JE NI KWELI UMESHINDWA KUACHA UZINZI NA UASHERATI?

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
Bwana YESU KRISTO atukuzwe watu wa MUNGU.
Ni siku za Karibuni kuna watu wengi waliniandikia jumbe ili niwasaidie jinsi ya kuachana na dhambi ya uzinzi na uasherati ambayo wanasema wamejaribu kuacha lakini imeshindikana.

Wanne kati yao maelezo yalikuwa hivi, ila kwenye jumbe zao nitaondoa majina yao na sehemu zao nitafuta ili hata wewe usiogope kuwajulisha watumishi wa MUNGU ili wakusaidie.

Mtu wa kwanza:
 Mtumishi Mabula habari za uzima wako. Mimi naitwa ........ Niko mkoani ....... Na ni mama wa watoto zaidi ya watano niliowapata nikiwa katika ndoa yangu. Mimi na mume wangu tulifunga ndoa kanisani japo sio Kanisa la Wokovu, na mume wangu ananijali sana na ni mume Ni mume mwema hakika maana anaisimamia vyema ndoa yake na familia yake. Mtumishi japokuwa mume wangu hana tatizo lolote lakini Mimi hata sielewi ni kwa sababu gani maana nimemsaliti mume wangu tangu mwanzo wa ndoa hadi sasa zaidi ya miaka 18 kwenye ndoa. Hata watoto hawa tulionao anaowapenda sana sijui kama kuna mtoto wake hata mmoja, maana nilikuwa nakutana kimapenzi na wanaume tofauti tofauti kila Mara. Wakati mwingine nimekuwa nafikilia na kulia sana maana hata Mimi sipendi na pia mume wangu ananihudumia vizuri mno. Mtumishi wa MUNGU naomba unitoe katika hili shimo la uharibifu nliloko.
Niko tayari kutubu na kuokoka maana siitaki jehanamu lakini nimejaribu na imekuwa ngumu. Mtumishi please nitoe ndani ya hili shimo. Niambie nikupigie simu lini uniombee


Mtu wa pili: 
Mtumishi kama nilivyokuambia siku ile kwenye simu hakika Mimi nahitaji tu Neema ya MUNGU, ukweli nimeshatembea na watu wengi sana na nimeshatoa mimba hata 10 zinavuka, nakutana na masomo yako nagundua kabisa ni MUNGU ananionya, nimeshatembea hadi na watumishi 4 ambao walihamia kwetu. Nimekuwa siwezi kumkataa mwanaume yeyote, na wengi wanaoniijia ni waume za watu. Natamani kuolewa lakini wanaokuja kwangu ni waume za watu tu na hao naishia kulala nao tu kisha wananiacha. Sijui hata MUNGU kama anaweza nisamehe ila nimelia sana Leo na nasukumwa kukueleza, nisaidie mtumishi vile ROHO wa MUNGU atakufunulia, nimechoka hii hali nataka nimtumikie Bwana YESU.

Mtu wa tatu
Kaka Mabula hongera sana kwa kazi ya MUNGU, hakika unawasaidia wengi sana hata kama huwaoni. Mimi ni mmoja wa wanafunzi wako wa siri, huwa nasoma kila somo ulalopost Facebook na kwenye blog yako ya maisha ya ushindi. Huwa si like wala kukomenti lakini Mimi husoma kila somo lako. Mtumishi Mimi naomba nikuambie siri hii. Mimi Nina virusi na huwa naombewa na kuhudhuria mikutano ya injili na kuna wakati huwa naamini kabisa kwamba nitapona ugonjwa huu lakini kizuizi changu ni uzinzi kaka, nimekuwa siwezi kuacha kushiriki tena na watu tofauti. Naamini kabisa kuendelea na dhambi hii ndio kunanifanya nisipone, lakini nimeshindwa kuacha. Naomba msaada wako na siku nikija Dar es salaam nitaomba kuonana na wewe ili uniombee, msalimie Scholar na nawapenda sana.

Mtuwa nne
Habari zako ndugu Mtumishi Peter Mabula, mimi kwajina naitwa ........... Nimesoma somo lako lililopita na baadhi ya vitu ulivyovisema vinafanana na tatizo ambalo niko nalo. ningeomba unisaidie kwa maombi.
Baada ya mimi kumpokea BWANA YESU niliokoka, lakini palifika kipindi fulani nikaanza kukumbuka mambo niliyokuwa nafanya kabla ya kuokoka, pakiwemo mambo ya uasherati, matukano, kujipenda, na mambo mengine. nikaanza kukumbuka mambo ya uasherati na kutamani wanawake kwa wingi na hata kuyaota, mpaka pakafika kipindi ambapo nikifikilia kichwani naona uzinzi, nikaomba kwa msamaha na ukombozi lakini iliendelea

hata sasa mambo haya yameshakua kichwani mwangu kwa wingi sijui nifanye nini ili niweze kupona.
nakuomba nisaidie maana sitaki kuendeleza haya, na najalibu sana kuachana na kujizuia na mambo haya kwa nguvu sana lakini haiwezekani. najisikia kama kuna vitu ndani yangu ambavyo vinanitumikisha
nakuomba nisaidie nifanye nini ili niweze kuponywa?
nakuomba sana tena sana nisaidie kuniombea na MUNGU akubaliki
Amen.

