BINTI USIONYESHE UDHAIFU WAKO KWA KILA MTU MAANA UDHAIFU WAKO UNAWEZA KUKUFANYA UKOSE MCHUMBA AU UACHWE.

Na Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU


 Bwana YESU KRISTO atukuzwe ndugu zangu wote.
Karibu tujifunze Neno  la MUNGU.
Walengwa hapa hasa ni wanawake ambao hawajaolewa lakini wanatamani au kutarajia kuolewa, pia somo kama hili linaweza kumsaidia yeyote hata kama yuko katika ndoa ili apate maarifa zaidi au apate kitu cha kuwasaidia wengine.
Ujumbe unasema Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.
 Katika utumishi wangu kwa KRISTO nimekutana na watu wengi na kuwasiliana na watu wengi, baadhi ya wanaume walilalamika kuwaacha wachumba zao kwa sababu fulani, sababu hizo ni udhaidu wa mabinti hao.
Mtu mmoja akanipigia simu akisema ''Namuacha Binti fulani japokuwa nampenda sana ila kwa sababu ya kupenda kwake pesa sitaweza kuvumilia maana ni hatari sana''
''Mtumishi mimi nilikuwa na mchumba na uchumba wetu ulikaa muda mrefu lakini sitaweza kuendelea naye tena kwa sababu ya ushaifu wake, je ni sawa Mtumishi kufanya hivyo?"
Wapo pia mabinti waliachwa na wachumba zao huku hawajui nini kimetokea, mara nyingi wengi wamesema shetani ameingilia kati, inawezekana ni kweli kabisa lakini wapo mabinti wanakosa wachumba au wanachwa na wachumba kwa sababu tu ya udhaifu wao.
Labda ngoja nianze na kufafanua maana ya neno udhaifu.
Udhaifu ni nini?
Kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili sanifu maana moja wapo kati ya maana mbili ya Neno ''udhaifu'' ni Hali ya kuwa na tabia mbaya.
Sasa Binti anaweza akaonekana mbele za mwanaume fulani anayetaka kumuoa kwamba binti huyo ana hali ya kuwa tabia mbaya.
Tabia hizi mbaya zilizo na maana ya udhaifu kwa macho ya kawaida ni kama sio mambo mabaya na sio dhambi, lakini wengi wameachwa sana kwa sababu ya udhaifu kama huo tu.
Binti anaweza akaachwa na Mchumba wake ambaye alimpata kwa maombi mengi lakini anakuja kuachwa kabla ya ndoa kwa sababu tu ya hali ya tabia mbaya yaani ana udhaifu.
Biblia inakutaka uwe na akili na Ukeshe/udumu katika maombi.
1 Petro 4:7 ''Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala.''.
Kwa kukosa akili wengi sana wamekosa waume na wengine kwa kukosa akili nzuri wameachwa na wachumba zao.

Mimi sikukatazi kuwa na udhaifu lakini wanaume wengi hutumia udhaifu wako kama silaha ya kukunyanyasa au hutumia udhaifu wako ili wewe uonekane takataka.
Mfano mmoja wapo unapoachwa huku ukidhihakiwa kwa sababu ya udhaifu wako ujue huko ni kufanywa uonekane hufai.
Udhaifu wako mwingi utakufanya uingie katika dhambi ya uasherati na kisha kuachwa.
Dhambi ya uasherati haitakiwi kamwe kuhusika na wewe.

1 Kor 6:18 ''Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe. ''

Uasherati unaweza hata kuleta vifungo vibaya vya giza katika maisha yako, hivyo epuka sana kuonekana dhaifu hata watu wautumie udhaifu wako kukuletea vifungo vya giza.


Yeremia 23:10 ''Maana nchi imejaa wazinzi; kwa sababu ya kuapa nchi inaomboleza; malisho ya nyikani yamekauka; mwenendo wao ni mbaya, na nguvu zao si za haki.''


Udhaifu uko mwingi sana lakini ngoja nikuambie baadhi ya makundi ya udhaifu yanayoweza kukufanya binti ukose Mchumba au uachwe na Mchumba.
1. Kupenda fedha.
 Jiulize kijana anakuchumbia au anakuambia tu kwamba anatamani akuchumbie kisha mje mfunge ndoa, wewe siku hiyo hiyo unaanza kuonyesha udhaifu wako wa kupenda pesa, mara unaomba pesa ya saluni, mara unaomba vocha, mara unataka upewe pesa ya nguo mpya, mara huna mafuta hivyo unahitaji pesa, mara unataka pesa ya chpsi n.k. Kijana huyo anaweza kuvumilia na kukupa mahitaji yako kwa mwezi mmoja lakini baadae akipiga hesabu ataanza kujuta na kutafuta mipango ya kukuacha, atajiuliza ''kabla hajafahamiana na mimi alikuwa namuomba nani hela kama hivi'' atajiuliza ''Kuingia kwenye ndoa na mtu kama huyu nitafilisika''.
Mwanaume akijua kwamba udhaifu wako ni kupenda pesa basi kama hana nia nzuri na wewe atakuwa anakupa sana pesa lakini ili akupate kingono, ukinasa katika mtego huo wa kishetani ndio kabisa umekwisha maana kila dhambi huzaa matunda mabaya.
Ndugu, kila mmoja anapenda fedha lakini kupenda fedha kuliko dhambi au kuliko udhaifu ni kule kutokulidhika na hali yako au na ulichonacho.
Biblia inasema '' Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, BWANA ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? -Weabrania 13:5-6'' Tena Biblia inasema 
''Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha;ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi-1Timotheo 6:10'' 
Kupenda fedha kuliko chukizo au kuliko udhaifu ni kule kutamani pesa na kuzihitaji hata kwa njia mbaya, kuwa katika kundi la kwamba bila kuwa na kiwango cha pesa unakuwa sisi wewe tena.
Sasa jiulize ulikuwa na maisha yako na mwanaume huyu alikupenda moyoni kipindi ukiwa katika hali yako tu hiyo lakini baada ya yeye kukuchumbia ndio umehamishia shida zote kwake, huo ni udhaifu mkubwa na wanaume wengi ambao baada ya muda huhesabu gharama hakika kuwaacha wachumba zao wapenda fedha ni jambo la haraka sana , na wanaume wengine akimwacha binti humtangaza na hivyo wanaume wote hapo mtaani, au Kanisani au kwenye mazingira hayo hujua kwamba wewe ni mpenda fedha, sifa hiyo inaweza kukufanya usipate mchumba tena.
Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

2. Kusifiwa.
 Kabla sijaendelea kuweka sawa juu ya udhaifu wa mwanamke katika somo hili,  napenda kukujulisha kwamba kuna baadhi ya udhaifu katika hatua ya uchumba unaweza kukufanya ukaachwa na Mchumba na udhaifu huo huo akiufanya mwanamke ambaye yuko ndani ya ndoa yake unakuwa ni udhaifu wa kuifanya ndoa yake iwe imara zaidi, hivyo jifunze sana kutofautisha maisha ya ndani ya uchumba na maisha ya ndani ya ndoa.
Mimi leo nazungumzia udhaifu wa hatua ya uchumba na baadhi ya udhaifu huo ndani ya ndoa unahitajika sana ili kuipa ndoa afya.
Sasa wakati wa uchumba ikifika hatua vijana wa kiume wakajua kwamba wewe udhaifu wako ni kusifiwa basi atatokea hata wakala wa shetani na kukusifia mara nyingi hadi anakunasa katika dhambi.
Nakuomba sana usiwafanye watu wote wakagundua kwamba udhaifu wako wewe ni kusifiwa, kumbuka baadhi ya wanaume huona ufahari kusimuliana habari za binti fulani hivyo wakigundua kwamba udhaifu wako wewe ni kusifiwa unaweza kujikuta unapata mchumba lakini ana ajenda za siri za kukuharibia maisha.
Udhaifu wako hakikisha haukufanyi kuwa mtu usio haki mbele za MUNGU.
Zaburi 12:8 ''Wasio haki hutembea pande zote, Ufisadi ukitukuka kati ya wanadamu. ''
Usiounyeshe udhaifu huu wakati wa uchumba.
Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

3. Kuongeleshwa kimahaba.
Inaweza ikatokea kijana mmoja akagundua kwamba udhaifu wako wewe ni kuongeleshwa kimahaba. Kuna mabinti akiongeleshwa kimahaba siku hiyo halali maana muda wote atakuwa anawaza jinsi alivyoongeleshwa kimahaba, kama udhaifu wako ni huo hakika unaweza ukaja hata kuangukia kwa wakala wa shetani na kwa njia hiyo udhaifu wako ukakuponza.
Mithali 23:27-28 '' Kwa maana kahaba ni shimo refu; Na malaya ni rima jembamba. Naam, huotea kama mnyang'anyi; Huwaongeza wenye hila katika wanadamu.'
Asije mtu akakuotea kwa maneno yake laini au ya kimahaba na akakunasa kama mwindaje anavyoteka mtego na kunasa mnyama aliyemkusudia.
Udhaifu wako usije ukakufanya kuwa mtu mba na hivyo kuongezeka idadi ya wanadamu wenye hila.
Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

4. Zawadi.
Zawadi ni jambo zuri na sio jambo baya.
Zawadi katika ndoa inaweza kuwa chanzo kizuri cha kuifanya ndoa kuwa na afya njema ndio maana nikakuambia kwamba kuna udhaifu katika uchumba ni mbaya sana lakini udhaifu huo ukifanyika katika ndoa ni udhaifu mzuri na wa kuifanya ndoa iwe njema.
Kama kijana wa kiume atagundua kabisa kwamba wewe udhaifu wako ni zawadi hakika anaweza akatumia zawadi kukupata hata kama hana mpango wa kukuoa.
Mithali 23:3-6 ''3 Usivitamani vyakula vyake vya anasa; Kwa maana ni vyakula vya hila. Usijitaabishe ili kupata utajiri; Acha kuzitegemea akili zako mwenyewe. Je! Utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, Kama tai arukaye mbinguni.  Usile mkate wa mtu mwenye husuda; Wala usivitamani vyakula vyake vya anasa;

Ukipewa zawadi pokea kama una amani lakini hakikisha hugunduliki kwamba wewe ukipewa zawadi unaweza ukatoa hata siri za wazazi wako na ndugu zako, usigundulike kwamba zawadi ndio udhaifu wako yaani ukipewa zawadi tu umepatikana.
Ndugu uwe na akili na usitende dhambi.
 Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

5. Mkiwa naye wawili umempata.
Nimewahi kuwasiliana na mabinti waliokuwa wameachwa na wachumba zao kwa sababu hii mbaya.
Kwanza binti kuruhusu kuwa na kina awa kiume wawili tu mahali fulani pa kificho ni jambo baya sana, binti mwenye akili hawezi kufanya hivyo.
Sasa kijana akishajua kwamba udhaifu wako ni awe na wewe sehemu tu huku ukikuongelesha basi network kwako inakata hakika unaweza kujikuta unahesabu wachumba hata wameshavuka kumi waliokuacha huku wewe unasingizia roho ya kukataliwa kumbe umeujulisha udhaifu wako kwa wanaume na wanaumtumia udhaifu huo kukuharibu na kukuharibia.

Kumbuka Mithali 6:26b ''Na kahaba humwinda mtu anase nafsi yake iliyo ya thamani ''.
Kahaba ni mtu anayefanya mambo ya uasherati.
Kahaba ni malaya.
Malaya ni mwanamke au mwanaume mwenye tabia ya uzinzi.
Kahaba humwinda mtu ili anase nafsi yake iliyo ya thamani, ndugu kataa dhambi hiyo.
Ndugu ukiruhusu kuingia katika uasherati hakika Biblia inasema wewe huna akili hata moja maaya tendo hilo nje na ndoa lina madhara mengi kiroho na kimwili.
Mithali 6:32 '' Mtu aziniye na mwanamke hana akili kabisa; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake.''
Usherati kuhufanya unajisike hivyo tafuta kwa kina kujua maana ya ''Kuwa najisi wa kiroho'' ndipo utagundua kwanini Biblia imesema kila mwanadamu anayefanya dhambi ya uasherati  au uzinzi mwanadamu huyo hana akili hata moja.
 Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya unase kwa watu wabaya na ukose Mchumba au uachwe.

6. Ukiahidiwa hata uongo basi unapatikana.
Kama mtu atagundua kwamba udhaifu wako ni huu basi atakudanganya kila aina ya uongo maana wewe ukidanganywa tu unanasa.
 Neno ''Uongo'' maana yake ni tabia ya kudanganya pia  unaweza kusema kwamba ''uongo'' ni kusema jambo ambalo sio la Kweli.
Uongo una mtoto anayeitwa uzushi.
''Uzushi'' maana yake hali ya kuzua mambo ambayo sio ya kweli.
Uongo ni bidhaa ya shetani inayowatesa watu wengi sana.

Biblia inawakataza wanadamu wote kwamba wasiwe waongo lakini wengi sana ni waongo waongo hivyo kama udhaifu wako wewe ni kuambiwa maneno mazuri hata kama ya uongo hakika udhaifu huo unaweza kukupanza daima.
Biblia inasema 
Waefeso 4:25 ''Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake.''
Kuna makundi mengi ya wanaume wanaokuwa wanataka kuingia katika mahusiano na binti fulani hata kama lugha yao itakuwa kumuoa binti yule, kuna wanaume ni waharibifu tu, kuna mawakala wa shetani, kuna waliojaa vifungo vya giza ndio maana maisha yao ni dhambi tu, kuna walioambukizwa magonjwa mabaya hivyo wanafanya hila kuwanasa watu safi.
Binti narudia kusema kwamba usikubali kuonyesha udhaifu wako wowote kwa mwanaume maana anaweza kuutumia udhaifu huo kukuharibia maisha yako na malengo yako.
 Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

7. Ukisemwa vizuri mbele ya rafiki zako.
Hakuna mtu anayetamani kusemwa vibaya mbele za watu lakini binti hakikisha huonyeshi mbele za watu kwamba ukisemwa vizuri akili zako zinahama hadi unapatikana kwa ajili ya mabaya na machukizo.
Mtu akijua kwamba huo ndio udhaifu wako basi anaweza kukusema vizuri mbele za marafiki zako au watu wako wa karibu lakini kumbe anasema kwa unafiki au kujipendekeza ili tu akufurahishe na kukunasa wewe, ndugu uwe makini sana.
Zaburi 12:2 '' Husemezana yasiyofaa kila mtu na mwenziwe, Wenye midomo ya kujipendekeza; Husemezana kwa mioyo ya unafiki;''
Kumbuka kuna wanaume akimaliza shida zake anawaeleza rafiki zake juu ya udhaifu wako, hivyo mtu anaweza akautumia udhaifu wako kukuharibia maisha na kukufanya uonekane takataka mbele za watu.
 Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

Yako madhaifu mengi sana na hayo yamewafanya baadhi ya wanawake kukosa wachumba au kuachwa.

Baadhi ya madhaifu mengi ni pamoja na haya.
8. Ukimvalia vizuri vile apendavyo unampata.
9. Ukiwafanyia kitu kizuri wazazi wake unampata.
10 Ukimsumbua sumbua tu unampata n.k
 Mwisho kumbuka kwamba udhaifu wako unaweza kukupelekea kufanya  ausherati na Biblia iko wazi sana kwamba hakuna mbingu ya waasherati.

1 Kor 6:9 ''Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa MUNGU? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,''

  Binti usionyeshe udhaifu wako kwa kila mtu maana udhaifu unaweza kukufanya ukose Mchumba au uachwe.

Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.

MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.

Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.

Bwana YESU Amekaribia Kurudi.

Je, Umejiandaaje?

Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na Bwana YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?

Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee Bwana YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.

Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.

Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.

Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.

Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.

Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.

+255714252292(Hadi whatsapp).





Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments