BINTI ATAMJUAJE MUME MWEMA?

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.

Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu.
Karibu kujifunza.
Leo nazungumzia mabinti katika swali ambalo wamewahi kuniuliza sana lakini hata wewe kuna kitu cha kujifunza katika ujumbe huu.
Kwa mabinti ambao hawajafunga ndoa.
Isaya 32:8 '' Bali mwungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana.'' 
Kunahitaji uungwana kutoka kwa binti muungwana ndipo kutafanikisha mambo mema yake yajayo.
Kuna maana mbili za Neno Muungwana.
1.  Muungwana ni mtu mwenye adabu na tabia zinazokubalika kwenye jamii.
2. Muungwana ni mtu asiye mtumwa.
Kwa maana hizo mbili naamini kabisa kwamba binti anatakiwa kuwa muungwana kwanza ndipo atafanikiwa katika mambo ya kiungwana.
Uungwana mzuri unaanza na kumtii MUNGU na Neno lake.
Chanzo cha uungwana wa Mteule wa MUNGU ni kuishi maisha matakatifu ndani ya Wokovu wa YESU KRISTO.
Baaba ya utangulizi mfupi huo sasa naingia katika kiini cha ujumbe wa Leo.

           Utamjuaje mume mwema wako?

1. kwa kufunuliwa baada ya kuomba.
Yeremia 33:3 ''Niite, nami nitakuitikia, nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua.''
Ahadi ya MUNGU ni kwamba ukimwita yaani ukiomba juu ya mambo fulani hakika MUNGU anaweza kukufunulia hata usiyoyajua.
Ukimwomba MUNGU hakika anaweza kufunulia juu ya mume wako.
Tahadhari katika hili ni kwamba shetani hupenda sana kuwafunulia mabinti kabla ili hata MUNGU atakapowafunulia hawataamini maana watakuwa wametendea kazi ufunuo kutoka kwa shetani.
Ndio maana ni rahisi tu kumkuta Binti anakuambia kwamba amewahi kufunuliwa kwa vijana watatu tofauti.
Jambo jingi muhimu kujua katika hili ni kwamba MUNGU hafunulii wateule wake kwa ndoto tu.
MUNGU anaweza akakufunulia kwa njia zifuatazo.
1. Kwa njia ya Neno lake.
2. Kwa njia ya watumishi wake waaminifu kukujulisha.
3. Kwa njia ya mazingira uliyopo.
4. Kwa njia ya Maono
5.  Kwa njia ya ROHO MTAKATIFU kukusemesha live.
6. Kwa njia ya Amani ya KRISTO.
7. Kwa njia ya ndoto.
Hizo ni baadhi tu ya njia ambazo MUNGU anaweza kukufunulia yale uliyokuwa hujajui, ila ni lazima uwe muombaji sana na ndio maana amekuagiza umwite ndipo atakuitikia na kukuonyesha mambo uliyokuwa huyajui.
Binti mmoja alifuatwa na kijana mmoja ili amkubalie wawe wachumba na kisha ifuate ndoa. Katika maombi yule binti alijulishwa kwamba yule kijana ni mchawi hivyo japokuwa moyo ulikuwa umeanza kumpenda kijana yule lakini aliachana naye maana ni heri kutokuolewa kwa muda huo kuliko kuolewa na mchawi.
Lakini ninachotaka kusema kwako binti ni kwamba MUNGU anaweza kusema na wewe kabisa lakini nakuomba usikariri tu kwamba ili MUNGU aseme na wewe ni hadi kwa ndoto tu.
 
2. Kwa kupewa amani kumhusu.
Wakolosai 3:15 '' Na amani ya KRISTO iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani.''
MUNGU anaweza kukujulisha kwa njia ya amani ya KRISTO kuamua moyoni mwako.
Isikilize sana amani ya KRISTO ili ikuamulie ndani yako.
Changamoto ya mabinti wengi ni kutaka amani ya KRISTO iwaamulie wakati hawana huyo KRISTO.
Huwezi kuamuliwa na amani ya KRISTO kama huna YESU KRISTO moyoni mwako baada ya kuokoka.
Amani ya KRISTO ni amani ya KiMUNGU inayotusaidia kuyatambua baadhi ya mambo kwa urahisi sana sana.
 Hata katika kumjua Mume mwema basi amani ya KRISTO inaweza kukuamulia na kwa njia hiyo tu ukampata mume mwema wako Ila ni lazima ujilidhishe kwamba amani hiyo ni kutoka kwa MUNGU maana kuna mabinti wengine husema hawana amani na vijana fulani wanaotaka kuwachumbua kumbe sio kwamba hawana amani bali wanajifanya hawana amani kwa sababu ya kuangalia vigezo ambavyo suio vya kiMUNGU.
Binti anaweza akasema hana amani na kijana fulani kumbe ni kwa sababu kijana huyo hajasoma au hana pesa.
Ndugu kumbuka kwamba masikini wa leo anaweza kuwa ndio tajiri wa kesho na tajiri wa leo akawa ndio masikini wa kesho.
Kama unakosa amani na mtu kwa sababu ya mambo ambayo hayatokani na neno la MUNGU basi hiyo ni amani yako na sio amani ya KRISTO.

3. Awe mcha MUNGU mwemye YESU ndani yake na awe mwenye utii kwa MUNGU.
 Yakobo 4:7 '' Basi mtiini MUNGU. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia.''
Mkristo yeyote jambo la kwanza ambalo anatakiwa kuwa nalo ni kumtii MUNGU katika KRISTO.
Kama kuna mwanaume anataka kukuoa lakini hamtii MUNGU basi huyo hafai kuwa mume wako na huyo wala hajatoka kwa MUNGU.
Kama kijana huyo anataka kutembea na wewe kwa sababu ya tamaa zake basi tambua tamaa hizo ni pando la shetani na pando hilo halitaondoka kwa sababu mtaoana bali pando hilo litaendelea na kwa njia hiyo atatamani na wengine baada ya kukupata wewe.
Kumbuka wasaliti wengi wa ndoa zao ni wale ambao walikuwa wasaliti hata wakati wa uchumba, walikuwa waasherati hata wakati wa uchumba.
Hao hofu ya MUNGU haimo ndani yao na kama hofu ya MUNGU haimo ndani yao basi hata wakiingia katika ndoa haitakuwa kosa kwao kutoka nje ya ndoa zao.
Kama huyo mwanaume hamchi MUNGU na hajaokoka basi hakika huyo hakufai.
Kumbuka kwamba MUNGU hawezi kukuletea mwabudu shetani wewe unayemwabudu katika roho na kweli, hivyo kanuni ya MUNGU ni kwamba wewe binti unayemcha MUNGU Baba katika Wokovu wa KRISTO basi hakika mume mwema wako atatoka katika kundi la watakatifu hata kama sio dhehebu lako.

4. Kwa wewe kumpenda upendo usiotokana na vitu alivyonavyo.
mfano fedha, Elimu, umaarufu, umbo n.k

 1 Kor 16:14 ''Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.''
Moja ya njia ambayo inaweza kukujulisha juu ya mume sahihi ni upendo wako kwake.
Wnaweza kukuijia vijana hata saba lakini upendo wako wa kweli ni lazima utakuwa kwa mmoja tu na sio wote.
Hivyo unaweza ukampenda kijana fulani na huo upendo ni ishara kwamba huyo ni mume mwema wako.
Lakini katika hili lazima uwe na tahadhari kubwa sana sana maana hata shetani anaweza akakuletea upendo na kwa sababu upendo huo unatoka kwa shetani basi hakika huo ni upendo feki.
Kama utampenda kijana anayetaka kukuoa nakuomba jiulize na kujijibu kwa usahihi maswali yafuatayo huko ukilinganisha na kanuni ya Kibiblia.
1. Je umempendea nini?
2 Je upendo wako kwake ni upendo wa kweli au ni upendo unaosababishwa na kutaka tu kuolewa?
3. Je Upendo huo unaambatana na amani ya KRISTO?
4. Je upendo huo una kibali cha ROHO wa MUNGU aliyeko ndani yako?
5. Je unampenda moyo wake na sio vitu vya nje vinavyoonekana?
Ukithibitisha kabisa kwamba unampenda kwa upendo wa kweli basi huyo anakufaa.
Lakini usimpende Mchumba wa wengine na chunguza sana chanzo cha upendo wako kwake.
Lakini tambua pia kwamba MUNGU anaweza kusema na wewe au kukujulisha juu ya mume anayekufaa wewe kwa kukuwekea tu upendo kwake ila ni lazima kwanza awe ni mteule wa KRISTO huyo kijana.

