UJUMBE WA KINABII KUHUSU KUNYAKULIWA KWA KANISA-Sehemu ya mwisho.

Na Askofu Mkuu Silyvester Gamanywa.

UTANGULIZI
Nimesoma michango ya majibu ya wasomaji pamoja na maswali maswali mbali mbali yaliyoulizwa. Maswali yote yaliyoulizwa kwenye sehemu ya nne yameulizwa nje ya mada. Ninaheshimu michango yote iliyotolewa kwa sababu kila utu wa mtu ni mawazo yake na ustaarabu kuheshimu mawazo ya mtu. Hata hivyo, maelezo yangu yote yalijikita katika kujibu kile ambacho Mathayo 24 iliandika kuhusu WATEULE kama ni KANISA au ISRAELI. Nilionesha maaelezo ya Yesu mwenyewe jinsi alivyosema kuwa alikuwa anaongea na taifa la Israeli na kwamba kanisa kwa muda huo lilikuwa halijakuwepo. Kwa yeyote asiyekubaliana na ukweli huu hilo ni suala la kimapokeo zaidi lakini si la tafsiri sahihi ya kibiblia.
Hii ni sehemu ya mwisho kuhusu mada hii. Yakiwepo maswali ynayolenga mfululizo wa mada hii tangu mwanzo ambayo msomaji anaona haijaeleweka nitakuwa tayari kujibu kwa kifupi kabla ya kufungua mada mpya. Vinginevyo nimesukumwa kuandika kitabu kinachohusu mada hii na kitakapokamilika msomaji wa ukurusa huu utakuwa wa kwanza kupata habari zake. Kwa sasa napenda kufunga mada hii kwa kuelezeka kwa mukhtasari tu kuhusu habari za DHIKI na mchakato wa mambo yakayojiri siku za mwisho:

TAFSIRI YA DHIKI KINABII

Taabu ya uchungu uliokithiri; mateso makali kupindukia; mazingira magumu yasiyovumilika. Dhiki ni kipindi ambacho ghadhabu ya Mungu itamwagwa juu ya ulimwengu uliomkataa Mungu kwa kipindi kirefu tangu alipomtuma Mwanawe Yesu Kristo kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu. Walimwengu walichagua uongo badala ya kweli na kuzidi katika uovu sugu kwa karne nyingi. Mungu alikuwa mvumulivu kwao kwa muda mrefu na sasa uvumilivu wake utafikia ukomo.
"Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo." (MT. 24:21-22)
"Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile." (DAN.12:1)

KUSUDI LA DHIKI KUU

Kusudi kubwa la kipindi cha dhiki ni kuliandaa taifa l Israeli kumkubali Masihi ambaye walimkataa wakati alipokuja kwao kwa mara ya kwanza. Kama ilivyoandikwa ya kwamba: “Alikuja kwa walio wake lakini hawakumpokea, bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu”.(YH.1:11-12) Kwa Israeli kumkataa Masihi, fursa ya neema ikapelekwa kwa Mataifa mpaka mpaka muda wake utakapokamilika (Rum.11:25-27)

Kipindi cha dhiki kimetafsiriwa kiunabii kuwa ni “wakati wa taabu ya Yakobo (Yer.30:7) kwa sababu ni wakati ambapo Mungu anashughulika na taifa la Israeli. Huu ndio wakati uamsho wa kiroho kwa wayahudi utasambaa kila kona ya dunia. Wengi watamwamini Yesu na kuanza kuandaa kizazi kipya cha Israeli watakaoingia kwenye utawala wa milenia. Mungu atatimiza unabii wa juma moja ili kutimiza kusudi lake kuhusiana na Israeli (Dan.9:24)

Ni wakati wa dhiki hata mataifa wasio wayahudi nao watamwamini Yesu kupitia Injili ya Ufalme itakayohubiriwa na wale wayahudi 144,000. Hawa mataifa watakaookolewa wakati wa dhiki kuu na ambao hawatakufa kwenye dhiki ndio watakajumuika kama kondoo kwenye hukumu ya Kristo kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24.
Kusudi la pili la dhiki ni Mungu kumwaga ghadhabu yake juu ya walimwengu ambao waliikataa Injili wakati wa kipindi cha kanisa la Kristo kabla ya dhiki kuanza. Wengi wakati huu watakuwa wamejisajili chini ya utawala wa Mpingakristo na kushikiri maovu yaliyokithiri na ghadabu ya Mungu atashuka kwa ajili yao ili kupatiliza maasi yatakayokuwa yakiendelea kila mahali duniani kwa wakato huo. (2 Thes.2:11-12) Kusudi la tatu la dhiki ni kufanya hukumu dhidi ya kanisa lililokengeuka ambalo litakuwa likiongozwa na Nabii wa uongo (Ufu.17:6) Ufu.17:15-18

MCHAKATO WA MAMBO KATIKA DHIKI

Baada ya kunyakuliwa kwa Kanisa, na utendaji wa Roho Mtakatifu kutoweka juu ya uso wa dunia hii, ndipo ukengefu wa kiimani na mmomonyoko wa maadili utakithiri kupindukia. Kiwango cha uasi dhidi ya mamlaka zilizoko kitapanda na kupoteza amani ya kijamii na uhuru wa kuabudu Mungu wa kweli utatoweka katika jamii. Uvunjwa wa amri za Mungu katika Biblia utakuwa ndio mtindo wa maisha ya kila siku katika jamii. Wakati huo hakuna tena Injili ya wokovu kwa kuwa aliyekuwa mtetezi wake hayupo tena duniani. (Hivi sasa yuko azuiaye)

Kutokana na mkenguko mkubwa wa kiimani na kimaadili katika dunia nzima, Shetani atatumia fursa hiyo kumtambulisha wakala wake ambaye ni Mpingakristo ambaye atajitokeza kuwa ni mpatanisha na mtatuzi wa matatizo ya kisiasa, kiuchumi na kidini ambayo yatakuwa yanasumbua dunia nzima. Huyu Mpinga Kristo atavuviwa na shetani katika kufanya hata miujiza ya uongo ili kuwadanganya walimwengu ambao waliikataa Injili ya kweli wakati kanisa la kweli la Kristo lilipokuwa bado liko duniani. (2 Thes.2:9-10)

Mojawapo ya miujiza mikubwa atakayofanya huyu Mpingakristo ni kufanikisha zoezi la kusaini mkataba wa Amani kuhusu mgogoro sugu wa Mashariki ya Kati, kati ya Israeli na Waarabu. (Dan.9:27) Mojawapo ya ushawishi wake kwa Israeli ni kukamilisha hitaji la ujenzi wa Hekalu la kiyahudi na wayahudi wataanza kutoa dhabihu za wanyama kama zamani. Na pia atafanikisha zoezi la kuundwa kwa serikali moja ya ulimwengu mzima ambapo mamlaka za mataifa binafsi yatajumuishwa pamoja chini ya utawala wa mfumo wa serikali moja ya dunia.

Wakati huo atatokea mtu mwingine mwenye ushawishi mkubwa katika mambo ya uchumi na dini (Ufu.13:11-17) Kazi ya mnyama huyu kwa jina maarufu la Nabii ya uongo atakuwa mpiga debe wa Mpingani Kristo katika kuhamasisha ulimwengu kumwabudu Mpingakristo sawa na Mungu. Atafanya ushawishi mkubwa kwa njia ya kuweka mfumo mmoja wa uchumi ambapo kila raia duniani atawajibika kujisajili kwenye mfumo huo ilia pate kufanikisha mambo yake ya kiuchumi.

AWAMU YA PILI YA DHIKI

Baada ya kipindi cha miaka mitatu na nusu ndipo awamu ya pili ya dhiki itaanza kwa Mpingakristo kuvunja mkataba wa amani aliofanya Israeli na waarabu. Mkataba huo utavunjwa kwa Mpingakristo kuingia kwenye hekalu na kujitangaza kuwa yeye ndiye Mungu na wayahudi wamwabudu yeye. Hilii ndilo linaitwa “chukizo la uharibifu” (Dan.9:27; 2 Thes.2:3-10) 

Hii awamu ya pili ya dhiki ndiyo inaitwa DHIKI KUU, (Ufu.7:14) na ndiyo inaitwa “wakati wa taabu ya Yakobo (Yer.30:7) Kilele cha dhiki kuu kitafikiwa pale ambapo Mpingakristo ataongoza vita ya kuiangamiza Israeli kuanzia Yerusalemu maarufu kwa jina la VITA YA ARIMAGEDONI. Kabla ya kutimiza mkakati huo ndipo Yesu Kristo mwenyewe ataamua kurudi mara ya pili duniani na majeshi yake ya Mbinguni na kuja kumwangamiza Mpingakristo na majeshi yake na kuwatupa kwenye ziwa la moto (Ufu.19:11-21)
Kazi ya Yesu pia itakuwa ni kumkamata Shetani mwenyewe na kumfunga kwenye shimo la giza kwa kipindi cha miaka 1000 (Ufu.20:1-6); na kisha Yesu kuweka utawala wa milenia, na makao makuu yakiwa jijini Yerusalemu. 

Nachukua fursa hii kuwashukuru wote mliofuatilia mada hii na kujibu kwa njia mbali mbali. Natarajia kwamba tutaendelea kuelimishana kwenye mada mpya zinazokuja mbeleni. Mbarikiwe sana.

Comments