![]() |
| Na Mwl Peter Mabula Mtenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi |
Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu.
Namshukuru MUNGU kwa neema yake kwangu.
Namshukuru MUNGU pia kwa ajili ya ambao walinipigia simu baada ya kusoma sehemu ya kwanza na wengine kuniandikia ujumbe kwamba niendelee kuwaeleza nilifanya nini baada ya kumpokea YESU KRISTO kama Bwana na Mwokozi wangu. Siwezi kusema yote maana ni mengi ila kwa sehemu nitakuambia ili kama kuna mahali unahitaji kutengeneza basi tengeneza kama mimi nilivyofanya au kama ambavyo ROHO wa MUNGU atakufunulia wewe binafsi.
Baada ya kuelezea mambo mawili ya kwanza sasa naendelea, Kumbuka Mambo haya yote yalifanyika nikiwa naishi Unguja Zanzibar wilaya ya Mjini-magharibu
3. Jinsi nilivyojua kuomba.
Wakati mimi naokoka nilikuwa sijui kuomba hata sekunde 30.
Na kama kuna kitu nilikuwa nakichukia sana ni kuombea chakula.
Nilikuwa sijui kuombea chakula na hiyo ilipelekea mimi kwa miaka mingi nikila chakula peke yangu nilikuwa siombei chakula.
Wakati mwingine mbele ya watu nilikuwa nachaguliwa kuombea chakula, kwa sababu nilikuwa nadhalilika kila mara mbele za watu kwa sababu sijui kuombea chakula basi nilianza kuchukia sana kitendo cha kuombea chakula.
Baada ya Kuokoka kwa muda kidogo nilikuwa kila nikiwa ibadani nilikuwa nawaangalia tu watu wanaomba.
Mchungaji akisema kila mtu aombe mimi nilikuwa tu najifanya naomba taratibu tararibu na kumbe nilikuwa siombi chochote maana nilikuwa sijui.
Nilikuwa nawashangaa watu wanaweza kuomba hata saa nzima bila kukoma, wakati mwingine katika mazingira hayo mimi nilikuwa napiga magoti kwenye kiti kama naomba na kumbe nasinzia.
Wimbo wa kuabudu ndio unakuja kuniamsha na Kiongozi wa maombi anasema ''Kila mmoja apige makofi ya furaha maana ameshinda vita ya kiroho'' Lakini mimi japokuwa nilikuwa napiga makofi na kushangilia lakini moyoni nilikuwa najua kabisa sijaomba chochote.
Niliogopa kuwasimulia watu ili wasinicheke kwamba sijui kuomba.
Siku moja jumapili wakati wa ibada Mchungaji alikuwa anaongoza maombi ya kuharibu nguvu za giza, sasa kwa neema ya ajabu na hata sijui kama nilipata ufunuo au ni nini ghafla rohoni nikasikia kama sauti ikisema ''Omba kama Mchungaji wako anavyoomba'' pale pale nilianza kutamka kwa kurudia kila Neno la kimaombi ambalo Mchungaji anataja.
Mfano Mchungaji akisema ''Eee MUNGU Baba ninaomba unipe afya njema mimi Amos Lukanula'' Maana ndilo jina la Mchungaji na Mimi akimaliza kutamka nilitamka ''Eee MUNGU Baba naomba unipe afya njema mimi Peter Mabula''
Mchungaji akisema Eee JEHOVA MUNGU wangu ninaomba uwapige wakuu wa giza wanaofuatilia maisha yangu'' Na mimi nilisema hivyo hivyo.
Siku hiyo ya ibada niliomba na hadi nikajisikia raha na ushindi.
Tangu siku hiyo nilikuwa kila ibada iwe ya mkesha, ibada ya jumatano au ibada ya ijumaa jioni au ibada ya jumapili nilikuwa narudia maombi ya Mchungaji alipokuwa analiongoza Kanisa kuomba, nilikuwa naomba hadi naona ushindi, nilikuwa naomba hadi huku nacheka, ghafla nilijikuta najua kuomba yaani ile hali ya kurudia anachoomba Mchungaji sijui iliishaje maana hata mwezi haukuisha nilishangaa naomba mwenyewe bila kuiga, nilikuwa naweza kuomba hata nusu saa bila kuiga.
Namshukuru MUNGU maana kwa sasa ikiwa ni miaka 18 imepita ninaendelea mbele na Wokovu na ninaweza sasa kuomba hata masaa 4 mfululizo bila kupumzika, nimewahi kuomba hivyo.
◼️Inawezekana na wewe unatamani kujua kuomba, ndugu ziko kanuni nyingi sana na kanuni nyingine nimewahi kukufundisha hapa, mfano somo linalosema jinsi na kuomba maombi ya muda mrefu kwa kutumia maandiko. Mimi nilijua kuomba kwa kufuata maombi ya Mchungaji.
➡️Maombi ni muhimu sana.
◼️Wakristo wanaofanikiwa kiroho na kushinda vita ya kiroho ni waombaji na watoaji, hivyo ndivyo nimejifunza na kuona katika maisha yangu ya Wokovu.
◼️◼️Bwana YESU Mwenyewe anamtaka kila aliyeokoka awe muombaji ''Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa.-Mathayo 7:7-8 ''
Unaweza ukatumia kanuni yangu niliyojifunzia maombi na utashangaa unaweza kuomba hata saa nzima, kuna Mama mmoja alitamani sana kujua kuomba nikamwambia kwamba awe anaamka usiku anafungulia Redio za Praise Power FM au Wapo FM na wakati wa Maombi ambapo wachungaji mbalimbali huwa wanaomba usiku basi na yeye awe anarudia maombi ya watumishi wale huku akilitaja kila hitaji lake, baada ya muda aliniambia kwamba anajua kuomba muda mrefu.
◼️Lakini ukitaka uwe unajua kuomba muda mrefu basi hakikisha kwanza unakuwa ni mtu wa kusoma Biblia na kuielewa.
4. MUNGU alinionya juu ya ubishi na mashindano.
Nakumbuka baada ya kuokoka nilikuwa nasikiliza vijana wa mitaani wanavyosema kuhusu Biblia au maandiko kadhaa ya Biblia.
Na kwa sababu mimi nilianza kuisoma Biblia yote nilijikuta nafahamu kwa sehemu mambo mengi kidogo.
Na Kanisani kwetu siku ya Ibada ya jumatano ni siku ya kujifunza Biblia na maswali yanaruhusiwa, hivyo nilikuwa muuliza maswali maarufu, wakati mwingine tulikuwa tunabishana hadi kupelekea kuvuruga ibada.
Nilikuwa nikiuliza swali huku nina maandiko hata matano ya kujijibu hivyo Mwalimu wa siku hiyo akisema tofauti tu na mimi ninavyotaka basi nilikuwa nampinga kwa maandiko na kama akiwa mbishi basi hata ibada ingevurugika. Japokuwa nilikuwa napenda sana kufahamu mambo mengi lakini nilikuwa kama nalazimisha na mkosoaji sana hata vitu ambavyo sina uhakika.
Siku moja Mwalimu wa siku hiyo katikati ya mahubiri yake alitaja watu wa dhehebu fulani kwamba hawawezi kwenda mbinguni kwa sababu wanakataza watu kumpokea YESU KRISTO kama Bwana na Mwokozi wao, wanakataza watu kuokoka, Mtumishi yule alikuwa sahihi kabisa lakini mimi kwa sababu ya kupenda ubishi na maswali ya mitego nilimwambia kwamba anionyeshe andiko ambalo linasema kwamba watu wa dhehebu hilo hawataenda mbinguni, alinijibu vyema ila hakunionyesha jina la dhehebu hilo kwenye Biblia. Alikuwa kila akifafanua hadi Kanisa zima wanapiga makofi ila akimaliza tu Mimi namwambia Nionyeshe andiko linalotaja jina la dhehebu hilo kwamba watu wale hawawezi kwenda uzima wa milele, tulibishana hadi Ibada ikavurugika.
Nilipotoka pale Yule Mtumishi aliniambia kwamba nimewafanya watu Kanisani hadi wamesahau alichofundisha na wanachokumbuka ni mabishano tu kati ya mimi na yeye, akaniambia kwamba ni heri ningemuuliza swali hilo baada ya ibada ili anisaidie.
Nilitoka pale nikijiona kwamba ni kama nimeshinda mechi ngumu kati yangu na yeye, walikuwepo walionisapoti na kunishangilia na niliona sawa tu. Baada ya kutoka hapo ndipo MUNGU alinionya kwa ufunuo na nikajigundua kwamba nilikuwa mkosaji sana, tangu siku hiyo sikuwa tena mtu wa kuuliza maswali ya mitego. Na ilipita miezi mingi kuna Mtumishi mmoja aliniuliza ''Mbona siku hizi huulizi maswali ili kuichangamsha ibada?'
Sikumjibu maana kwa jinsi ambavyo MUNGU alinionya niliogopa sana.
Sikuwa tena na tabia na kubishana na nilibadilika sana.
◼️Nilisoma maandiko na kukuta Biblia inanitaka kwamba nisiwe mtu wa kujivunia akili.
Warumi 12:16-18 '' Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili. Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote.
Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.''
Nilibadilika mno baada ya hapo. Na maonyo yale yamenisadia sana hata sasa maana hata mimi nimekutana na watu wengi sana na wa kila aina mtandaoni wakitaka wanisaidie kuelewa Biblia, ni watu ambao wana akili kama nilizokuwa nazo mimi zamani za kutaka kujionyesha. Ndio maana hata sasa naweza kuandika somo na kuna Mtumishi akisoma ananipigia simu akisema ''Nimeona somo lako ni zuri ila ngoja nikusaidie'' Mfano kuna Nabii mmoja alinipigia akisema kwamba ''Mtumishi Mabula hongera sana kwa huduma ila kuna kitu unakosea sana, Biblia inasema usiwape mbwa chakula cha watoto, unajua maana yake? Ni kwamba masomo yako usiwe unapost mitandaoni hadi kila mtu anaona na wengine wanatajirika kupitia wewe na wewe uko hivyo hivyo, masomo yako uwe unaandaa na kuwauzia watumishi ili wao wafundishe makanisani kwao, hata mimi nakuomba ukiandaa somo lolote kuhusu mahusiano, uchumba na ndoa naomba uwe unanitumia mimi bila kulifundisha popote na nitakulipa vizuri, unavyoweka mtandaoni kila mtu anasoma hutafaidika lolote''
Nimefupisha alichosema mtu huyo ila alifafanua sana kuhusu andiko linalosema kwamba usiwape mbwa chakula cha watoto. Kwa sababu na mimi nilishawahi kuwa mbishi sana na mtu wa kujihesabia haki sana basi nilimwambia tu ubarikiwe na baada ya hapo kila akiandika ujumbe nikawa simjibu.
Hata leo wapo watumishi wengi huniandikia ujumbe kunikosoa hata pale ambapo hawana andiko. huwa tu nawaambia wanipe andiko katika kile wanachotaka wanakosa na wengine huwa tu nawaambia ubarikiwe.
Wako watu wametawaliwa zaidi na roho chafu za udhehebu, hao ndio wanachojua ni ubishi tu na kujionyesha, mimi nilishapitia huko ndio maana kwa sasa mimi huwa naishia tu kucheka na kusema ubarikiwe.
Sio kwamba mimi huwa siulizwi maswali au sijibu maswali bali naulizwa sana sana na najibu sana sana ila nikigundua kwamba muulizaji ananijaribu au anatafuta heshima mtaani kupitia mimi basi simjibu huyo.
Wako watu ni rahisi tu kujua kwamba ananipima ili aone kama najua, huyo huwa najiepusha naye.
Watu wengine waliniambia kwamba ''wewe ni Mtumishi mzuri sana lakini kama hufundishi nyota na mafuta ya upako hutakuwa na huduma kubwa'', Nilibaki kucheka tu maana hata mimi nilishawahi kuwa na roho ngumu mpaka ya kuvuruga Ibada na kumbe mimi ndio mkosaji.
Kuna watu wanaonipigia simu na kuniandikia jumbe za kunifundisha kinyume kabisa na Biblia, mimi huwa nagundua tu kwamba wale wako katika hali kama ambayo mimi nilikuwa nayo mwaka wa kwanza wa kuokoka kwangu yaani ubishi na mashindano.
◼️Biblia iko wazi sana kwamba haitupasi kuwa watu wa mashindano na manung'uniko yasiyo na maana.
Wafilipi 2:14 ''Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano,''
Andiko hili hapa chini siku moja lilitaka kuniliza maana nilikuwa sijatulia kabisa Ibadani, yaani akili yangu ilikuwa tu inatafuta udhaifu wa Mtumishi katika somo lake ili nimuulize maswali, nilikuwa natafuta tu maswali ya mitego katika somo lake.
Andiko ambalo lilinibadilisha ni hili.
Mhubiri 5:1-2 '' Jitunze mguu wako uendapo nyumbani kwa MUNGU; Maana ni heri kukaribia ili usikie, Kuliko kutoa kafara ya wapumbavu; Ambao hawajui kuwa wafanya mabaya. Usiseme maneno ya ujinga kwa kinywa chako, wala moyo wako usiwe na haraka kunena mbele za MUNGU; kwa maana, MUNGU yuko mbinguni, na wewe upo chini, Kwa hiyo maneno yako na yawe machache.''
◼️Kanisani hakutakiwi kamwe kuwapo na mabishano mabaya, mashindano au kudharauliana kulingana na elimu ya mfundishaji.
Mfano unaweza kujiona wewe form 4 na Mhubiri wa siku hiyo darasa la 7 hivyo ukadhani huyo hawezi kukusaidia chochote na kumbe anayekufundisha ni ROHO MTAKATIFU kupitia yule Mtumishi.
Natamani niseme mengi mno lakini naamini mwenye kuelewa ameelewa.
MUNGU akubariki kwa kujifunza somo hili muhimu pia kitabu changu cha MAOMBI YA KINA kinapatikana, tuwasiliane nitakujulisha jinsi ya kukipata.
Asante kama umelielewa Neno la MUNGU la siku ya leo ila nina neno moja la mwisho kwako leo.
Bwana YESU Amekaribia Kurudi.
Je, Umejiandaaje?
Je, Unaendeleza Dhambi Ili Siku Ile Uachwe Na Bwana YESU? Je, Umeshika Wokovu Na Utakatifu Hata Unyakuliwe Siku Ile Kwa Ajili Ya Kwenda Uzima Wa Milele?
Majibu Sahihi Yako Moyoni Mwako Ila Nakusihi Mpokee Bwana YESU Kama Hujampokea Na Nakusihi Ishi Maisha Matakatifu Ukiwa Ndani Ya Wokovu.
Vya Dunia Tulivikuta Na Tutaviacha.
Ndugu, Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Kuokoka.
Vya Dunia Visikupotezee Muda Wako Hata Ukasahau Wokovu Wa Bwana YESU Kwako.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU.
+255714252292(Whatsapp).
Nakuomba share kwa marafiki zako ujumbe huu.

Comments