5. Anakupenda kwa upendo wa dhati.
 Warumi 12"9 ''Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema.''
Kama vile ambavyo wewe  MUNGU anaweza akaweka upendo ndani yako juu ya mmoja ya vijana waliokufuata wakitaka kukuoa basi vile vile MUNGU anauwezo wa kuweka upendo ndani ya kijana fulani kwa ajili yako na huyo akawa ndio mume mwema wako.
Usimdharau kila anayekupenda maana hata mume wako anaweza kutokea ndani ya kundi hilo lakini lazima uwe makini pia.
Anayekupenda kwa dhati atakupenda kama ulivyo hata kama kibinadamu unapungukiwa na mambo mengi.
Unaweza ukamweleza madhaifu yako yote hata bila kumficha lakini bado akakupenda tu na madhaifu yako hayo.
Wakati mwingine madhaifu yako yanaweza kuwa ndio kitu cha kuongeza upendo kwako kama upendo huo umetoka kwa MUNGU.
Nimewahi kuoa wabinti wanaokojoa kitandani wakiolewa na ndoa zinakuwa njema tu.
Nimewahi kuona wamama wasiozaa wakiishi kwa furaha tu katika ndoa zao.
Nimewahi kuona wamama wasiojua hata kusoma na kuandika hata neno moja lakini waliolewa na kuishi maisha mazuri sana ya ndoa.
Nimewahi kuoa vilema wakiolewa na kuishi maisha safi ya ndoa.
Nimewahi kuoa mwanamke hajuo hata kupika lakini mume wake alimpenda  sana na ndoa yao ni kielelezo.
Nimewahi kuoa wagonjwa wakiolewa na maisha ya ndoa zao kuwa safi sana.
Ndugu hakikisha huyo kijana ana upendo wa kweli kwako.
Kama ana upendo feki hakika anaweza kukukimbia hata ukifeli mtihani tu au ukishindwa kitu kidogo tu katika familia.
Kama kijana atakuwa hana upendo wa kweli wa Ki MUNGU hakika anaweza kukukimbia wakati wa uchumba tu.
 
6. Kumgundua wakati wa uchumba kwa kuangalia yafuatayo:
A. Upendo wake kwako.
B. Anakataa uzinzi wakati wa uchumba.
C. Ana nia njema ya kufunga ndoa na wewe na Anafanya mipango ili mfunge ndoa. 

D. Anakusikiliza kama mtu wa thamani kwake.
E. Anawaheshimu wazazi wako na ndugu zako na kuwapa heshima stahiki.

 F. Anakushauri mambo mema na yanayompendeza MUNGU.
G. anajiheshimu.

Isaya 32:8 '' Bali mwungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana.''

7. Unamgundua kwamba anaweza kulibeba kusudi la MUNGU huu yako.
1 Kor 15:58 '' Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya BWANA sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika BWANA.''
 
Mwanaume anayekufaa ni lazima alibebe kusudi la MUNGU kwako.
Leo kuna mabinti walikuwa na huduma njema za kumtumikia MUNGU lakini walipoolewa tu waume zao waliwakataza kumtumikia MUNGU.
Hiyo ni hatari sana na ni mbaya sana.
Kama mfano wewe ni mwimbaji basi huyo kijana ni lazima apende pia huduma yako na akusapoti.
Kila mmoja anajua anamtumikia MUNGU kwa nini hivyo ni lazima mume mwema wako anayetoka kwa MUNGU ni lazima aipende huduma yako na kukusapoti.
Ukiona mchumba wako anakukataza kumtumikia MUNGU hakika huyo wala hajatoka kwa MUNGU.
Labda tu amtoka kwenye tamaa zako au kwenye macho yako.
 
MUNGU akubariki na pia Ukipenda kunisapoti kwa sadaka katika huduma yangu karibu sana na pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa BWANA YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la BWANA YESU.
0714252292.
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments