HAKIKISHA UNAMKIMBILIA DAKTARI HUYU WA AJABU ILI UPONE.

 

Na Mwl Peter Mabula

Bwana  YESU KRISTO atukuzwe ndugu yangu!.
Karibu tujifunze neno la MUNGU.

"Bwana YESU ndio tabibu wa ajabu."

✓✓Tabibu ni maana nyingine ya Neno Daktari au anayetibu.

◼️Bwana YESU Anaitwa tabibu wa ajabu maana anatibu pale ambapo matabibu wa kibinadamu hawawezi kutibu.

◼️Bwana YESU anatibu kuanzia dhambi hadi magonjwa yote.

Luka 2:17 ‘’ YESU aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi. ‘’

Kuna kila sababu ya kumkimbilia  huyu tabibu wa ajabu ili akuponye dhambi, magonjwa na balaa zote.

Nimekuandalia sababu 7 kwanini tunatakiwa tumkimbilie tabibu wa ajabu ambaye ni YESU KRISTO.

    1. Anaponya magonjwa.

Zaburi 103:3-6 ‘’ Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako ukarejezwa kama tai; BWANA ndiye afanyaye mambo ya haki, Na hukumu kwa wote wanaoonewa.‘’  

Na ili kuonyesha uponyaji wake ulivyo wa ajabu, Biblia inasema ‘’ Naye YESU alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina.   -Mathayo 9:35‘’

◼️YESU alikuwa anaponya magonjwa yote.

Kumbe hakuna ugonjwa wa kumshinda Bwana YESU KRISTO.

Ndugu unaumwa nini?
YESU aliponya wagonjwa wote na hata Leo analonya magonjwa yote.

   2.  Anatibu dhambi hata inafutika.

Mathayo 26:28 ‘’ kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.‘’

◼️Kifo cha YESU KRISTO kilizaa ongoleo la dhambi kwa kila anayeamua kutubu katika yeye.

Na kwa kulithibitisha hilo Biblia inasema

1 Timotheo 1:15 ‘’ Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba KRISTO YESU alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi.‘’

✓✓Tulisafishwa dhambi zetu zote siku tulipompokea Bwana YESU na kutubu kabisa.

✓✓Tulioshwa dhambi zetu zote katika damu yake YESU.

    3.  Anatibu laana hata inakuwa baraka.

Wagalatia 3:13-14 ‘’ KRISTO alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti;  ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika YESU KRISTO, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani.‘’

✓✓Laana haina nguvu tena maana KRISTO ametuweka huru mbali na laana. Na tena Biblia inaongeza kwa kusema Wakilaani BWANA anabariki.

   4.  Anatibu waliokufa kwa kuwafufua.

Yohana 11:17,41-44 ‘’Basi YESU alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne. .....  Basi wakaliondoa lile jiwe. YESE akainua macho yake juu, akasema, BABA, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye YESU akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.‘’

 ✓✓Ni jambo gumu sana mtu aliyekufa kufufuka lakini sio jambo gumu kwa Bwana YESU kumfufua mtu yeyote aliyekufa.

✓✓Biblia inasema Bwana YESU Atatufufua siku ya mwisho lakini pia haimsumbui hata leo kumfufua mtu ampendae, haimsumbui hata leo kufufua ndoa iliyokua imekufa n.k

✓✓Haimsumbui hata leo kufufua uchumi wako uliokuwa umekufa.

✓✓Haimsumbui hata leo  kufufua ushindi wako ambao unadhani hauwezekani.

Mkimbilie Bwana YESU KRISTO aliye tabibu wa ajabu ili afufue jambo lako jema ulitakalo ambalo adui aliliua kwa muda mrefu.

   5.  Anatibu wanyonge na waliodharauliwa duniani hata wanaupata uzima wa milele na kuitwa heri.

Yohana 3:16-18 ‘’ Kwa maana jinsi hii MUNGU aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana MUNGU hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa MUNGU.‘’

✓✓Kupitia kumpokea YESU leo unaweza ukaepukana na mateso ya ziwa la moto ambalo waovu wataingi huko.

Uzima wa milele haupatikani kwa pesa hata waende uzimani matajiri tu.

uzima wa milele haupatikani kwa elimu hata wasomi tu ndio waende uzimani, bali uzima wa milele ni kwa wote hata wasio na kitu kabisa cha kidunia. Wakimpokea YESU tu na kuanza kuishi maisha mataktifu hakika uzima wa milele ni wao.

-Unaweza ukadharaulika leo katika ukoo wako wote  au kijiji kizima wakawa wanakuona wewe ni takataka lakini ukimpokea YESU na kuanza kuishi maisha matakatifu hakika wewe una thamani mbele za MUNGU kuliko matajiri 100 wasio na haja ya kuokoka.

-Dhambi ni ugonjwa mbaya sana lakini ukiokoka hakika unapona kutoka kwenye madhara ya dhambi na dhara kubwa kuliko yote ambayo utayaeupuka baada ya kuokoka ni ziwa la moto.

    6. Anatibu kukataliwa na kuwa kupendwa

Mwanzo 37:28 ‘’ Wakapita wafanya biashara Wamidiani; basi wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika, wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri. ‘’ 

Yusufu aliuzwa na ndugu zake.
Wanadamu walimpangia Yusufu kuwa mtumwa na mfuaji wa nguo za matajiri tu.
Lakini yuko BWANA wa mabwana na ni MUNGU wa miungu ambaye anaweza kugeuza mateso yote na kuja furaha kuu.

Wanadamu Walijua hakuna tumaini tena kwa Yusufu la kufikia baraka za MUNGU lakini BWANA  akaondoa kukataliwa kwa Yusufu na kuwa kupendwa.

Mwanzo 45:4-5 ‘’ Yusufu akawaambia ndugu zake, Karibuni kwangu; basi, wakakaribia. Akasema, Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri. Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana MUNGU alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu.‘’

-Ndugu, unakwama wapi?

-Unalia nini wakati Tabibu wa ajabu yuko leo ili akusaidie?

Nakuomba leo tena sasa mkimbilie Bwana YESU KRISTO aliye tabibu wa ajabu sana.

Madaktari wa kidunia wanaweza kutibu lakini Bwana YESU KRISTO yeye hatibu bali anaponya.
Mimi Peter Mabula Nimewahi kushuhudia mgonjwa wa Ukimwi akipona.
Nimewahi kushuhudia mgonjwa wa kifua kikuu akipona.
Nimewahi kushuhudia viziwi wakisikia na vilema wakiona.
Nimewahi kuona wiwete wakitembea na nimewahi kuona kwa macho yangu wenye uvimbe mbaya wakipona na kumshangilia Bwana YESU KRISTO.

Ninaposema mkimbilie tabibu wa ajabu ninakuwa najua ninachoongea maana Kwake yote yanawezekana, utakatifu na imani tu ndivyo mafuta ya kujipaka ili ungae ukiwa na uzima wako katika KRISTO YESU, MUNGU mwenye nguvu na njia pekee ya uzima wa sasa na uzima wa milele.

   7.  Anatibu uteka na kuwa ushindi mkuu.

Ayubu 42:10-13 ‘’ Kisha BWANA akaugeuza uteka wa Ayubu, hapo alipowaombea rafiki zake; BWANA naye akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza. Ndipo wakamwendea nduguze wote, waume kwa wake, nao wote waliojuana naye hapo zamani, wakala chakula pamoja naye katika nyumba yake; ........... ... Basi hivyo BWANA akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng'ombe elfu, na punda wake elfu. Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu.‘’

-Inawezekana kabisa umeteseka kwa miaka mingi juu ya jambo fulani, lakini habari njema ni kwamba YESU KRISTO anaponya na anaweza  kukuweka huru mbali na uonevu wote.

-Inawezekana unalia kila siku kwa sababu ya ndoa yako. lakini habari njema ni kwamba kwenda kwenye maombezi kutaiponya ndoa yako na hata kama una miaka 7 hujaambiwa ''i love you'' lakini kwa BWANA kukufungua wewe na ndoa yako hakika furaha ya ndoa yako itarejea na utamshangilia MUNGU kila iitwapo leo.

-Inawezekana hadi umefikia hatua ya kusema nasubiri kufa tu, lakini napenda kukuambia kwamba wewe hujafikia mateso ya Ayubu wala hata robo tu ya mateso ya Ayubu hujafikia lakini Ayubu alipona na kubarikiwa mara saba zaidi. MUNGU wa Ayubu hakika atakuponya baada ya wewe kuchukua hatua ya kuokoka na kuombea na kuanza kuishi maisha  mataktifu katika KRISTO.

-Inawezekana kabisa umekata tamaa hadi unawaza kwamba ''MUNGU ana upendeleo'' lakini taarifa ya kimbingu kupitia Biblia inasema ''Hakika natambua ya kuwa MUNGU hana upendeleo;-Matendo 10:34''

Bwana YESU ni mwema sana na atatenda mema kwako kama tu utaamua kumpokea na kuanza kuishi maisha matakatifu huku ukihudhuria maombezi Kanisani au kwenye mikutano ya injili au kwenye semina za Neno la MUNGU.

MUNGU akubariki sana wewe uliyesoma ujumbe huu mwanzo hadi mwisho, huu ni ujumbe wenye nguvu sana na nakuomba ukusaidie kufungua macho yako ya ndani ili ukajue msaada wako pekee kwamba ni Bwana YESU KRISTO tu.

Naamini kabisa kuna kitu umejifunza, lakini lengo la kwanza la MUNGU ni wewe uokoke. Kama unaishi maisha ya dhambi ndugu nakuomba tubu na okoka.

Kama hujampokea YESU nakuomba umpokee leo na uanze kuanzia leo kuishi maisha matakatifu ya wokovu.

Kama wewe ni mtu wa kanisani lakini maisha yako yamejaa dhambi nakuomba okoka upya na amua kumpendeza MUNGU kuanzia leo.

Kama wewe umegeuza kanisa kama kichako chako cha kuficha uovu wako , nakusihi sana umche MUNGU maana kuna ziwa la moto kwa waovu, lakini pia kuna uzima wa milele kwa wateule wa KRISTO wanaoishi maisha matakatifu.

MUNGU wangu akubariki sana na akupe
ufahamu wa kumjua yeye na Neno lake, akupe
ufahamu wa kuliishi kusudi lake jema kwako.
ubarikiwe sana pia kwa kujifunza masomo yangu.
By  Peter  Mabula.
+255714252292.
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments