![]() |
| Peter na Jemimah Mabula Watenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi |
Bwana YESU KRISTO Mwokozi atukuzwe rafiki.
Karibu Tujifunze Neno la MUNGU.
◾Daudi siku Moja aliona aibu kwa ajili ya Nyumba ya MUNGU.
2 Samweli 7:2 "mfalme akamwambia Nathani, nabii, Angalia sasa, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, bali sanduku la MUNGU linakaa ndani ya mapazia."
➡️Daudi aligundua yeye anakaa katika nyumba nzuri na imara lakini Sanduku la Agano linakataa katika nyumba ya mapazia tu ndipo wazo la Daudi kujenga Nyumba ya MUNGU likaanza moyoni mwake.
➡️Daudi kwa sababu alikuwa na ROHO wa MUNGU aliona sio sawa kabisa yeye kuwa na Nyumba nzuri Lakini Nyumba ya MUNGU haieleweki.
➡️Leo tuna baadhi ya Wakristo hawana wivu na kazi ya MUNGU, Mtu anaweza kuwa na majumba hata 10 lakini hajawahi kununua hata bati 50 tu kwa ajili ya Kanisa.
➡️Mtu mmoja Maarufu wakati anafunga Ndoa hakutaka rafiki zake ambao nao ni watu Maarufu, hakutaka waje kwenye Ibada ya Ndoa Kanisani kwao, alitaka tu waje Ukumbuni usiku.
Kwanini alifanya hivyo?
Yeye anaishi Maisha ya kitajiri, ana nyumba na gari lakini Kanisani kwao ni jengo dogo la mabati yaliyochakaa sana maana ni kama yalitolewa kama msaada baada ya Mtu mmoja kuamua kubadilisha bati za nyumba yake ambazo zilikaa muda mrefu sana hivyo akawagawia Kanisa, Sasa hapo ndio Kanisani kwa Mtu maarufu ambaye Kila Mtu nchini kwake anamfahamu.
Yaani Mtu huyu hakuwa na namna tu nadhani akilini mwake angetamani atafute Kanisa kubwa zuri ndio huko afungie Ndoa ila ikashindikana.
Jambo la kujiuliza hata kama ni huyo tu Mtu mmoja angekuwa na wivu wa kazi ya MUNGU angeweza kujenga Kanisa zuri peke yake, lakini tatizo hajawahi kuona wivu kwa ajili ya Nyumba ya MUNGU.
◼️Ndugu yangu, kama kweli Mimi na Wewe ni Wakristo tuliookolewa na Bwana YESU KRISTO basi ni vizuri sana tukawa na wivu wa kazi ya MUNGU, ni vizuri sana tukawa tunaweza kuona haya kwa ajili ya Nyumba ya MUNGU ili nayo iwe vizuri.
1 Timotheo 3:15" Lakini nikikawia, upate kujua jinsi iwapasavyo watu kuenenda katika nyumba ya MUNGU, iliyo kanisa la MUNGU aliye hai, nguzo na msingi wa kweli."
➡️Ndugu usiwe kama watu wa wakati wa Nabii Hagai ambao hadi Ufunuo wa MUNGU ulipofika ndipo wakakumbuka kuijenga nyumba ya MUNGU.
Hagai 1:2-5 " BWANA wa majeshi asema hivi, ya kwamba, Watu hawa husema, Huu sio wakati utupasao kuja, huu sio wakati wa kujenga nyumba ya BWANA. Ndipo neno la BWANA lilikuja kwa kinywa cha nabii Hagai, kusema, Je! Huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika? Basi sasa, BWANA wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu."
➡️Kuna watu hadi MUNGU awaadhibu ndipo wataikumbuka nyumba ya MUNGU.
Hagai 1:8-11 " Pandeni milimani, mkalete miti, mkaijenge nyumba; nami nitaifurahia, nami nitatukuzwa, asema BWANA. Mlitazamia vingi, kumbe vikatokea vichache; tena mlipovileta nyumbani nikavipeperusha. Ni kwa sababu gani? Asema BWANA wa majeshi. Ni kwa sababu ya nyumba yangu inayokaa hali ya kuharibika, wakati ambapo ninyi mnakimbilia kila mtu nyumbani kwake. Basi, kwa ajili yenu mbingu zimezuiliwa zisitoe umande, nayo nchi imezuiliwa isitoe matunda yake. Nami nikaita wakati wa joto uje juu ya nchi, na juu ya milima, na juu ya nafaka, na juu ya divai mpya, na juu ya mafuta, na juu ya kila kitu itoacho nchi, na juu ya wanadamu, na juu ya wanyama, na juu ya kazi zote za mikono."
➡️Ndugu, hakuna jengo la Kanisa limewahi kujijenga Bali lilijengwa kwa gharama za watu Wenye Moyo wa kumpenda Bwana YESU KRISTO, jitahidi na Wewe katika Maisha Yako uwe na Moyo wa kumpenda MUNGU na kuithamini nyumba yake.
➡️Kama nyumba Yako Wewe Ina vioo unaweza kuhakikisha na Kanisa Lina vioo.
◼️Hata Injili Kuna wakati inatakiwa ipelekwe kwa pesa zako na hilo ni kusudi la MUNGU Kabisa naye atakubariki.
Warumi 10:15 "Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!"
➡️Jitahidi kuwa kama Eliya aliyeona wivu kwa ajili ya watu kumwacha MUNGU na kuanza kuabudu miungu.
1 Wafalme 19:10 "Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya BWANA Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu, waiondoe."
Asante kwa kujifunza Neno la siku ya leo, Kabla sijamaliza nakuomba Wewe ambaye hujaokoka au uliokoka ukarudi nyuma, nakusihi sana amua Leo kumpokea YESU KRISTO kama Mwokozi wako na Jina lako litaandikwa katika kitabu Cha uzima Mbinguni, katika maeneo Yako tafuta Kanisa safi la kiroho linalohubiri Wokovu wa KRISTO YESU nenda kamweleze Mchungaji atakuongoza Sala ya Toba utaokoka Kisha baada ya hapo fuata mafundisho ya Neno la MUNGU hapo Kanisani.
MUNGU wa Mbinguni akubariki sana.
By Mwl Peter Mabula
Mtenda kazi katika Shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi.
+255714252292 ( kwa Ushauri, maombezi, pamoja na Whatsapp)
Ubarikiwe

Comments