UMEITWA NA MUNGU KUONGOZA NINI?

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU
 Bwana YESU atukuzwe ndugu yangu.
MUNGU akubariki sana kwa nafasi hii ya kujifunza Neno lake.
Kila Mteule wa MUNGU aliyeokolewa na Bwana YESU ni kiongozi.
Uongozi ni nini?
Ni tendo la kutangulia mbele, kusimamia, kulinda na kuelekeza watu njia ya kuiendea ili kuleta mafanikio halisi.
Uongozi ni tendo la kuongoza.
 Kwanini nasema kwamba kila Mteule wa KRISTO ni kiongozi?
Biblia inasema ''Kwa maana ndiye MUNGU atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema. Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa MUNGU wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu, mkishika neno la uzima; nipate sababu ya kuona fahari katika siku ya KRISTO, ya kuwa sikupiga mbio bure wala sikujitaabisha bure.   -Wafilipi 2:13-16''
 Kumbe ni MUNGU atendaye kazi yake ndani yetu sisi  wateule wake.
Kama umeokoka hakika wewe ni kiongozi na unatakiwa kuongoza katika mambo ya ki MUNGU ambayo MUNGU atakupa.
Ninaposema wewe ni kiongozi sina maana ya uongozi wa cheo au uongozi wa kuchaguliwa au kuteule, bali wewe ni kiongozi kwa sababu unafanyia kazi anachokupa ROHO MTAKATIFU ndani yako kwa ajili ya kazi ya MUNGU inayompa MUNGU utukufu kupitia wewe.
Ngoja nikupe mfano hai.
Kanisa fulani kwa miaka 7 walikuwa wakiabudu  kila wiki na kiongozi wa kila kitu ibadani alikuwa ni mchungaji.
Yaani Mchungaji ndio alikuwa anaongoza ibada, anaomba, anaimbisha nyimbo za kusifu na kuabudu, anakaribisha wageni, anafundisha Neno la MUNGU na kufanya kila kitu ibadani, na pia kushuhudia mitaani.
Sio kwamba Mchungaji alipenda hali hiyo bali alijaribu kuwafundisha watu lakini kila mmoja aliogopa au kukwepa.
Baada ya miaka saba Baba mmoja akashuhudiwa injili na yule Mchungaji kisha akaja kanisani hapo na  kuongozwa sala ya toba, akaokoka. Baada tu ya kuokoka yule Baba baada ya kuhudhuria ibada kama mbili hivi aliamua kumfuata Mchungaji na kumweleza kwamba anasikia Msukumo ndani yake wa kuanzisha Kikundi cha Kusifu na kuabudu na kwaya ili kumpunguzia Mchungaji majukumu.
Mchungaji akafurahi sana na kumpa kibali. Yule ndugu akaanzisha kwaya na Kikundi cha kusifu na kuabudu. Baada ya muda kwaya ile ikarekodi na baada ya muda kwaya ile ikawa moja ya kwaya maarufu sana nchini. Kanisani watu wakaongezeka sana na waliokuwepo kabla yake walibaki wakishangaa tu kwamba kwanini hayo hayakufanyika kwa miaka saba na wao walikuwepo, hadi alipokuja huyu ndugu?
Naamini sasa unanielewa.
Sasa wewe unayesoma ujumbe huu umeitwa katika KRISTO kuongoza nini?
Kila kitu kanisani au katika injili kuna mtu alianzisha, huko ni kuongoza.
Ukiona vyombo vya mziki kanisani kwenu ujue kuna mtu mmoja tu ambaye ndiye chanzo, huko ni kuongoza.
Ukiona Mnakalia viti kanisani ujue kuna mtu mmoja alimtii ROHO MTAKATIFU ndio maana mnakalia viti vizuri ibadani.
Ukiona Jengo la kanisa ujue kuna mtu alisikia msukumo, huko ni kuongoza.
Kila Mristo ni kiongozi.
Biblia inakutaka umtumikie MUNGU, Je unamtumikia katika nini?
Una msukumo ndani yako wa kufanya nini katika kazi ya MUNGU?
1 Kor 15:58 '' Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya BWANA sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika BWANA.''
Ngoja niendelee kukupa mifano.
John Wesley alikuwa Mtumishi wa MUNGU kama ulivyo wewe, yeye ndiye aliyeanzisha mikutano ya injili ambayo haikuwepo tangu baada ya nyakati za YESU na Mitume. Ilipita miaka karibia 1800 Bila kuwa na mikutano ya injili na ndugu huyu akaanzisha mikutano ya injili. Alipigwa vita sana sana lakini hadi leo kila mara tunasikia mikutano ya injili katika viwanja au sokoni au popote, lakini wapo walioanzisha.
Wewe umeitwa katika nini?
Kila kitu kina Mwanzilishi, je wewe katika Kanisa lenu umeitwa kuanzisha nini?
Kanisani kwetu mwanzo hakukuwa na mkesha siku za ijumaa, baadae Mtumishi wa MUNGU mmoja akajulisha kwamba lazima tuwe na mkesha wa maombi kila ijumaa ya mwisho ya mwezi. Baadae mtumishi mmoja akajulisha kwamba tuwe na mkesha kila ijumaa, mwanzo ilikuwa vigumu na vita lakini baadae watu wakawa wengi wanaohudhuria mkesha na maombi yakawa ni makali, Ni kazi kubwa sana inayofanyika katika maombi hayo ya mkesha, lakini kuna mwanzishaji.
Je wewe umeitwa kuongoza katika nini?
Hapa sizungumzii kutafuta sifa za uongozi bali ROHO wa MUNGU amekupa msukumo gani wa kufanya katika kazi ya MUNGU?
Siku moja nilikutana na Mtumishi mmoja wa MUNGU hapa Dar es salaam, yeye  akiwaona mateja anawaendea na kuwahubiria, akiwaona hadi analia. Ana mzigo mkubwa sana wa kuwasaidia watu hao, kila siku anawaombea na kuwahubiria.
Wewe umeitwa kuongoza katika nini?
Kuna mtu asipowatembelea wagonjwa mahospitalini hakika atajiona kama hajaokoka.
Kuna watu wameitwa kutegemeza Watumishi wa MUNGU kwa pesa, vyakula au nguo.
Kuna mtu asipokwenda kuwahubiria wafungwa magerezani atajiona kama hajaokoka.
Kuna mtu ameitwa kuanzisha kundi la maombi kanisani kwao.
Kila Mteule wa KRISTO ameitwa katika kazi ya MUNGU.
Ziko kazi za MUNGU maelfu na ni MUNGU anayetenda kazi ndani ya wateule wake.
Lakini pia ni muhimu sana kujua kwamba sio kila mtu ameitwa kuanzisha jambo fulani la ki MUNGU bali wengine wameitwa kuendeleza kazi ya MUNGU ambayo ilikwisha kuanzishwa na wengine.
Kuna watu wameitwa kujenga misingi.
Ipo misingi mingi tu, baadhi ya misingi hiyo ni Maombi, kuwahi ibadani,Utakatifu, Utoaji sahihi, nidhamu, Kuomba katika ROHO MTAKATIFU, Kumtegemea MUNGU n.k
Kuna watu wameitwa kutengeneza palipobomoka.
Mfano inawezekana kabisa kanisani kwenu wamama au vijana wamekalia umbea tu na masengenyo, Kwa sababu hawana kazi ya ki MUNGU ya kufanya wakikutana, lakini MUNGU anaweza akaweka msukumo ndani yako na ukawafanya wamama au vijana mkikutana mnajifunza Neno la MUNGU, Kuomba sana, kutembelea waliorudi nyuma na kushuhudia n.k
Kuna watu wameitwa Kuelekeza njia, hawa ni walimu wa Neno la MUNGU, hata kama huwa hawasimami madhabahuni kuhubiri.
Kuna watu wameitwa kuwa walinzi wa kiroho.
Hawa kazi yao ni kuomba yaani kila mara amefunga anaomba, anaomba usiku, anaonya watu ili wasiende upotevuni n.k
Kuna watu wameitwa kushauri viongozi.
Kuna watu wameitwa kwa kazi ya muda mfupi na kuna watu wameitwa kwa kazi ya muda mrefu, wote ni watumishi wa MUNGU, na MUNGU anaitenda kazi yake ndani yao.
1 Kor 4:1-2 ''Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za MUNGU. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu.''
 Ndugu omba MUNGU ili kujua umeitwa katika nini, ili ikusaidie kutumiza kusudi la MUNGU na kuokokolewa kwako.
Mimi Peter binafsi sitasahau tarehe 2 April ya mwaka mmoja ambapo ROHO MTAKATIFU kwa sauti alisema na mimi kwamba ameniita kuwa Mwalimu wa Neno la MUNGU. Nilimshukuru MUNGU na nikajitambua na kutambua wajibu wangu. Namshukuru MUNGU maana kwa sehemu naendelea vyema, pia  mtandaoni nafundisha Neno la MUNGU kwa njia ya kufanya uinjilisti na somo hili ni la 761 tangu nimeanza Mwishoni mwa mwaka 2012. Maana uinjilisti ni kuwa na injili ya KRISTO kisha injili hiyo uipeleke kwa watu ili wajua wajibu wao kwa MUNGU.
Nina shuhuda nyingi mno zilizotokana na masomo hayo,  siwezi kusema hapa maana nafasi haitoshi ila kwa ufupi sana kwa matukio mawili ni kwamba, watu watatu wamepona ukimwi kwa njia ya kuwaombea baada ya wao kusoma Neno la MUNGU lililoandika, Mtu mmoja alikuwa kiziwi lakini baada ya kusoma somo akaniandikia meseji akisema kwamba yeye  ni kiziwi hivyo akipiga simu nipokee na kuanza kuomba maana nikiongea hatanisikia, nilimuombea na wakati naomba akaanguka chini na mtu aliyekuwa karibu yake akachukua simu na kuanza kuniambia kwamba amedondoka na hata hawajui wafanyeje, nilimwambia amwekee siku sikioni na aishikilie huku nikiendelea kuomba, hakika baada ya muda aliinuka na kuanza kuzungumza akirukaruka huku akishangilia kwamba amepona, niliongea naye kwa simu na nikamweleza kwamba inampasa sasa kutafuta kanisa huko aliko na aokoke. Shuhuda ni nyingi mno mno.
Je wewe umeitwa katika nini?
Umeitwa kuanzisha nini? Au umitwa kuendeleza kazi gani ya MUNGU? Umeitwa kufufua nini katika kazi ya MUNGU?
Ndugu mmoja yeye kila ukitokea mchango wa pesa kwa ajili ya kazi ya MUNGU, Yeye anakuwa wa kwanza kutoa. Sio kwamba yeye ni tajiri sana ila ana moyo wa kutoa na ROHO wa MUNGU humpa msukumo wa ndani ili alitimize kusudi la MUNGU.

Ngoja nikupe mifano kadhaa ya watu wa MUNGU walioitwa kama viongozi ili kuongoza kitu fulani cha ki MUNGU kilichokusudiwa.

1. Adamu na Eva kama viongozi walipewa jukumu la kuzaa na kuongezeka.
Mwanzo 1:27-28 '' MUNGU akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa MUNGU alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba. MUNGU akawabarikia, MUNGU akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.''
 Sasa  tujiulize, ingekuwaje Adamu na Eva  wangezaa mtoto moja tu ambaye ni Kaini kisha baada ya kupata mtoto huyo Eva angefunga uzazi?
Hakika wangukuwa ni viongozi wasiojua wajibu wao.
Kwa kama wangefanya hivyo hakika mimi na wewe tusingekuwepo, maana wanadamu wote walitoka katika Adamu na Eva tu.
Ni watoto watatu tu wa Adamu wanaotajwa kwa majina katka Biblia ambao ni Kaini, Habili na Sethi. Na huyu Sethi alizaliwa miaka 300 baada ya Habili kuuawa na Kaini, hivyo kwa miaka mia tatu hiyo hakika Adamu na Eva walikuwa wameshazaa watoto wengi sana na inawezekana na hata wajukuu walikuwa wamewapata, waliotokana na watoto wao.
Ndio maana MUNGU akawapa kuishi miaka zaidi ya Mia tisa(900) ili watimize kazi yao waliyopewa na MUNGU ya kuzaa na kuongezeka.
Adamu na Eva kama viongozi waliopewa jukumu la kuzaa ili kuongezeka hakika walitimiza wajibu wao, maana walizaa watoto wengi sana wa kiume na wa kike.
Mwanzo 5:4 '' Siku za Adamu baada ya kumzaa Sethi zilikuwa miaka mia nane, akazaa wana, waume na wake.''
 Mfano huo uko kimwili na kiroho, sasa wewe umitwa kuzaa nini katika kazi ya MUNGU?
Kuna watu wameitwa kuzaa kiroho.
Kuna watu wameitwa kuzalisha vitu vua Ki MUNGU  katika kanisa la MUNGU.
Kuna watu wameitwa kupanda makanisa kila mahali, huko ni kuzaa ili kuongezeka.
Kuna watu ni wapandaji wa huduma fulani kanisani, huko ni kuzaa ili kuongezeka.
Kuna watu wameitwa kuhamasisha maombi, kushuhudia,kusifub na kuabudu, hizo ni huduma za kuzaa ili kuongezeka.
Je wewe umeitwa katika Wokovu wa KRISTO ili kufanya nini cha  ki MUNGU?

2. Ibrahimu aliitwa ili kuanzisha taifa ya MUNGU la wacha MUNGU.
Mwanzo 12:1-2 '' BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka;''
 Kazi ya Ibrahimu inaweza kuwa tofauti na kazi ya Adamu na Eva.
Kwa Ibrahimu ili litokee taifa la MUNGU la wacha MUNGU basi alitakiwa kuwa thabiti kiimani. Ndio maana hata leo Ibrahimu ndiye Baba wa Imani na hata Wateule wa KRISTO wote ni Uzao wa Ibrahimu. Ibrahimu hata kama angezaa mtoto mmoja tu yaani Isaka ingetosha kabisa kutengeneza taifa la wacha MUNGU, na ndivyo ilivyokuwa. Adamu angezaa mtoto mmoja angekosea lakini sio Ibrahimu, yeye alikuwa na jukumu lingine na la kiimani ndio maana akapewa mtihani wa imani na kushinda hata akawa baba wa imani kwa wateule wa KRISTO wote.
Wagalatia 3:26-29 '' Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa MUNGU kwa njia ya imani katika KRISTO YESU. Maana ninyi nyote mliobatizwa katika KRISTO mmemvaa KRISTO. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika KRISTO YESU. Na kama ninyi ni wa KRISTO, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.   ''

 3. Yusufu aliitwa ili kulihifadhi taifa la MUNGU.
Mwanzo 45:4-8 '' Yusufu akawaambia ndugu zake, Karibuni kwangu; basi, wakakaribia. Akasema, Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri. Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana MUNGU alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu. Maana miaka hii miwili njaa imekuwa katika nchi, na iko tena miaka mitano isiyo na kulima wala kuvuna. MUNGU alinipeleka mbele yenu kuwahifadhia masazo katika nchi, na kuwaokoa ninyi kwa wokovu mkuu.  Basi si ninyi mlionipeleka huku, ila MUNGU; naye ameniweka kama baba kwa Farao, na bwana katika nyumba yake yote, na mtawala katika nchi yote ya Misri. ''
 Nalipenda Neno hili  la Yusufu ''maana MUNGU alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu.''
Kuna watu leo wameitwa katika KRISTO kwa jukumu  kama la Yusufu.
Wakati mwingine jiulize wewe uliyeajiriwa au uliyejiajiri kwamba jukumu lako ni nini katika Mwili wa KRISTO?
Inawezekana kabisa uliombewa upate kazi nzuri na kupitia kazi hiyo MUNGU anataka uwategemeze watumishi katika injili.
Inawezekana kabisa uko katika idara hiyo ya Serikali ili uhakikishe Kanisa la MUNGU hawaonewi wala kunyanyaswa. Nilikaa mkoa fulani ambako kupata kiwanja cha kujenga Kanisa la kiroho ni mtihani mkubwa sana, kule makanisa kadhaa ambao kwa nguvu za MUNGU walipata viwanja vya kumjengea MUNGU nyumba za ibada lakini hata wao kila mwezi wana kesi za kujibu mahakamani wakisingiziwa kwamba wamejenga makanisa katika maeneo yasiyo sahihi. Wanaojenga bar wanaruhusiwa lakini sio kanisa, hizo ni hila za shetani lakini akiwepo Yusufu katika idara inayohusika na huko haikika hatakubali kwa njia ya rushwa kanisa lionewe. Kumbuka watu wa kanisa hatutoi rushwa  hivyo wanaotumia rushwa wanaweza kusumbua sana kama hakuna hofu ya MUNGU huko.
Haina maana kwamba wewe Yusufu kwenye idara yako uonee watu ambao hawamwabudu MUNGU wa kweli, bali hakikisha huoneo mtu yeyote na hakikisha unawahifadhi kanisa la MUNGU.
Yusufu aliwasaidia hadi wamisri waliokuwa wana imani tofauti na yake lakini hakuwasahau Kanisa la MUNGU aliye hai.
Mimi naamini kama kuna uzushi kwa kanisa la MUNGU au kwa mtumishi wa MUNGU basi akina Yusufu walioko kwenye mamlaka watabaini hila hizo na kumtendea mema mtumishi wa MUNGU anayeonewa. Kumbuka Kanisa lina vita na shetani na shetani anao watu wake kwenye kila eneo ili tu kuwamisha kazi ya MUNGU. Wewe Yusufu kaa kinyume na watumishi wa shetani katika idara yako wanaotaka kuhakikisha Injili ya KRISTO YESU haiendi. Nimesema katika ROHO na najua akina Yusufu wengi sana mmenielewa.
Hifadhi watumishi wa MUNGU kwa mali yako, kwa elimu yako, kwa kazi yako na tambua kwamba mbinguni hutapewa heshima kwa sababu ya kazi yako ya kuajiriwa, ila kama ulifanya kazi ya MUNGU hakika kuna taji mbinguni.
Toa mali yako kupeleka injili, toa vibali vya kuhubiri injili, baini uongo wa shetani na ukatae.
Je umejuwa sasa kwamba umeitwa katika nini?

4. Musa aliitwa kulitoa utumwani taifa la MUNGU.
Kutoka 3:9-10 '' Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri. ''
 Hata wewe unaweza ukaitwa ili kuwatoa watu katika utumwa wa dhambi au utumwa wa kufuata mambo ya dunia.
Jukumu la Musa kiungozi lilikuwa tofauti na Adamu, Nuhu, Ibrahimu au Yusufu, na kwa njia hiyo hiyo jukumu lako kiuongozi linaweza likawa tofauti na jukumu la mtu mwingine.
Inawezekana kabisa familia yako au ukoo wako wako utumwani kwa shetani, ni jukumu lako kuwatoa huko.
Inawezekana kabisa kanisani kwenu watu hawamtaki ROHOB MTAKATIFU na kweli ya MUNGU, Ni jukumu lako kuwatoa katika utumwa huo.
Je umeitwa katika nini?

Wako wengi sana walioitwa na MUNGU, hatuwezi kuwataja wote maana nafasi haitoshi lakini tambua kwamba na wewe uliyempokea YESU KRISTO kama Mwokozi wako hakika umeitwa, msikilize ROHO MTAKATIFU na jifunze Neno la MUNGU ili upate akili ya ki MUNGU ya kukusaidia kutimiza wajibu wako na wito wako.
Yoshua hakuitwa kuwatoa watu Misri lakini aliitwa kuwavusha mto Yordani na kuwalithisha nchi ambayo MUNGU aliwaahidi.
Wewe umitwa katika nini?
Kumbuka kazi ya MUNGU inahitaji watenda kazi maana Bwana YESU anasema hao watenda kazi ni wachache sana, hivyo wanahitaji wengi.
Luka 10:2 '' Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni BWANA wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. ''
Kuna njia nyingi za kutenda kazi ya MUNGU, Sio lazima uwe mhubiri au Mchungaji bali kwa hayo ambayo nimekueleza kwenye somo hili na yale ambayo ROHO MTAKATIFU atakusemesha au kukupa msukumo katika kazi ya MUNGU hakika hapo utakuwa unamtumikia MUNGU.

Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
0714252292.
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments