijiti” kilichokuwa kinawaka “moto”, lakini bila kuteketea. Mungu alimwambia Musa hili: “Usikaribie hapa; vua viatu vya miguuni mwako; maana mahali hapo unaposiamama ni nchi takatifu” (Kutoka 3:5).
Mungu alikuwa ana maana gani alipomwambia Musa hivi: “vua viatu vyako miguuni mwako…?” Kufuatana na Waefeso 6:15 – “miguu” huwa inabebeshwa jukumu la kuchukua “utayari wa kutumwa” kupeleka habari muhimu mahali inapotakiwa kupelekwa!
Wakati ule Mungu alipokuwa anazungumza na Musa, “miguu” ya Musa ilikuwa imebeba “utayari wa kutumwa” na baba mkwe wake aliyeitwa Yethro - kwenda kuchunga kundi lake la mifugo!
Na inaonekana wazi ya kuwa Mungu aliona ya kuwa “viatu alivyovaa” Musa au “utayari” aliokuwa nao Musa wa kumsikiliza Baba mkwe wake – kwa “wakati ule”, usingempa “usikivu” wa kutosha wa kusikiliza kile ambacho Mungu alitaka kusema naye!
Mungu hakujifunua kwa Musa - wala kumpa maelekezo yaliyohusu wito wake - hadi Musa “alipovua” viatu vyake! Kwa hiyo tunaweza kusema Mungu alijifunua kwa kutumia “moto” kwenye kijiti, “ili apate utayari na usikivu wa moyo wa Musa katika kile alichotaka kuzungumza naye wakati ule”!
Kumbuka : Agano la kale lilifungwa kwa mwili, au kwa mtu kutahiriwa kwa jinsi ya mwili; lakini agano jipya lilifungwa na linafungwa, kwa mtu kutahiriwa moyo wake - kwa jinsi ya rohoni.
Kwa mantiki hii – ina maana katika agano jipya -“moto” wa Roho Mtakatifu - ambao Mungu atatuwekea mioyoni mwetu, wakati anataka mioyo yetu iwe na utayari na usikivu kwake!
Kwa hiyo - wakati mwingine unaposikia “moto” unawaka moyoni mwako, “bila kuzimika”, ujue kuna uwezekano mkubwa kuwa Mungu anatafuta utayari na usikivu wa moyo wako, katika kile anachotaka kukueleza.
“Moto” kwenye “kijiti” uliambatana na kile ambacho Mungu alitaka asikie - lakini baada ya Musa “kugeuka” na “kuitika”. Kwa hiyo - unaposika “ moto” moyoni mwako - mwambie Mungu kwa njia ya maombi ya kuwa “umegeuka” na “uko tayari” kumsikiliza. Naamini Mungu atakusemesha kile alichotaka ukisikie kutoka kwake.

 Mfano wa 3 ni huu: “Moto ndani yako kama ishara ya Roho Mtakatifu, kukuhimiza usiache kufanya kile ambacho amekuingiza ukifanye, hata kama upinzani dhidi yako ni mkubwa ili usikifanye”.
Nabii Yeremia alikutana na hali ya namna hii, wakati wa kipindi alipokutana na upinzani dhidi ya utumishi aliokuwa amepewa na Mungu. Upinzani huo ulimfikisha mahali pa kuona ya kwamba amekuwa “kitu cha kuchekesha mchana kutwa;(Yeremia 20:7).
Nabii Yeremia aliona kama vile “neno la Bwana limefanywa shutumu na dhihaka” kwake “mchana kutwa” (Yeremia 20:8). Na kwa sababu hiyo anasema: “Nami,,,sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake...”(Yeremia 20:9).
Kwa tafsiri nyingine – upinzani dhidi ya utumishi aliopewa na Mungu – ulimfikisha mahali pa kuamua kutokusema tena kwa jina la Mungu,...wala asimtaje Mungu popote tena!
Uamuzi huo haukumfanya Mungu anyamaze, bila kufanya jambo lililomwonyesha nabii Yeremia ya kuwa Mungu hakukubaliana na uamuzi wake ule!
Nabii Yeremia anaeleza yaliyotokea hii: “Nami nikisema sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake; basi ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami siwezi kustahimili, wala siwezi kujizuia”(Yeremia 20:9).
Kwa tafsiri nyingine – nabii Yeremia alitaka tujue ya kuwa alipoamua kuacha kufanya alichotumwa na Mungu, kwa sababu ya upinzani dhidi yake, Mungu aliwasha “moto” ndani yake – ambao aliona kama vile umefungwa ndani ya mifupa yake!
Na ujumbe wa Mungu katika “moto” ule, ulikuwa niwa kumhimiza Yeremia abadili msimamo wake wa kuacha kufanya kazi aliyopewa na Mungu. Na badala yake aamue kuendelea kufanya kazi kama alivyoelekezwa na Mungu, hata katikati ya upinzani dhidi yake!
Ukisoma vizuri mstari huo, utaona ya kuwa Yeremia hakukubali mapema kuufuata ujumbe wa Mungu uliokuja kwake kwa njia ya ishara ya “moto” ndani yake! Ndio maana anasema juu ya moto ule ya kuwa “nami siwezi kustahimili, wala siwezi kujizuia”!
Moto ule ulikuwa “mkubwa” sana “moyoni” mwake, kiasi cha kuusikia ukiwaka na kufukuta kama vile umefungwa ndani ya mifupa yake!
Hali ile ya “Moto” ule - ilimfanya abadili uamuzi wake na akaamua aendelee kuifanya kazi aliyopewa aifanye na Mungu! “Moto” ule haukuja kumpa taarifa kuwa Mungu atamuondolea upinzani mbele yake – bali atampa ushindi dhidi ya upinzani wake!
Nabii Yeremia anakiri kwa kinywa chake, juu ya ujumbe ulioingia moyoni mwake kwa njia ya moto wa Mungu uliowaka ndani yake - ya kuwa “lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana… wataona aibu ya milele, ambayo haitasauliwa kamwe” (Yeremia 20:11).
Kwa hiyo - unapoacha au unaposita kuendelea kuifanya kazi ya Mungu uliyopewa, kwa sababu ya upinzani dhidi yako unaokutana nao; usishangae ukisikia “moto” mkubwa ukiwaka “moyoni” mwako!
“Moto” huo moyoni mwako, ni ishara ya Roho Mtakatifu ya kukupa ujumbe wa Mungu kwako:
i.Ya kuwa usiache kuifanya kazi ya Mungu unayoifanya, hata ikiwa umesongwa na upinzani mkubwa dhidi yako – unaokukatisha tamaa usiendelee kuifanya.
ii.Ya kuwa – Mungu yu pamoja nawe, na atakupigania na kukupa ushindi dhidi ya upinzani uliokuandama!
Ni maombi yangu kwa Mungu kwamba anapokuwekea ishara ya “moto” wake moyoni mwako kwa njia ya Roho Mtakatifu atakupa na ufafanuzi wake, ili ujue “moto” huo una ujumbe gani wa kimaelekezo kwako kutoka kwake!
Mungu awabariki!

Comments