Hao ni sehemu ndogo sana za watu walioniandikia wakisema wamejaribu kuacha uzinzi na uasherati lakini wameshindwa. Ningekupa shuhuda hata kumi na wote wanadai wameshindwa kuacha.
Ndugu zangu Mimi Peter naamini kabisa kwamba ukiwa na njaa sana na mbele yako kikaletwa chakula kizuri sana lakini ukaambiwa kwamba chakula hicho kina sumu Kali sana, ukila humalizi dakika mbili unakufa, hakika hutakula chakula hicho hata kama una njaa Kali sana. Kama kirahisi tu tena bila kusukumwa na mtu unaweza kuacha kula kile chakula basi kwa uzinzi na uasherati unaweza kuacha pia maana uzinzi na uasherati ni sumu mbaya kuliko sumu zote za kawaida. Uzinzi na uasherati unaweza kujutenga na MUNGU Muumbaji wako milele, uzinzi na uasherati unaweza Kukufanya uwe jehanamu na sio mbinguni, uzinzi na uasherati unaweza kukufanya upate magonjwa na dhambi hiyo ni mlango wa shetani kukuvamia katika kila eneo la maisha yako, hata uchumi unaweza kuyumba, majini kukukaba n.k kwa sababu tu ulifungulia mlango.

Kwa ujumla majibu yangu kulingana na watu walioniuliza au kutaka ushauri ni haya.

Ukitaka ushinde uzinzi na uadherati zingatia haya:

1. Tii Neni la MUNGU na zingatiasana tu neno la MUNGU. Neno linakutaka kuikimbia zinaa.
 
1 Wakorintho 6: 18
" Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake;ila yeye afanyaye ZINAA hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe."


2. Kujitenga na marafiki wabaya, wanaokushawishi kufanya dhambi hiyo.

Zaburi 1:1 "Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki; Wala hakusimama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha."


3. Kuacha kuangalia picha za ngono au video za ngono.
 
1 Wathesalonike 5:22 "jitengeni na ubaya wa kila namna."


4. Muda ambao mawazo ya dhambi yanakujia wewe utumie muda huo kusoma neno la MUNGU.

Waebrania 4:12" Maana Neno la MUNGU li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo."


5. Achana na wote uliokuwa na uhusiano nao na futa hadi namba zao au badilisha line ya simu.
 
Mithali 1:10 "Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, Wewe usikubali."


6. Amua kufanyika kiumbe kipya asiyekumbuka mambo ya zamani wala kuyafuata tena.
 
Isaya 43:18 "Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani."


7. Waza uzuri wa mbinguni ambao hautakiwi kuokosa kwa sababu ya dhambi.

2 Petro 3:13-14 "Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.
Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake."


8. Wafuate watumishi wa kweli wa YESU KRISTO na uwe wazi kwao ili wakuombee ufunguliwe.
 
2 Nyakati 20:20 " ........... mwaminini BWANA, Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa."


9. Usiionee aibu dhambi Bali ikemee na iweke wazi kwa mchungaji wako ili usaidiwe kiroho.

Zaburi 34:14-16 " Uache mabaya ukatende mema, Utafute amani ukaifuatie.
Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao. Uso wa BWANA ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani."


10. Kumbuka ukifa dhambini unaenda jehanamu hivyo kwa akili zako zote na nguvu zako zote Fanya kila njia ya kukwepa uzinzi na uasherati.
 
Waebrania 9:27 " Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu;"


11. Mche MUNGU wakati wote.
 
Waebrania 13:4 "Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi MUNGU atawahukumia adhabu."


12. Nipigie simu nikuombee ili kama kuna kifungo cha Giza au madhabahu ya ki shetani inakushikilia na kukutumikisha itakuachia, ili kama una majini mahaba yanayokumiliki na kukutawala yataondoka kwako. Pia wapo watumishi wa MUNGU wengi sana uwe muwazi mbele yao ili wakuombee na vifungo vya Giza vitakutoka na utakuwa huru. Watumishi wa MUNGU wana msaada kwako mkubwa sana, wafuate watakusaidia.
Yakobo 5:14-16 " Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii."
Watumishi wa MUNGU ni watu wa thamani sana kwako.
Wanaweza kukuombea na nguvu za Giza zikakuacha, wanaweza kukuombea na kukuongoza sala ya toba na jina lako likaandikwa katika kitabu cha uzima.
Watumishi wamepewa jukumu na YESU KRISTO hivyo wasikilize itakusaidia.
Yakobo 5:19-20 "Ndugu zangu, ikiwa mtu wa kwenu amepotelea mbali na kweli, na mtu mwingine akamrejeza; jueni ya kuwa yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu, ataokoa roho na mauti, na kufunika wingi wa dhambi."

  '' Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo ROHO ayaambia makanisa.-Ufunuo 3:22   ''
Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
BWANA YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na BWANA YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee BWANA YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
0714252292(Hadi whatsapp).
0786719090
mabula1986@gmail.com
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments